Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

9. HAKI ZA WAISLAMU WOTE KWA UJUMLA

 

Bila ya shaka kila mmoja wetu amepata kuliona jengo refu, imara na madhubuti, likampendeza na kumvutia kiasi cha kujikuta anasimama kulishangaa. Ni dhahiri kuwa jengo hili zuri ni natija ya msingi imara, nguzo madhubuti, kuta zilizoundwa na mkusanyiko wa matofali, vyuma vya pua na baki ya vifaa vingine vya ujenzi. Mkamatano na mshikamano wa matofali umezaa kuta imara, mkusanyiko wa kuta hizi ukazaa jengo zuri lililosimama juu ya msingi madhubuti usiotetereka ukiungwa mkono na nguzo thabiti. Ni kutokana na mchanganyiko na muungano wa vitu vyote hivi ndio likapatikana jengo imara na madhubuti likushangazalo. Huu ndio mfano wa uma wa Kiislamu kama jengo moja, madhubuti na imara. Kama unavyoelezwa na kauli ya Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Muumini kwa muumini mwenzie ni kama (mfano wa) jengo likamanatalo baadhi moja na nyingine.” Bukhaary, Muslim & Tirmidhiy. Matofali hapa ya kulijenga na kulisimamisha jengo hili juu ya msngi imara ni umoja, mshikamano na mapenzi chini ya udugu wa Kislamu. Sasa ni lazima vipatikane mchanga, saruji na maji ya kutengenezea matofali ya umoja mapenzi na mshikamano utakaowafikisha katika kuitekeleza amri ya Mola wao: “NA SHIKAMANENI KWA KAMBA (dini) YA ALLAH NYOTE NA WALA MSIACHANE (msitengane/msifarikiane)…..” (3:103)

Sasa basi ili kuwafikisha waislamu kuwa uma mmoja kama anavyowataka Mola wao: “KWA YAKINI HUU UMMA WENU NI UMMA MMOJA, NA MIMI NI MOLA WENU (mmoja) KWA HIVYO NIABUDUNI.” (21:92)

Na kuwafikisha kujihisi mwili mmoja kama alivyosema Mtume wao-Rehema na Amani zimshukie: “Mfano wa waumini katika kupendana kwao, kuhurumiana kwao na kuoneana kwao sikitiko ni mithili ya mwili mmoja. Kinapoumwa kiungo kimoja katika (mwili) huo, baki ya mwili hushirikiana nacho katika homa na kukesha .” Bukhaariy & Muslim

Ndio uislamu ukaweka haki za kila muislamu juu ya nduguye muislamu. Haki ambazo kama zitafuatwa na kila muislamu kama itakiwavyo, bila ya shaka zitakuwa na msaada mkubwa katika kuleta umoja, mapenzi na mshikamano baina ya waislamu. Haki hizi pia zina dhima ya kulinda na kuhifadhi umoja na mshikamano wa uma wa Kiislamu. Haki za muislamu kwa muislamu mweziwe ni nyingi mno, miongoni mwa hizo ni kama zinavyoelezwa na kauli ya Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie: “Haki za muislamu kwa muislamu ni sita:

  • Ukikutana nae mtolee salamu, na

  • Akikuita (akikualika) muitike,

  • Akikutaka nasaha/ushauri mnasihi

  • Akipiga chafya na akamuhimidi Allah, mshemue (mwambie “Yarhamukal-laah”),

  • Akiumwa mkague (mjulie hali) na

  • Akifa lifuate jeneza lake (kamzike)”.

Katika hadhithi hii Bwana Mtume anatubainishia haki kadhaa baina ya waislamu kama ifuatavyo:

 

SALAMU:

Muislamu anapompitia nduguye muislamu, anapomzuru au anapotaka idhini ya kuingia nyumbani au kazini kwake ni haki ya ndugu yake huyo kumtolea tamko la amani. Tamko litakalomuhisisha amani na kuituliza nafsi yake, kwa kumtolea salamu kwa tamko la: ASSALAMU ALAYKUM WARAHMATULLAAH. Hayo ndio maamkizi ya waislam leo duniani na kesho kule akhera: “…MAAMKIANO YAO HUMO YATAKUWA SALLAMUN ALAYKUM (za kila upande, yaani Amani tu juu yenu na furaha na salama).” (14:23)

