Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

B. HAKI ZA MUME                            Inaendelea

 Faida

8. Ni wajibu wa mke kumuheshimu mumewe heshima iliyochanganya huruma na upendo. Asimbughudhi mumewe kwa sababu tu ya uzuri au mali yake akiwa ni tajiri au ana hadhi kuliko mumewe huyo.

 

9. Mke anapaswa kuwa na huruma na nasaha njema kwa familia ili kuilinda dhidi ya mmomonyoko wa kimaadili. Asijenge mazoea ya kuwatukana na kuwalaani watoto, kwani hilo litawapelekea na wao kujengeka hivyo watakapokuwa baba/mama wa familia. Jambo dogo tu atakalofanyiwa na mumewe lisiwe ndio kifutio cha mema na mazuri yote aliyofanyiwa na mumewe huyo katika kipindi chote cha maisha yao. Ni lazima tukubali ukweli kuwa haya ni maumbile na tabia ya wanawake walio wengi. Kwamba kosa/jambo dogo tu la mumewe humfikisha kusema: (Mume gani wewe, tangu unioe sijaona jema lako hata moja, wewe nawe mwanamume katika wanamume!). Mambo haya hayafai kwani humsafishia mwanamke huyo njia ya kwendea motoni. Imepokelewa kwamba Mtume-Rehema na Amani zimshukie-aliwaona wanawake ndio akthari (wengi) ya watu wa motoni, akaulizwa sababu yake ni nini. Akajibu: “Wanakithirisha mno laana (wanalaanilaani mara kwa mara watoto kwa jambo dogo tu) na wanakanusha wema na ihsani ya mume”. Bukhaariy, Muslim & Ahmad.

Hizi kwa mukhtasari ndizo baadhi ya haki za mume kwa mkewe au wajibu wa mke kwa upande wa mumewe. Ni matumaini yetu kuwa kutokana na silsila (mlolongo) ya masomo haya wanandoa watakuwa kwa kiasi kikubwa wamezijua haki na wajibu wa kila mmoja wao kwa mwenziwe. Allah Mola Muumba jike na dume katika kila kitu atuwafikishe kuwa waume na wake wema wenye kupigiwa mithali mahala tuishipo-Aaamiyn.

7. HAKI ZA VIONGOZI NA HAKI ZA RAIA (WAONGOZWA):

Ni maumbile ya wanadamu kukhitilafiana kifikra, kimawazo, kiufahamu na kiakili. Na mara nyingi watu huongozwa na matamanio na matashi ya nafsi zao bila ya kujali sheria au haki za wenzao. Maumbile haya ya wanadamu ndio yanayowajibisha kuwepo kwa sheria zitakazowatawala na kuwahukumu. Na ili sheria hizi zifanye kazi na kuheshimiwa ni lazima yawepo mamlaka/nguvu itakayosimamia utekelezaji wa sheria hizi. Hapa ndipo inapojitokeza haja ya jamii yo yote ya wanadamu kuwa na kiongozi atakayekuwa na jukumu/dhima ya kuchunga maslahi ya uma kwa mujibu wa sheria iliyokubaliwa na kuridhiwa na jamii husika. Kama ambavyo ni wajibu wa raia (waongozwa) kuheshimu sheria, kadhalika ni wajibu wa kiongozi kuhakikisha kuwa sheria zinaheshimiwa kupitia mamlaka aliyopewa.

Ni wajibu wa kisheria bali ni sehemu ya dini, waislamu kumsimika (kumtawalisha) kiongozi wanayemkubali atakayewatawalia na kuwaratibia mambo yao kwa mujibu wa sheria ya Allah (Qur-ani) na Suna (hadithi za Mtume). Kunawawajibikia waislamu kumchagua miongoni mwao mtu anayefaa kubeba dhima ya uongozi wa uma. Kiongozi atakayechaguliwa na uma ni lazima awe ni muislamu kweli anayeujua Uislamu wake, mcha-Mungu, muadilifu, mwenye elimu ya sheria, uongozi na mahusiano ya kijamii. Suala la kumsimika kiongozi si suala geni katika historia ya jamii za wanadamu, na hii ni kutokana na umuhimu wa suala lenyewe kwa kila jamii. Katika Uislamu, uongozi/kuwa na kiongozi ni suala lililothibiti katika Qur-ani (sheria mama) na suna (sheria shereheshi). Tukiyapekua mabuku ya tarekh (historia) na sira, tutayakuta yametusajilia upelekaji wa vikosi vya vita alivyovituma Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-sehemu mbali mbali. Mabuku haya yanaonyesha kwamba Bwana Mtume hakukituma kikosi cho chote, kikubwa au kidogo ila alikisimikia kiongozi atakayekiongoza na akakiusia kumtii kiongozi wao. Kadhalika Bwana Mtume hakuuacha mji wo wote wa Kiislamu bila ya kuutawalishia Amiri kama tarekh inavyolithibitisha hilo. Kadhalika Mtume alipokuwa anaondoka nje ya Madinah kwa ajili ya kuongoza vita au kwa sababu nyingine, alimteua mmoja wa maswahaba wake kukaimu nafasi yake mpaka atakaporudi. Matendo yote haya ya Bwana Mtume ni ushahidi wa wazi unaoonyesha nafasi ya uongozi katika Uislamu na kwamba ni lazima jamii ya Kiislamu bali jamii ya wanadamu bila ya kujali itikadi/imani kuwa na kiongozi.

