Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

10. HAKI ZA MAKHADIMU (WATUMISHI WA MAJUMBANI), VIBARUA NA WAAJIRIWA

 Faida

Huduma/utumishi ni suala lisilopuuzwa wala kudharauliwa katika mfumo sahihi wa maisha (Uislamu). Umuhimu wa suala hili unatokana na ukweli kwamba maisha ya watu katika jamii yo yote ile ni maisha ya kutegemeana na kushirikiana. Ni ukweli usiohitaji ubishi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kujitegemea mwenyewe kwa kila hali. Kwa mantiki hii maisha ya mwanadamu ni maisha ya nihudumie nikuhudumie ili tusonge mbele kimaisha. Huduma na utumishi unaotolewa katika jamii unatofautiana baina ya mtu na mtu. Tofauti hii inatokana na uwezo, ujuzi na vipawa vya watu kwani kama alivyosema Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Kila mmoja amewepesishiwa aliloumbiwa kwa ajili yake”. Ahmad, Bukhaariy, Muslim & Abuu Daawoud.

Katika anga la udugu wa kiislamu, ndugu hawa wa imani wote husaidiana katika misingi ya wema na taqwa (ucha-Mungu). Hii ni katika jumla ya kuitekeleza amri ya Mola wao: “...NA SAIDIANENI KATIKA WEMA NA TAQWA...” [5:2] Na kigezo na kipimo cha ubora wa mtu katika Uislamu hakitokani na elimu, cheo, mali au kazi aifanyao. Bali msingi wa ubora umo katika tamko tukufu la Allah: “ENYI WATU! KWA HAKIKA TUMEKUUMBENI (nyote) KWA (yule) MWANAMUME (mmoja; Adamu) NA (yule yule) MWANAMKE (mmoja; Hawwa). NA TUMEKUFANYENI MATAIFA NA MAKABILA (mbalimbali) ILI MJUANE (tu basi, siyo mkejeliane). HAKIKA AHISHIMIWAYE SANA MIONGONI MWENU (mbora) MBELE YA ALLAH NI YULE AMCHAYE ALLAH ZAIDI KATIKA NYINYI. KWA YAKINI ALLAH NI MJUZI, MWENYE KHABARI (za mambo yote)”. [49:113]

Taqwa (ucha-Mungu) kama ijielezavyo aya ndio kigezo pekee cha ubora wa mtu katika Uislamu. Kwa yakini Uislamu umelihimiza sana suala la mtu kufanya kazi na kula kutokana na jasho lake. Uislamu unawataka waumini wake kujifunza kazi/ufundi mbalimbali utakaowawezesha kujitafutia riziki zao kwa njia za halali. Kwani kufanya kazi ndio njia pekee ya kuistawisha na kuijenga dunia yetu hii. Uislamu umetangaza kwamba chakula chema na kizuri anachokila mtu kwa raha na furaha ni kile anachokipata baada ya taabu na uchovu mkubwa unaotokana na harakati za kukitafuta. Mwanadamu huonja katika chakula hicho shida/taabu ya kazi yake na starehe ya matunda yake. Kuhusiana na hili Mtukufu Mtume wetu-Rehema na Amani zimshukie-anatuambia: “Kamwe hajapatapo ye yote kula chakula kilicho bora kuliko kula kutokana na kazi ya mikono yake. Na kwa yakini nabii wa Allah; Daawoud alikuwa akila kutokana na kazi ya mikono yake”. Bukhaariy

Mja anapojitahidi kufanya kazi kwa ajili ya kutafuta maisha na riziki/chakula chake binafsi na cha familia yake. Na kwa ajili ya kujizuia na vilivyomo mikononi mwa watu, mtu huyu afahamu kwamba ana ujira adhimu mbele ya Allah kutokana na amali yake hiyo. Imepokelewa kwamba: “Mtu mmoja alimpitia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-maswahaba wa Mtume wakaiona juhudi na bidii yake ya utendaji kazi. Wakasema: Ewe Mtume wa Allah, (waonaje) lau (juhudi na bidii) hii ingelikuwa (ingelitumika) katika njia (ya kuipigania dini) ya Allah? Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema:-

Ikiwa ametoka akifanya juhudi kwa ajili (ya riziki ya) wanawe wadogo (ambao hawajaweza kujitegemea), basi yeye yuko katika njia ya Allah.

Na ikiwa ametoka akifanya juhudi kwa ajili (ya chakula cha) wazazi wake wawili walio watu wazima wakongwe, basi huyo yuko katika njia ya Allah.

Na akiwa ametoka akifanya juhudi kwa ajili (ya riziki ya) nafsi yake ili aizuie na kuomba, basi huyo yuko katika njia ya Allah.

