|
Hakika haya ni muhimili wa kheri na ni elementi katika kila
tendo linalo ichafua, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema:
“Uchafu haukuingia katika kitu ila hukitia towa na haikuwa haya
katika kitu ila hukipamba kitu hicho”. Tirmidhiy-Allah amrehemu.
Lau
haya ingeli jivika kiwiliwili ikawa mtu, basi angeli kuwa (mtu huyo) ni
nembo ya wema na utengenevu. Imepokewa kutoka kwa Bibi Aysha-Allah
amuwiye radhi-ya kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alimwambia: “Lau haya ingeli kuwa ni mtu, basi angeli kuwa
ni mtu mwema. Na lau kuwa uchafu ungekuwa ni mtu, basi angeli kuwa ni
mtu muovu/mbaya”. Twabaraaniy-Allah amrehemu.
Na
katika jumla ya mtu kuwaonea haya watu, ni kuzijua daraja za wenye haki
na kumpa kila mwenye kustahiki heshima, heshima yake. Kwani anao kijana
kwa wale walio mzidi umri na anao mwanafunzi kwa waalimu zake, mwenendo
unao simama juu ya msingi wa kuwa na adabu na utangulizi. Basi si vema
na wala haipendezi yeye (kijana) kuinua sauti yake mbele yao na wala
asipige hatua mbele yao (asiwatangulie katika kutembea). Imepokewa
katika hadithi: “Nyenyekeeni kwa yule mnaye jifunza kwake”.
Twabaraaniy-Allah amrehemu.
Kadhaalika katika hadithi nyingine: “Ewe Mola wa haki! Ninakuomba
zisinidiriki zama ambazo humo hafuatwi anaye jua na wala hastahiwi humo
mtu mpole”. Ahmad-Allah amrehemu.
Na haya
si uwoga, kwani mtu mwenye haya mara nyingine huweza kuona bora kumwaga
damu yake kuliko kumwaga maji ya uso wake (machozi). Na huo ndio ushujaa
katika taswira yake ya juu kabisa. Na pengine ikiwepo katika haya
sehemu/kitu katika khofu, pamoja na kwamba hiyo inaweza ikawa ni khofu
ya mtu bora kuchelea tabia zake njema na sifa zake bora,
kuondoshwa/kupotezwa na mazingira hatarishi. Na khofu/uchelea wa aina
hiyo ni mkabala wa ujasiri katika sehemu zake unamotakiwa na kusifiwa.
Pale
zamani Mayahudi walipo rudi nyuma wasiende kupigana na wale walio
takabari katika ardhi takatifu: “WATU WAWILI MIONGONI MWA WACHAMNGU
AMBAO ALLAH AMEWANEEMESHA, WALISEMA: WAINGILIENI KWA MLANGONI. MTAKAPO
WAINGILIA BASI KWA YAKINI NYINYI MTASHINDA...”. [05:23] Basi hawa ambao
wanao mcha Mungu na wanaogopa aibu/fedheha na wanaona haya kutimua mbio,
hao ndio ambao lau vita vitatokea, wangeli ongoza hujuma dhidi ya adui
na kuukurubisha ushindi.
Na wala
hapana shaka kwamba haya iliyo kamilika, hutanguliwa na maandalizi
maumbile yaliyo tayari. Kwani ziko tabia nyingi ambazo ufedhuli/usafihi
unakurubia kuwa ni sehemu yake iliyo lazimiana nazo. Katika wakati
ambapo unamuona mtu fulani ni mwingi wa soni, dhaifu wa hisia kwa
kiwango kikubwa. Lakini hizo soni, pamoja na ukweli kwamba ni elementi
inayo jitokeza kupitia haya, inapatikana katika kheri (wema) na shari
(uovu). Na pengine inaweza kumtumbukiza mdau wake kwenye mashaka/shida
na hali ngumu. Ama haya, basi haiwi ila ndani ya wigo wa mipaka ya
sheria, kwa mantiki hiyo basi yule anaye ogopa kuwakosoa na kuwakemea
wafanyao ya batili, huyo hazingatiwi kuwa ni mtu mwenye haya. Kwani
hakika haya ya kweli, haiwi kwenye upande wa batili na wala haina nafasi
kwa watu pindi wanapo potea. Na wala haina nafasi katika nyenendo pale
anapo kuwa mtu mahala akiinusuru haki hapo. Washirikina walipata
kuukosoa Uislamu eti ya kwamba umeyadharau masanamu na ukayafedhehesha
kwa kushindwa kwake hata kuumba nzi, tena si tu huko kuumba nzi bali
hata kushindwa kujihami pale yanapo shambuliwa na nzi. Wakasema: Hakika
hali ilivyo si sehemu ya haya kushambuliwa miungu yao kwa mtindo huo.
Hapo ndipo ikashuka kauli yake Allah Ataadhamiaye: “HAKIKA ALLAH HAONI
HAYA KUTOA MFANO WA MBU NA ULIO WA ZAIDI YAKE. AMA WALE WALIO AMINI
HUJUA YA KWAMBA HIYO NI HAKI ILIYO TOKA KWA MOLA WAO MLEZI, LAKINI WALE
WALIO KUFURU HUSEMA: NI NINI ANALO KUSUDIA ALLAH KWA MFANO HUU?...”