Maamkizi haya ya kiislamu ni suna kokotezwa (muakadah) kama ilivyothibiti kutoka kwa Bwana Mtume. Na maamkizi haya ni katika jumla ya sababu za kuleta mshikamano, mtungamano na mapenzi baina ya waislamu kama umma. Hili linashuhudiwa na kauli yake Mtume wa Allah- Rehema na Amani zimshukie: “Wallah, hamtangia peponi mpaka muwe waumini na hamtakuwa waumini mpaka mpendane. Basi hivi nikuambieni jambo mtakapolitenda mtapendana, enezeni salamu baina yenu.” Muslim

Bwana Mtume ambaye anasifiwa na Mola wake: “NA BILA SHAKA UNA TABIA NJEMA KABISA.” (68:4)

Alikuwa akimuandiliza kwa salamu kila anayekutana nae, yaani anapokutana na mtu yeye ndiye huanza kumtolea salamu mtu huyo. Kadhalika hakuwapuuza watoto wadogo, bali ili kuwajengea mapenzi alikuwa akiwatolea salamu anapowapitia. Huyu ndiye Mtume ambaye Allah anatuambia: “BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA (ruwaza nzuri) KWA MTUME WA ALLAH (lakini mfano huo ni) KWA MWENYE KUMUOGOPA ALLAH NA SIKU YA MWISHO NA KUMTAJA ALLAH SANA.” (33:21)

Ilivyo suna katika salamu ni mdogo kuanza kumtolea salamu mkubwa wake na wachache wawatolee salamu walio wengi. Aliyepanda kipando (mnyama/gari n.k) amsalimu mwenda kwa miguu. Lakini iwapo mtu mwenye kuwajibika kutoa salamu hakuifuata suna hii ya Mtume, isiwe ni sababu ya kutokuamkiana. Huyu aliyekuwa na haki ya kuanza kusaliminwa, atoe salamu isipotee. Kwa hivyo itakaposadifu kuwa mdogo hakumtolea salamu mkubwa, basi yeye amtolee salamu huyo mdogo ili ahodhi ujira na fadhila ambazo agezipata lau angeanza yeye kutoa salamu. Amesema swahaba wa Mtume Ammaar Ibn Yaasir–Allah awawiye radhi: “Mambo matatu mtu akiyakusanya hukamilika imani yake:-

Uadilifu kwa nafsi yako, na

Na kuutolea salamu ulimwengu, na

Kutoa wakati wa dhiki”. Bukhaariy

 

Muradi wa kuutolea salamu ulimwengu ni kumsalimia na kumuamkia kila unayekutana nae. Ikiwa kuanza kutoa salamu ni suna, basi bila ya shaka kuijibu salamu ni fardhi toshelezi (kifayah). Yaani mmoja wa wanakundi waliosalimiwa akiitikia atakuwa amewatoshea wenzake kutokana na kuitikia kwake huko. Uwajibu huu wa kuitikia salamu ni amri ya Allah katika kitabu chake kitukufu: “NA MANPOAMKIWA KWA MAAMKIO YO YOTE YALE, BASI ITIKIENI KWA YALIYO BORA KULIKO HAYO, AU REJESHENI YAYO HAYO HAKIKA ALLAH ANAFANYA HISABU YA KILA KITU.” (4:86)

 

KUITIKA WITO:

Humtokea mwanadamu neema za Allah zikamfurahisha mithili ya kuoa au kuozesha, kuruzukiwa mtoto, kuponywa maradhi, kufaulu mtihani, kupata cheo na kadhalika. Ili kumshukuru Allah Mola mneemeshaji huamua kufanya karamu halali na kuwaalika ndugu na majirani zake kuja kushirikiana nae katika furaha yake hiyo. Ndio Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie–akatuambia: “Akikuita (akikualika) muitike,” kwani kuitika wito wa ndugu yako muislamu ni “Suna kokotezwa”. Usuna huu unatokana na yale yanayopatikana katika kuitika wito, ikiwa ni pamoja na kuimarisha udugu wa Kiislamu na kujenga mapenzi na mshikamano. Ni kweli kuwa mtu anapokualika katika jambo lake, huwa amekuthamini upeo, sasa kama hukumuitika huwa umemvunja moyo na kumfanya ajiulize kwa nini. Na pengine akahisi kudharauliwa na hivyo kumfanya ajenge chuki badala ya mapenzi. Kwa hivyo basi ni suna kuitika wito wa nduguyo muislamu kama hauna udhuru mkuu. Na hata kama umeudhurika basi ni vema ukamfahamisha kabla pamoja na kumuomba akuwiye radhi. Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie anatuambia: “Akialikwa mmoja wenu chakula, basi na aitike (mualiko huo), akiwa hakufunga na ale na akiwa amefunga basi na awaombee Mungu (waliomualika)”. Ahmad, Muslim, Abuu Daawoud, Tirmidhiy & Ibn Maajah.

TANBIHI: Si suna kuhudhuria karamu ambayo:-

Wamealikwa matajiri au watu mashuhuri pekee na kubaguliwa masikini na wanyonge Mtume wa Allah– Rehema na Amani zimshukie anatuasa: “Shari ya chakula (ni) chakula cha karamu, wanaalikwa matajiri na kuachwa mafakiri…” Bukhaariy, Muslim, Abuu Daawoud, & Nasaai.

Inawachanganya pamoja wanamume na wanawake na wanamume ambao si maharimu.

Ndani yake kuna jambo la haramu kama ulevi na kucheza muziki au karamu kufanywa mahala pa shari kama baa.

 

NASAHA:

Mwanadamu kimaumbile ni kiumbe anayekumbana na magumu yake. Kadhalika kimaumbile mwanadamu ni kiumbe tegemezi anayeishi katika kundi na asiyeweza kujitegemea mwenyewe katika uamuzi khususan wa magumu ya maisha. Sasa mwanadamu anaposibiwa na jambo gumu likamuhemeza asijue la kufanya na kuhitajia ushauri nasaha kutoka kwako. Hapo ndipo Mtume wako– Rehema na Amani zimshukie–anakwambia: “Akikutaka nasaha/ushauri, mnasihi.” Yaani atapokujia nduguyo muislamu kukutaka ushauri katika lililomsibu au analotaka kulifanya, basi ni wajibu wako kumpa ushauri/nasaha njema. Na utambue kwamba hilo alilojia ni haki yake aliopewa na Uislamu, na wewe kumpa nasaha na ushauri unaolenga kujenga au kutatua ni sehmu ya dini kwani Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie– ametuambia: “Dini ni nasaha kwa ajili ya Allah, kitabu chake, Mtume wake, viongozi wa waislamu na watu wote.”

Muslim, Ahmad, Nasaai & Abuu Daawoud.

Hata kama hakukujia kukutaka ushauri na ukaona kuwa atafikwa na madhara au janga fulani kutokana na mwenendo fulani alionao. Basi ni wajibu wako umkusudie na umnasihi kwa mapenzi ya udugu wa Kiislamu, lakini ni vema ukatambua kuwa wajibu wako ni kutoa nasaha tu na sio kumlazimisha kufuata nasaha. Kadhalika ni kheri ikiwa utatambua kwamba nasaha/ushauri ni amana, kwani anayekuja kukutaka ushauri huwa ameakuamini na kukuthamini. Kwa hivyo basi ni wajibu wako nawe kujithaminisha kwake na kuonyesha kuwa unastahiki heshima aliyokupa kwa kumpa ushauri mzuri. Kama hukufanya hivyo, yaani kwa makusudi mazima ukaamua kumpa ushauri nasaha utakaomtosa, utakuwa umemkhini (umemfanyia khiyana). Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie anatuambia: “…Atayempa nduguye ushauri kwa jambo ambalo anajua uongofu uko katika jingine, kwa yakini amemkhini” Abuu Daawoud & Al-Haakim

Na Allah Mola Mwenyezi anatuambia: “…HAKIKA ALLAH HAWAPENDI WAFANYAO KHIYANA.”

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |