Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

SOMO LA TATU

Faida

i/. SUBIRA NA KUSTAHAMILI MAUDHI.

Miongoni mwa tabia nzuri na njema ambazo muislamu hujipamba nazo ni kuwa na subira na kustahamili maudhi. Tusite hapa na tujiulize kabla hatujaendelea, subira ni nini? Kwa ibara nyepesi yenye kufahamika haraka tunaweza kuiarifisha subira kuwa ni hali ya mtu kuizuia nfsi yake dhidi ya ayachukiayo. Tuliweke wazi ainisho na arifisho hili, muislamu mathalan huizuia nafsi yake dhidi ya iyachukiayo. Inaeleweka wazi kwamba nafsi inachukia na haipendi ibada na mambo ya twaa na badala yake humvutia mtu kwenye maasi, uonvu na uchafu kwani ndio maumbile yake: “--- KWA HAKIKA (kila) NAFSI NI YENYE KUAMRISHA SANA MAOVU ISIPOKUWA ILE AMBAYO MOLA WANGU AMEIREHEMU ---“ [12:53]

Muislamu huilazimisha na kuondosha nafsi katika maumbile yake haya ya kupenda maovu na kuipeleka katika twaa, haipi kabisa nafasi ya kuyakurubia maasi ambayo hujidhihirisha katika sura nzuri yenye kuvutia na ladha tamu yenye kutamanisha na kutia uchu. Kadhalika huizuia kupapatika inapofikwa na balaa na majanga mbalimbali. Silaha pekee anayoitumia muislamu katika vita vyake hivi vigumu ni SUBIRA inayomuwezesha kusubiria ladha ya maasi na kumeza shubiri ya njema aitoayo Mola wake ikiwa ni mkabala wa twaa wazitendazo waja wake. Kamio la Allah la ahabu kali itakayowafika watendao maasi pia hutoa mchango mkubwa kwa muislamu katika vita yake hii dhidi ya nafsi yake. Muislamu anakumbuka kwamba daima qadari ya Allah ni yenye kupita; haipingwi na wala hina kuzizi, hukumu yake ni ya uadilifu; isiyo na dhulma wala upendeleo kwa ye yote. Mwanadamu akisubiri au akipapatika itapita tu, kwa hivyo ni vema asubiri ili apate ujira mkubwa kwani kupapatika kwake hakutamaanisha kingine zaidi ya kupata dhambi na hukumu ya Allhah kubakia pale pale.

Subira na kutokupapatika wakati wa majanga mbalimbali ni miongoni mwa tabia ambazo ni zao la mazoezi na mapambano ya muda mrefu yaendeleayo muda wa maisha ya mtu. Muislamu humuomba Mola wake amruzuku subira akiamini kuwa anaitekeleza amri ya Mola wake isemayo: “ENYI MLIOAMINI! SUBIRINI NA MUWASHINDE MAKAFIRI (katika kusubiri) NA KUWENI. IMARA (nyoyo zenu) NA MCHENI ALLAH ILI MPATE KUFAULU.” [3 : 200]

Aya inabainisha kwamba subira ni sifa ya waumini hawi na subira ni alama ya kufaulu. Pia anaitekeleza amri isemayo: “ENYI MLIDAMINI! JISAIDIENI (katika mambo yenu) KWA SUBIRA NA SWALA; BILA YA SHAKA ALLAH YU PAMOJA NA WANAOSUBIRI.” [2 : 153]

Hapa pia inatubainikia kwamba subira na swala vina mchango na msaada mkubwa katika kuyafanikisha mambo yetu mbalimbali katika harakati za maisha yetu  ya kila siku. Wenye subira wako pamoja na Mola wao aliyewataka kuwa na subira nao wakamtii wakasubiri, kwa ajili hiyo akawaahidi msaada wake katika shughuli na mambo yao yote. Katika kusubiri kwake, muislamu huitia matendoni amri ya Mola wake: “NA SUBIRI, NA KUSUBIRI KWAKO KUSIWE ILA KWA AJILI YA ALLAH TU ---.” [16 : 127]

Tunafahamikiwa kutokana na aya hii kwamba ili subira itoe matunda mema ni lazima muislamu ahakikishe kwamba subira yake ni kwa ajili tu ya kutarajia kupata radhi na ujira wa Allah tu na si vinginevyo: “--- NA KWA YAKINI SISI TUTAWAPA WALIOSUBRI UJIRA WAO (Mkubwa kabisa) KWA YALE MAZURI WALIYOKUWA WAKIYATENDA.” [16 : 97]

Hebu ione thamani na kima cha subira kupitia kauli hii tukufu ya mtukufu Mtume wa Allah Rehema na Amani zimshukie isemayo: “Na atakyejizuia na machafu, Allah atamuwezesha kujizuia nayo, na atakayejikwasia  na kuomba (watu), Allah atampa ukwasi, na atakayesubiri, Allah atamsubirisha. Na hajapewapo ye yote kipawa kilicho bora na kikunjufu kuliko subira.” Bukhaariy