[02:26]
Kwa
hivyo basi, kudhihiri kwa masanamu katika sura hii ya ajizi (ushindwa)
na uduni ni haki: “...LAKINI ALLAH HASTAHI KWA JAMBO LA HAKI...”.
[33:53]
Na
katika njia ya kuthibitisha haki, muislamu hamuogopi yeyote na wala
hachelei ubaya. Na haya katika daraja zake za juu na tukufu kabisa,
inakuwa kwa Allah Ataadhamiaye, kwa hivyo sisi basi, tunakula katika
kheri zake na tunapumua katika anga lake na tunatembea kwenye ardhi yake
na tunafunikwa na mbingu yake. Na mtu kwa mkabala wa neema (wema) ndogo
anaona haya kumtendea ubaya aliye mneemesha neema hiyo. Basi iweje watu
wasione haya kumtenda ubaya Mola Muumba wao ambaye zinawafunika neema
zake tangu utotoni mpaka mwanandanini na kwenye maisha baada ya hapo ya
milele?!
Hakika
haki za Allah kwa waja wake ni kubwa mno, lau waja wangeli zipa haki
yake stahiki, basi wangeli ziendea haraka kheri kuzitenda kwa utashi
wao. Na wangeli kaa mbali na maasi kwa kuona haya kwa kuzikabili kheri
tupu kwa upingaji na uduni. Imepokewa kutoka kwa Ibn Masoud-Allah
amuwiye radhi: Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema:
“Muoneeni haya Allah haki ya haya, tukasema: Ewe Mtume wa Allah! Hakika
sisi tunamuonea haya Allah – tunamshukuru Allah (kwa hilo) – (Mtume)
akasema: Huko siko kumuonea haya Allah, haki ya haya ni kuhifadhi kichwa
na kilivyo navyo, tumbo na lililo vibeba na ukumbuke kufa na
kuchakafuka. Na aitakaye Akhera, huacha pambo (starehe) la maisha ya
Dunia na akaifadhilisha Akhera kuliko Dunia. Atakaye yafanya hayo,
hakika huyo ndiye amemuonea Allah haya haki ya haya”.
Tirmidhiy-Allah amrehemu.
Mawaidha haya – ambayo inasemekana ni ya Ibn Masoud – yamekusanya nyingi
miongoni mwa adabu za Uislamu na njia za maadili. Kwani ni wajibu wa
muislamu kuuepusha ulimi wake kuingia kwenye batili, na ayazuie macho
yake kuona tupu au kutazama matamanio. Na sikio lake aliepushe kuiba
siri au kufichua ubaya. Na ni juu yake kuliachisha haramu tumbo lake na
alikinaishe na kilicho kizuri (cha halali) kipatikanacho. Kisha tena
ajilazimishe kuutumia wakati wake katika yanayo mridhi Allah na
kuzifadhilisha thawabu zilizoko kwake. Basi zisimdunishe starehe
zihadaizo za Dunia, akiyafanya hayo kwa hisia kwamba Allah anamuona na
kwa kukimbia kuchupa mipaka upande wa Allah, bila ya shaka huyo atakuwa
amemuonea haya haki ya haya.
Hakika
kutetemeka kwa mtu na kubadilika kwa rangi ya uso wake katika baadhi ya
hali, ni dalili ya utukufu ulio jificha na tabia njema, na “haya ndio
kheri yote”. Ama pale itakapo ondoka rangi na pako la haya usoni mwa
mtu, kama linavyo dondoka gamba/gome bichi la mti mbichi. Hapo huwa haya
imetoa rukhsa ya kuondoka kwa maadili mema na mtu huyo ndiye aambiwaye:
“Usipo stahi (usipo kuwa na haya), basi tenda utakalo”.
Bukhaariy-Allah amrehemu.
Na haya
kwa mjumuisho huu, ndio dini yote, inapo wekwa kwenye kundi la amali
njema, basi hiyo ni sehemu ya imani na ni athari yake. Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Imani ina mafungu sabini na
kadhaa, bora lake (mafungu hayo) ni kauli ya ‘Laa Ilaaha Illal-laah’ na
la chini yake ni kuondosha udhia njiani. Na haya ni sehemu ya imani”.
Muslim-Allah amrehemu.
Hakika
mwanaadamu mbele ya watu anao waheshimu, huwania kuwaridhi na hudhibiti
mwenendo wake kikamilifu. Kwa sababu hiyo basi, huzungumza kwa heshima
na huwa na hadhari katika matendo yake. Na kwa muktadha huo basi,
muislamu anaye jua kupitia mafundisho ya dini yake ya kwamba katu yeye
haghibu (hatoweki) kwenye uoni wa Allah, kwani Yeye yu pamoja naye
katika hali zake zote, mchana na usiku. Kunampasa khofu yake kwa Allah
iwe ni kubwa mno, na kuwa na adabu na sheria zake kwa ukamilifu mkubwa. |