|
m)
Kujua kwamba maisha
ya mafanikio ni mafupi sana:
Mtu mweledi anajua kwamba maisha yake ya sawa
sawa, maisha ya mafanikio na utulivu, ni maisha mafupi sana. Kwa hivyo
basi, kwa kuukiri na kuujua ukweli huu, anajua ya kwamba haitakikani
kwake kuzidi kuyafupisha kwa kuwa na wahaka/huzuni na jakamoyo. Kwani
yote hayo ni kinyume na maisha ya sawa sawa, kwa ajili hiyo huionea
unyimi sehemu kubwa ya maisha yake kuporwa na wahaka/huzuni/jakamoyo. Na
katika hili hapana tofauti baina ya mja mwema na yule aliye muovu.
Lakini muumini yeye katika wasifu huu, ana fungu toshefu la Duniani na
Akhera.
Na pia inatakikana mja atakapo patwa na la kuchukiza au
akachelea kupatwa nalo, yeye kulinganisha baina ya baki ya neema
zipatikanazo kwake, zile za kidini na zile za kidunia. Na baina ya yale
machukivu yaliyo mpata, katika huo mlinganisho utamdhihirikia wingi wa
neema alizo nazo na hivyo kumezwa kwa machukivu yaliyo msibu. Nae akawa
mwepesi mno wa fuadi na bali na hivyo kuyaepa kabisa madhara ambayo
yangeweza kumpata kutokana na wahaka/jakamoyo.
Na hali kadhalika alinganishe baina ya madhara anayo
yachelea kumtokea na baina ya imkani nyingi za kusalimika na mabaya
hayo. Kwa mantiki hii basi, asiiache imkani dhaifu kuzishinda imkani
nyingi zenye nguvu. Kwa kufanya hivi, utaondoka wahaka/huzuni/wasiwasi
na jakamoyo lake. Na akadirie imkani kubwa kabisa ambazo kuna uwezekano
wa kumsibu, basi aifanye makini na kuituliza nafsi yake kwa ajili ya
kutokea kwake ikiwa yamekadiriwa kutokea. Na ajishughulishe kuondosha
yale ambayo hayajatokea na kuyaondosha au kuyapunguza yale yaliyo kwisha
tokea.
Na katika jumla ya mambo nufaishi, ni wewe kujua kwamba
maudhi ya watu wanayo kufanyia khususan kauli zao chafu, hayakudhuru
wewe bali huwadhuru wao wenyewe. Yatakudhuru tu iwapo utaishughulisha
nafsi yako kuyajali na kuyapa nafasi ya kuzimiliki hisia zako. Basi ni
wakati huo ndipo yatakapo kudhuru kama yanavyo wadhuru wao. Lakini ikiwa
wewe hutayajali, basi hayatakuwa na upenyo wa kukudhuru kwa lolote.
Na utambue ya kwamba maisha yako yanafuata fikra zako,
basi zikiwa fikra hizo ni katika yale ambayo manufaa yake huirejea dini
au Dunia, basi maisha yako yatakuwa ni mazuri yenye kunadi saada
(mafanikio ya kweli). Na kama fikra zako hazitakuwa hivyo, basi hapana
shaka kwamba hali itakuwa kinyume na hivyo.
Na miongoni mwa sababu za kuondosha wahaka/huzuni, ni
wewe kuimakinisha nafsi yako kutokutaka shukurani ila kwa Allah. Kwa
hivyo usijali wala kulazimisha kushukuriwa na yule uliye mtendea wema.
Kama alivyo sema Allah Atukukiaye kwa upande wa waja wake makhsusi:
“HAKIKA SISI TUNAKULISHENI KWA WAJIHI WA ALLAH. HATUTAKI KWENU MALIPO
WALA SHUKRANI”. [76:09] Na hili linakokotezeka zaidi katika muamala wa
wake na watoto na wale ambao una mafungamano nao ya karibu. Basi wakati
wowote utakapo imakinisha nafsi yako juu ya kuwaondoshea shari/madhara,
hapo utakuwa umejiondoshea shari wewe mwenyewe na utakuwa umejipumzisha.
Na katika jumla ya vileta raha na amani ya moyo, ni wewe
kuyaweka mbele ya macho yako mambo yenye manufaa na tenda amali katika
kuyatekeleza. Na wala usiyageukie mambo yenye kudhuru, ili kwa kufanya
hivyo upumbazike na sababu zenye kuleta wahaka/huzuni na wasiwasi na
jakamoyo.
Na miongoni mwa mambo yenye manufaa, ni wewe kuzimaliza
kazi/amali zako katika wakati huo na kuwa na faragha katika wakati ujao.
Kwa sababu kazi kama zitakuwa hazikumalizwa, zitakurundikia kazi zilizo
tangulia na hizi za sasa na hivyo kuwa mzigo mzito usio bebeka juu yako.
Lakini utakapo kimaliza kila kitu kwa wakati wake, utayaingia mambo
yajayo kwa nguvu ya fikra na nguvu ya kazi.
Na inatakikana uchague na kuteua katika matendo/kazi
nufaishi, ile yenye umuhimu mkubwa kuliko zote, kisha inayo ifuatia hiyo
na kama hivi kwa mpango huu. Na upambanue baina ya ile inayo pondokewa
na kupendwa zaidi na nafsi yako. Kwani kinyume chake husababisha uchovu,
ukimwa na maharibiko. Na jisaidie juu ya hilo kwa kuleta fikra sahihi na
kuomba ushauri, kwani katu hakujuta aliye omba ushauri. Na ukistadi kwa
makini unacho taka kukifanya, utakapo thibitisha kuwa kina manufaa na
ukaazimia kukitenda, basi hapo mtegemee Allah, kwani hakika Allah
anawapenda wamtegemeao.
Mpendwa msomaji wetu-Allah akurehemu-kwa auni na taufiq
yake Allah, mfululizo wa makala: NJIA FAIDISHI KWA MAISHA YENYE
MAFANIKIO, umetamatia. Tunamshukuru Allah kwa ukamilifu na tunamuomba
maghufira kwa mapungufu. Tumuombe Allah atuwafikishe kukutana juma
lijalo katika mfululizo wa makala mpya.
|