Hii ndio subira tunayoikusudia au ikusudiwayo na uislamu. Ama kustahamili maudhi pia ni sehemu ya subira iliyo ngumu zaidi kwa wanadamu wengi. Kustahamili maudhi ndio bidhaa ya masadiki na ndio nembo ya watu wema. Ukitaka kuwajua na kuwafahamu watu wema, basi zitizame hali zao wanapoudhiwa, utaona ni namna gani wanavyoziangusha mweleka nafsi zao katika kukabiliana na maudhi watendewayo. Kustahamili maudhi hudhihiri pale muislamu anapoudhiwa na kubughudhiwa kwa ajili ya Allah, hapo akaonysha subria na uvumilivu wake. Mfano mzuri wa kupigwa na kuigwa katika hili ni mtume wa Allah Rehema na Amani zimshukie. Namna makurayshi walivyomfanyia maudhi yasiyohimilika kwa ajili ya kuwafikishia ujumbe wa Allah. Malaika wanatumwa na Allah kuja kutoa msaada, wanamtaka idhini Bwana mtume ya kuwaangamizia mbali watu wabaya wale. Ndugu yangu muislamu unafikiri mtume wako alifanya nini. Anamuelekea Mola wake na kumuomba awasamehe waja wake badala ya kuwaombea na kuwaidhinishia adhabu na maangamivu. Hapo ndipo malaika Mkuu jibril Amani ya allah imshukie anampa Mtume wa Allah shahada na tuzo ya juu ya uvumilivu anamwambia: “Amesema kweli aliyekuita MPOLE MWENYE HURUMA.”

Katika kustahamili maudhi, muislamu haulipi ubaya aliotendewa kwa ubaya bali hulipa uovu kwa wema ikiwa ni kulitekeleza agizo la Mola wake: “ONDOSHA MABAYA (unayofanyiwa) KWA (kulipa) MEMA ---.” [23 : 96]

Na lile lisemalo: “MAMBO MAZURI NA MABAYA HAYAWI SAWA ONDOSHA (Ubaya unaofanyiwa kwa mema); TAHAMAKI YULE AMBAYE BAINA YAKO NA YAKE KUNA UADUI ATAKUJA KAMA NI JAMAA (yako) MWENYE KUKUFIA UCHUNGU.”[41 : 34]

Jifunze kustahamili maudhi kupitia tukio hili lililomtokea Bwana Mtume Rehema na Amani zimshukie siku moja Mtume wa Allah aliwagawia maswahaba mali iliyopatikana vitani. Mmoja wa mabedui (waliokuwepo hakuridhika na mgao ule alioupata) akasema: Mgao huu haukukusudiwa dhati ya Allah {Mtume kafanya upendeleo}. Habari zile zikamfikia Mtume wa Allah, akageuka na kuwa mwekundu {kutokana na mtambao wa ghadhabu na hasira}. Kisha akasema: Allah amrehemu ndugu yangu Mussa alifanyiwa maudhi makubwa kuliko haya na akasubiri {nami nasubiri},” Bukhaariy na Muslim. Huyu hapa Mola wetu akitusimulia ustahamilivu wa Mitume wake Rehema na Amani ziwashukie kutokana na maudhi waliyoyapata kutoka kwa watu wao katika kuwafikisha ujumbe wa Mola wao: “NA TUNA NINI TUSIMTEGEMEE ALLAH, NA HALI AMETUONYESHA NJIA ZETU NA TUTAYAVUMILIA MNAYOTUUDHI BASI KWA ALLAH TU WATEGEMEE WATEGEMEAO.” [14 : 12]

Nabii Issa mwana wa Mariam Amani na Rehema iwashukie alikuwa akiwaambia wana wa israil: “Mliambiwa hapo kabala (yangu katika Taurati) kwamba jino (hung’okwa) kwa jino na pua (hukatwa) kwa pua. Nami sasa ninakuambieni msikabiliane na shari (ubaya) kwa shari, bali atakayekupiga shavu lako la kulia wewe mgeuzie shavu la kushoto. Na atakayekutwalia mtandio wako, wewe mpe na shuka yako.” Imam Ghazaali katika IHYAAD ULUUMID DIYN.

Kustahamili maudhi ni mizani inayopima uzito wa imani ya mja. Baadhi ya maswahaba wa Mtume Allah awawiye radhi walikuwa wakisema: “Tulikuwa hatuihisabu imani ya mtu kuwa ni imani kama hakuyasubiria maudhi.” Kupita mifano hai hii yenye kujieleza na kujitafsiri yenyewe ya subira na ustahamilivu wa maudhi, muislamu anatazamiwa aishi maisha ya subira na ustahamilivu huku akitaraji radhi na maghufira adhimu kutoka kwa Mola wake. “NA ANAYESUBIRI NA KUSAMEHE (atalipwa wema wake.) BILA SHAKA HILO NI KATIKA MAMBO MAKUBWA YA KUAZIMIWA KUFANYWA (na kila muislamu)”. [42:43]


TUJIFUNZE NA TUKUBALI kuwa: “NA AMBAO HUSUBIRI (wakawashahamilia wenziwao) KWA KUTAKA RADHI YA MOLA WAO, NA WAKASIMAMISHA SWALA NA WAKATOA KATIKA VILE TULIVYOWAPA, (wakavitoa) KWA SIRI NA DHAHIRI, NA WAKAYAONDOA MAOVU KWA MEMA. HAO NDIO WATAKAOPATA MALIPO (mema) YA NYUMBA (ya Akhera). MABUSTANI YA MILELE WATAYAINGIA WAO (pamoja) NA WALIOFANYA WEMA MIONGONI MWA WAZEE WAO NA WAKE ZAO NA KIAZI CHAO. NA MALAIKA WANAWAINGILIA KATIKA MILANGO (wanawaambia): IWE AMANI JUU YENU (Salaamun Alaykum), KWA SABABU MLISUBIRI (mlistahamili katika kufanya mema na kuacha mabaya na mkastahamiliana mkakaa vizuri na wenzenu). BASI NI MEMA YALIYOJE MATOKEO YA NYUMBA (ya Akhera kwa wamchao Allah).” [13 : 22 - 24]


Forum | Guestbook | Tuandikie |