Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

KUHANGAIKA KUPUNGUZA MAGUMU YA DUNIA KWA KUKADIRIA MABAYA ZAIDI YANAYOWEZA KUTOKEA

 Faida

 

 i.       Kuhangaikia kupunguza magumu ya Dunia kwa kukadiria mabaya zaidi yanayo weza kutokea:

         Na katika jumla ya sababu za kuondosha wahaka, huzuni, shaka, wasiwasi na jakamoyo pale mja anapo sibiwa na majanga ya Dunia. Ni mja huyo kuhangaika kuyapunguza  na kuyaona hafifu, kwa kukadiria mabaya zaidi yanayo weza kumtokea kuliko hayo yaliyo msibu na aifunge nafsi yake juu ya hilo. Atakapo fanya hivyo, basi na ajishughulishe kuyapunguza yale yanayo mkinika kuyapunguza kwa kadiri ya imkani. Basi kwa ufungaji huo wa nafsi na muhangaiko huo wenye manufaa, huondoka wahaka na jakamoyo lake. Na kunakuwa kutoa juhudi hiyo katika kuvuta/kuleta manufaa na katika kuondosha madhara, ni jambo jepesi kwa mja.

Zitakapo mshukia mja sababu za khofu, maradhi, ufakiri na kukosa avipendavyo miongoni mwa vipendwa mbali mbali. Basi na ajikinge na hilo kwa kuwa na utulivu na aifunge nafsi juu ya utulivu huo. Kwani hakika kuifunga nafsi juu ya uwezekano wa kutokea kwa magumu, kunayafanya magumu hayo kuwa mepesi na hivyo kuondosha dhiki iletwayo nayo. Na khususan pale atakapo ishughulisha nafsi yake kuyaondosha kwa kadiri ya uweza wake. Basi kwa ajili hiyo hukusanyika kwa upande wake ufungaji wa nafsi pamoja na juhudi nufaishi ambayo humfanya kuacha kuyashughulikia masaibu na majanga. Na ailazimishe nafsi yake kuzifanya mpya kila mara nguvu zake za kupambana na magumu ya maisha. Pamoja na kumtegemea Allah katika hili na kuwa na imani njema kwake kuwa anaweza kila kitu.

Na wala hapana shaka yoyote kwamba mambo haya yana faida yake kubwa katika kupatikana kwa furaha na ukunjufu wa moyo. Pamoja na yale anayo yatarajia mja miongoni mwa thawabu za Dunia na Akhera. Na hili ni jambo lionekanalo dhaahiri katika maisha yetu ya kila siku na limethibiti kiamalia kwa baadhi yetu.

 

 j.       Nguvu ya moyo na kutokuuzonga kwa wahaka:

         Na miongoni mwa dawa kubwa kabisa za maradhi ya moyo bali pia na maradhi ya mwili, ni kuwa na nguvu ya moyo na kutokuuzonga na kuushakizia mawazo na taswira mbaya ambazo huletwa na fikra mbaya. Kwa sababu mwanaadamu atakapo jisalimsha kwa taswira na moyo wake ukashakizika kwa viathiri miongoni mwa khofu, maradhi, ghadhabu na tashwishi za visababishi machungu. Na kutazamia kutokea kwa magumu na kuondoka kwa vipendwa nafsi, hilo litamtumbukiza katika wahaka, jakamoyo na wasiwasi na maradhi ya moyo na mwili.

Na pindipo moyo utakapo tawakali na kumtegemea Allah na wala usijisalimishe kwa fikra mbaya, wala usimilikiwe na taswira mbovu, ukamuamini kidhati Allah na ukazitumai fadhila zake. Huondokwa na wahaka, wasiwasi na jakamoyo na huondokwa na mengi miongoni mwa maradhi ya moyo na mwili. Na hupata nguvu, ukunjufu na furaha ambayo hakumkiniki kuielezea.