Na ikiwa ametoka akifanya juhudi kwa ajili ya kujionyesha na kujifakharisha (mbele za watu kuwa yeye ni mfanyakazi bora), basi huyo yuko katika njia ya shetani”. Twabaraaniy

Kadhalika imepokewa kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwamba yeye amesema: “Hakika Allah anampenda muumini mwenye ustadi/ujuzi wa kazi”. Al-Baihaqiy

Pamoja na Uislamu kuwahimiza waumini wake kufanya kazi, kadhalika haukulisahau suala la haki za msingi za watumishi, vibarua sambamba na waajiriwa. Uislamu umeweka katika misingi ya sheria yake haki zinazolinda maslahi, hadhi na heshima ya watumishi, vibarua na waajiriwa. Katika jumla ya haki ambazo Uislamu umeziweka ni kama zifuatavyo:-

HAKI YA UDUGU WA KIISLAMU NA KUSHIRIKIANA KATIKA CHAKULA NA MAVAZI:

Uislamu unasema muislamu ni ndugu ya muislamu na mafungamano ya udugu huu wa kiislamu ni mafungamano ya imani/itikadi. Imani ambayo inawajumuisha na kuwakusanya pamoja watumishi na watumikiwa, waajiri na waajiriwa na wafanyakazi na wafanyiwa kazi (mabwana). Uhusiano na mafungamano ya wawili hawa ni huu udugu wa kiimani. Kwa mantiki hii, ni wajibu chakula na mavazi ya ndugu hawa yawe mamoja kwa njia ya kusaidiana na si kwa njia ya usawa wa moja kwa moja (wa kila kitu). Wale chakula cha aina moja hata kama hawakukaa pamoja wakati wa kula, haya ndiyo mafundisho sahihi ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Watumishi wenu ni ndugu zenu (katika imani), Allah amewaweka chini ya mamlaka yenu. Basi ye yote ambaye nduguye (huyo) atakuwa chini ya mamlaka yake na amlishe anachokula yeye na amvishe anachokivaa yeye”. Bukhaariy & Muslim.

HAKI YA UJIRA (MSHAHARA):

Ujira/malipo ya kazi au utumishi, hii ni haki iliyowajibishwa na Uislamu. Hili linatokana na ukweli kwamba kila amali (kazi) ina ujira wake bila ya kuzingatia uzuri au ubaya wa amali hiyo. Kigezo na kipimo cha ujira wa amali katika Uislamu ni msingi usemao: (Jazaa/malipo ni kwa kadri ya amali iliyotendwa). Yaani ujira uzingatie ukubwa, uzito, hatari, mazingira na muda uliotumika katika kuitenda kazi husika. Mtumishi/muajiriwa/kibarua atapoitekeleza kazi yake kama walivyokubaliana na kuelekezwa na muajiri wake. Tayari amestahiki kulipwa ujira wa kazi hiyo kwa ukamilifu, uadilifu na kwa mujibu wa makubaliano na maagano yao kabla ya kuanza kwa kazi. Kuhusiana na haki hii ya ujira Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anatuambia: “Mpeni muajiriwa ujira wake kabla jasho halijakauka”. Ibn Maajah

Yaani apewe ujira wake bila ya kucheleweshewa au kusumbuliwa kwa kuambiwa njoo kesho, kesho akija anaambiwa tena njoo kesho, basi ilimradi kesho hiyo haitofika kamwe. Huu si Uislamu na muislamu wa kweli anayemtii Allah, Mtume wake na siku ya mwisho hathubutu katu kuyafanya hayo. Vipi atathubutu kuyafanya na ilhali anaikiri, anaiamini na kuikubali kauli ya Mtume wake-Rehema na Amani zimshukie: “Mbea tatu za watu, mimi ni khasimu wao siku ya kiyama”....akataja miongoni mwao....

“Mtu aliyemuajiri muajiriwa akamtekelezea kazi yake (kwa ukamilifu), naye asimpe ujira wake”. Ahmad & Ibn Maajah

Na hoja si tu kulipa ujira, bali je huo ndio ujira mliokubaliana au baada ya kufanyiwa kazi unaamua kumlipa kinyume na makubaliano yenu. Na je, ujira huo unalingana na kazi aliyoifanya? Kama wewe ndio ungekuwa katika nafasi yake-yaani muajiriwa na yeye ndio muajiri wako, ungeridhika na ujira huo unaompa yeye?! Ni vema ndugu muislamu ukajiuliza kwanza maswali haya kabla hujaamua kutoa ujira unaotaka kuutoa.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa “Amana/uaminifu huvuta (huleta) riziki na khiana huvuta ufakiri”. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie.


Forum | Guestbook | Tuandikie |