Uislamu kama dini na mfumo sahihi wa maisha ili kuhakikisha kuwa haki na uhuru wa kila mtu unalindwa kupitia sheria zinazosimamiwa utekelezaji wake na kiongozi aliyekubaliwa na kuchaguliwa na uma. Ili hili lifikiwe, Uislamu umeweka haki na wajibu baina ya kiongozi na raia (waongozwa). Kwa maneno mengine tunaruhusika kusema kuwa majukumu/wajibu wa kiongozi ndio haki za raia na wajibu wa raia ndio haki za kiongozi.

WAJIBU WA KIONGOZI/HAKI ZA RAIA:

Kiongozi akishachaguliwa ni wajibu apewe madaraka/mamlaka kamili kwa mujibu wa sheria bila ya kupingwa au kuingiliwa katika maamuzi/hukumu azitoazo maadam hazipingani na sheria. Raia nao wana wajibu wa kumuunga mkono na kumsaidia kiongozi wao katika kuitekeleza dhima/majukumu waliyompa. Miongoni mwa majukumu/wajibu muhimu wa kiongozi ni kama yafuatavyo:-

WAJIBU WAKE KWA UPANDE WA DINI WENYE MASLAHI KWA RAIA WAKE:

Miongoni wa wajibu mkubwa aliobebeshwa kiongozi mabegani mwake ni kusimamia, kuhifadhi na kuiendeleza dini. Ahakikishe kuwa anapanda mbegu ya mapenzi ya dini mioyoni mwa raia (uma) wake ili waweze kuzifuata kwa ukamilifu hukumu za dini. Ni wajibu wa kiongozi kuona kuwa mwenendo, silka, tabia na utamaduni wa dini ndio unaoitawala jamii (uma) yake. Kiongozi afunge mianya na milango yote inayoweza kuleta/kusababisha mmomonyoko wa maadili miongoni mwa raia wake. Akate mizizi ya tamaduni zote zinazopingana na sheria ya Allah na badala yake awajengee raia wake mazingira ya kuupenda, kuuthamini, kuujali na kuufuata utamaduni wa dini yao. Sambamba na kushikamana na mwendo (suna) wa Mtume wao. Kiongozi na jamii kwa ujumla itambue kuwa maovu na maasi yanayotapakaa katika jamii kwa kasi ya moto nyikani chini wa mwavuli wa kile kinachoitwa ‘kwenda na wakati’ na watu wakayazoea na kuyaona kuwa ni mema. Watambue kuwa hilo ni gonjwa hatari litakaloisambaratisha na kuiangamiza jamii. Njia na dawa pekee ya kulitibu na kuliangamiza gonjwa hili na kuiokoa jamii na athari yake ni kwa kiongozi kuhakikisha kuwa hukumu ya sheria inamuangukia kila mtenda maovu aendaye kinyume na sheria. Aadhibiwe na kutiwa adabu kwa mujibu wa sheria kulingana na kosa/dhambi aliyoitenda. Mbali na usimamiaji huu wa sheria, kiongozi anapaswa kuhakikisha kuwa raia wake wanaijua sheria sambamba na haki zao za kisheria bila ya kusahau wajibu wao. Raia waelimishwe mpaka watambue kuwa sheria na adhabu zitolewazo kufuatia makosa mbalimbali zimewekwa kwa maslahi yao kama uma. Sheria na adhabu hizi zina dhima kuu ya kuhifadhi na kulinda uhai, mali, dini, heshima na akili ya mtu. Jamii ikipata hifadhi na ulinzi wa vitu hivi ndipo watu wanaweza kuishi kwa amani. Na ni chini ya mwavuli huu wa amani na utulivu raia wataweza kuendesha shughuli zao za kila siku kwa ufanisi mkubwa ili kujiletea maendeleo yao binafsi na ulimwengu kwa ujumla. Ni katika mazingira haya ndipo watapata utulivu mkubwa utakaowawezesha kumuabuadu Allah Mola Muumba wao kwa unyenyekevu na utii. Watu waelewe kuwa kama kungelikuwa hakuna sheria na wasimamiaji wa sheria (viongozi), basi ulimwengu huu ungelikuwa ni ulimwengu wa samaki. Ambamo samaki mkubwa hummeza aliye mdogo na hakuna wa kumuuliza.

KUSIMAMISHA UADILIFU:

Kiongozi wa Kiislamu anatakiwa na Uislamu kutambua kwamba kuwafanyia uadilifu raia wake ni wajibu wake yeye. Na wao raia huo uadilifu wake ni haki yao ya kisheria waliyopewa na Allah, kwa hivyo hakuna wa kuwapokonya. Ahakikishe kuwa anatoa hukumu ya haki, isiyo na upendeleo kwa kigezo cho chote kiwacho baina ya mahasimu wawili waliofika mbele ya sheria. Achukue haki ya mdhulumiwa kutoka kwa dhalimu na kumpa huyo mdhulumiwa kwa namna anayostahiki. Watu wote wawe sawa mbele ya sheria, usiwepo kabisa mwanya wa upendeleo. Mfalme asipewe haki kwa sababu tu ya ufalme wake, sheria isipindwe kwa tajiri kwa kigezo cha utajiri wake na mnyonge asionewe kwa ajili tu ya unyonge wake. Ni wajibu wa kiongozi kuyasimamia yote haya kwa kuhakikisha kuwa uadilifu unakuwa juu ya utajiri, cheo na umaarufu wa mtu. Kiongozi akumbuke kuwa uadilifu ndio msingi mkuu wa haki na utawala bora unaoenziwa na wapenda haki wote bali na Allah. Kiongozi wa Kiislamu anatakiwa kujipangia utaratibu wa kusikiliza malalamiko na matatizo ya raia wake. Awe karibu sana na watu wake, ashirikiane nao na kuwaenzi katika dhiki na faraja kiasi cha kuwafanya wamuhisi na kumkubali kuwa ni mwenzao. Kiongozi muumini hatakiwi kujenga uzio baina yake na raia wake, akawa hana nafasi ya kukutana nao na kujua matatizo yao yanayowakabili, kwani kufanya hivyo ni kuwaghushi raia. Bwana Mtume, kiongozi muadilifu kuliko wote waliopata kuwepo na watakaokuwepo-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Hapana mja ye yote atakayepewa uongozi na Allah Mtukufu, akafa siku ya kiyama na il-hali amewaghushi raia wake ila Allah atamuharamishia pepo (kiongozi huyo ghashashi)”. Bukhaariy & Muslim.

Na akasema tena: “Ye yote atakayetawalishwa cho chote katika mambo ya waislamu, kisha asiwatumikie upeo wa juhudi yake na asiwape nasaha zake ila hataingia pamoja nao peponi”. Muslim

Na Allah Mola Mwenyezi anatuambia: “HAKIKA ALLAH ANAKUAMRISHENI KUZIRUDISHA AMANA KWA WENYEWE (wanaozistahiki) NA MNAPOHUKUMU BAINA YA WATU MUHUKUMU KWA HAKI...” [4:58]

KUKUBALI NASAHA NA USHAURI MWEMA WA RAIA WAKE:

Kiongozi wa Kiislamu hawi dikteta kama ambavyo hawi bendera akafuata upepo unakomuelekezea. Ni haki yao raia kama uma kumnasihi na kumpa kiongozi wao ushauri mzuri unaolenga kujenga na sio kubomoa. Na ni wajibu wa kiongozi kuukubali na kuupokea ushauri na nasaha hizo bila ya kinyongo. Pamoja na kukubali nasaha na kupokea ushauri, kiongozi anapaswa kuwa na chujio/chekecheo la kuchekechea nasaha na kuuchujia ushauri huo aliopewa na raia wake. Autupilie mbali ulio mbaya unaolenga kubomoa na aukumbatie na kuufanyia kazi ule ulio mzuri unaolenga kujenga na kudhamini maslahi ya uma. Kukubali nasaha na kutaka ushauri ni miongoni mwa nguzo za sheria ya Uislamu. Hebu tumuangalie Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-namna alivyokuwa akiusikiliza ushauri na kuukubali. Katika vita vya Badri, Mtume wa Allah alipiga kambi mahala fulani ili kukabiliana na mushrikina. Swahaba wake Al-Habaab Ibn Al-Mundhir-Allah amuwiye radhi-akamuendea Bwana Mtume na kumwambia kwa adabu: “Ewe Mtume wa Allah, unaionaje kambi hii, je ndio kambi aliyokushusha hapo Allah (kama ni hivyo) hakutufalii sisi kuhoji wala kupinga. Au hizi ni fikra (zako tu) na mbinu za vita? (Mtume) akamjibu: Bali hii ni fikra yangu (sio amri ya Allah) na mbinu za vita. Akasema (Al-Habaab): Ewe Mtume wa Allah, hakika hapa si mahala panapofaa kupiga kambi. Ondoka na watu twende mpaka tufike eneo lenye maji lililo karibu na watu (mahasimu wetu), tupige kambi hapo. Kisha tuzibe visima vyoye vilivyo nyuma yetu, kisha tujenge mahodhi ya maji na kuyajaza maji. Halafu ndio tuanze kupambana nao wakati ambapo sisi tutakuwa tuna maji ya kunywa na wao hawana. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Hakika umetoa rai nzuri” na akaifuata na kuikubali rai hiyo ya Al-Hubaab. Angalia Siyratu Ibn Hishaam.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa waislamu: “...WANASHAURIANA KATIKA MAMBO YAO...” [42:38]

Bwana Mtume anaagizwa: “...NA USHAURIANE NAO KATIKA MAMBO...” [3:159]


Forum | Guestbook | Tuandikie |