Ni hospitali nyingi zimesheni wagonjwa waathirika wa mawazo mabaya au yaliyo pindukia mpaka na fikira potoshi. Na ni mara nyingi sana mambo haya yameathiri nyonyo za watu wenye nguvu za kimaada na kimaana, seuze watu wanyonge. Na ni mara nyingi tu mawazo yamepelekea wadau wake kuangukia katika lindi la upite na uwenda wazimu! Na msalimika ni yule aliye opolewa na Allah na akamuwafikisha kupigana jihadi na nafsi yake ili kupata sababu nufaishi zenye kuutia moyo nguvu, zenye kuondosha wahaka wake. Allah Atukukiaye amesema: “...NA ANAYE MTEGEMEA ALLAH YEYE HUMTOSHA...” [65:03] Kwa mantiki hiyo basi, mwenye kumtegemea Allah ni mtu mwenye moyo thabiti usio athiriwa na fikra/mawazo mabaya na wala hatikiswi na vituka/vizuka. Hili ni kwa sababu ya kujua kwake kwamba huo ni udhaifu wa nafsi na khofu ambayo haina hakika. Na pamoja na hivyo, anajua kwamba Allah amekwisha chukua dhamana kwa yule atakaye mtegemea Yeye, kumtosheleza na kumtoshea kuliko timia. Basi yeye na amuamini kidhati Allah na aiyakinishe ahadi yake hiyo. Hapo utaondoka wahaka wake na jakamoyo lake na uzito wake utageuka kuwa wepesi na khofu yake kuwa amani.

Katika kauli yake Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Muumini mwanaume asimchukie muumini mwanamke, akiichukia kwake tabia moja, atairidhia kwake tabia nyingine”. Kuna faida mbili kubwa:

FAIDA YA KWANZA: Kuna muongozo/maelekezo ya namna ya kuamiliana na mke, ndugu, rafiki, mwenzi katika shughuli na kila ambaye mna mahusiano ya namna fulani baina yenu. Kwamba inakupasa uwe makini na yakini ya kuwa yeye kama binaadamu ni lazima atakuwa na aibu/kasoro/mapungufu au jambo unalo lichukia. Utakapo lichomozea na kulikuta hilo, basi hapo linganisha baina ya kasoro hiyo na ile nguvu ya mahusiano na ubakiaji wa mapenzi unao kuwajibikia. Ulinganishe kwa kukumbuka mazuri aliyo nayo na makusudio khususi na yale enevu. Kwa njia hii ya kuyafumbia macho makosa/mapungufu na kuyaangalia mema/mazuri, hudumu ule usuhuba/muambatano na yale mafungamano na raha hutimia na kupatikana kwako.

FAIDA YA PILI: Kunapatikana kuondoka kwa jakamoyo na wasiwasi na kunabakia utakaso wa moyo na kupatikana kwa raha na amani ya moyo baina pande zote mbili.

Mtu ambaye hakuongozeka na muongozo huu wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-bali akaligeuza suala hili. Akayaangalia makosa/mapungufu na kuyapa upofu mema/mazuri, huyo ni lazima utampata wasiwasi. Na hapana shaka mahusiano yake na wale anao fungamana nao na hivyo kusababisha kukatika kwa haki nyingi ambazo zinamlazimu kila mmoja wao kuzichunga.

Na wengi miongoni mwa watu wenye hima za juu wanazidhibiti nafsi zao wakati wa kutokea kwa majanga na mazonge, kwa subira na utulivu. Lakini wakati wa mambo mepesi ya hovyo wanapatwa na jakamoyo na kukosa amani ya moyo. Sababu ya hili ni kwamba wao wamezidhibiti nafsi zao katika mambo makubwa na kujisahau katika mambo madogo. Basi kwa ajili hiyo, hayo madogo waliyo yadharau yakawadhuru na kuathiri amani ya mioyo yao na hivyo kuziharibu raha zao. Kwa hivyo basi mtu makini mwenye akili kunjufu, ni yule anaye idhibiti nafsi yake na kuifanya imara juu ya mambo madogo na yale makubwa. Na si hivyo tu, bali anamuomba Allah Mola Mlezi wake msaada juu ya hayo makubwa na madogo yanayo msibu katika mchakato mzima wa maisha yake katika ardhi hii ya Manani. Na amuombe asimtupe mkono japo kwa kitambo cha upepesi wa jicho, basi wakati huo ndipo yatakapo kuwa mepesi kwake madogo kama yalivyo kuwa mepesi kwake makubwa. Naye atabakia kuwa mtulivu wa nafsi, mwenye amani ya moyo na mwenye raha ya maisha.

 

  



 | Tuandikie |