|
02.
Hekima/Falsafa ya kuoa
zaidi ya mke mmoja:
Hakika Uislamu umeruhusu kuoa zaidi ya mke mmoja
kiasili na wala haukulifanya jambo hilo kuwa ni FARADHI iliyo lazimu. Na kwa
yakini Uislamu, umeruhusu huku kuoa zaidi ya mke mmoja, kwa kuwa unalenga
malengo ya mbali katika utengenefu wa jamii. Hayadiriki kuyatambua malengo hayo
ila yule mwenye uoni mpevu, hizi hapa ni baadhi tu ya hikma/falsafa:
1.
Kwa kuruhusu kuoa zaidi ya mke mmoja,
Uislamu umelenga kumuhami/kumsitiri yule asiye toshelezwa na mke mmoja. Na hilo
ni jambo la kimaumbile, linaweza kumsukuma kutenda yale yasiyo pendelewa na
sharia.
Basi lililo bora kwao hawa wasio tosheka na mke mmoja na kwa
jamii, ni wao hawa kuoa mke mwingine kuliko kujitumbukiza katika uchafu wa
zinaa.
2.
Hali kadhalika Uislamu unalenga
kumuhifadhi mwanamke kuzengewa na wanaume wenye kuburuzwa na matamanio yao, si
kwa ndoa itakayo walinda watoto wake. Bali kwa njia ya uchafu na uhawara ambayo
humfanya mwanamke huyo kuwa dango la kutupwa na kunyimwa haki zote. Na kuwafanya
watoto wake alio wazaa katika njia hiyo, kuwa wanyimwa wa haki za nasabu, na
huruma ya ubaba.
Basi mwanamke huyu kuwa mke wa pili (mwenza) aliye na haki na
heshima ni bora kwake mara alfu kuliko kuwa mjane au hawara.
Kwa hivyo basi, lengo la Uislamu katika kuruhusu kuoa zaidi ya
mke mmoja ni kumuhifadhi mwanamke dhidi ya zinaa. Na wakati huo huo kumlinda
mwanamke dhidi ya kuwa muhanga wa matendo machafu ya wanaume waovu wasio na soni
wala haya. Na hali kadhalika kuilinda jamii dhidi ya fisadi na mmomonyoko wa
kimaadili na uenda hovyo.
i.
Sababu pelekeshi katika
kuoa zaidi ya mke mmoja:
Ziko sababu ambazo zinaifanya sharia ya kuoa zaidi ya
mke mmoja kuwa ni suala lenye hekima iliyo dhaahiri na faida iliyo wazi. Na ili
uelewe vema hili tunakupigia baadhi ya mifano:
1.
Mwanaume mwenye umeo na wanawake ana mke
mwenye ukinaifu na wanaume, ama ni kwa sababu ya maumbile au maradhi.
Basi je, lililo bora ni huyu mwanaume kuzini, ikapotea dini,
mali na siha yake? Au abakie na haja yake huku akiiadhibu nafsi yake? Au aoe mke
mwingine kwa sharti ya kumudu familia na kufanya uadilifu na kutofanya dhulma
katika tangamano?
Hapana shaka kwamba hili la tatu ndilo bora zaidi kwa huyu
mwanaume na ndilo lenye manufaa mno kwa jamii.
2.
Mfumuko wa vita duniani ambavyo leo
vimekuwa ni sehemu isiyo epukika ya maisha ya wanaadamu. Vita hivi vimeyagharimu
na vinaendelea kuyagharimu maisha ya wanaume maelfu kwa maelfu. Matokeo yake ni
kuzidi idadi ya wanawake kuliko ile ya wanaume kwa kiwango kikubwa.
Basi je, lililo bora kwa wanawake ni mwanaume kuoa mke mmoja tu
na wanawake wengine wasalie wakiwa wamenyimwa huruma ya mume mlezi wa familia?!
Na wakiwa wamekosa fursa ya kuzaa mtoto atakaye wasaidia katika utu uzima wao?!
Haya ni miongoni mwa ambayo yanaweza kumsukuma kutenda dhambi na kutumbukia
kwenye machafu ili kuishibisha haja yake. Au lililo bora ni kumruhusu mwanaume
kujikusanyia zaidi ya mke mmoja chini ya kivuli cha uangalizi kamili wa
kisheria?!
Hakika sisi hatutakuwa tumeidhulumu mantiki na haki, kwa
chochote, tutakapo sema: Hakika kuoa zaidi ya mke mmoja katika hali/mazingira
haya, kunazingatiwa kuwa ni kitendo cha ubinaadamu/utu kinacho faradhishwa na
murua na ghera. Na wala hatutakuwa tunapingana na hali ilivyo, tutakapo sema:
Hakika uoaji wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wa zaidi ya mke mmoja,
sehemu yake kubwa ilikuwa ni kwa namna hii tukufu ya utu. Baadhi ya wakeze kuna
ambaye alihajiri peke yake na kuwaacha jamaa zake, na yupo aliye fiwa na mume
wake hali ya kuwa ni shahidi na kumuacha mjane asiye na mwangalizi. Mtume wa
Allah akampunguzia uzito wake na akamkusanya nyumbani kwake na akawa kwake yeye
ni msimamizi/muangalizi bora. Naye akapata sharafu ya umama wa waumini na
fadhila ya kuungana na Bwana wa mitume.
3.
Mtu amemuoa mwanamke wanaye pendana,
lakini mwanamke huyu ni tasa hazai, naye anatamani kupata mtoto. Basi je, lililo
bora ni sisi kumzuia mtu huyu kuoa mke wa pili na kumuacha akiwa mpweke wa moyo
asiye na mwana?! Au tumuamuru amtaliki mke wake anaye mpenda au tumruhusu kuoa
mke mwingine pamoja na kumuhami yule wa kwanza kudhulumiwa?! Hakika hili la
mwisho ndilo suluhisho bora kuliko yote yaliyo tangulia, kwani ndilo lililo
chunga maslahi ya mwanaume na mwanamke kwa kiwango sawa.
4.
Hakika mataifa na jamii ambazo
zimeharimisha kuoa wake wengi, zimetumbukia ndani ya khatari kubwa na madhara
makubwa mno kuliko hayo madhara ya kuoa wake wengi kama wanavyo dai. Ni ukweli
usio kanushika kwamba fisadi imekithiri katika mataifa/jamii hizo na kumeenea
humo kuendeana kinyume baina ya wanandoa na nyumba ndogo za siri. Mambo haya
yamewafanya wenye akili/busara wao kupaaza sauti za kutaka kuweko na sheria
inayo ruhusu ndoa ya wake wengi na kondosha fisadi hizo zinazo damirisha
(angamiza) maisha yao ya kijamii.
Tanbihi:
Hakika
utumiaji mbaya wa ruhusa ya kuoa zaidi ya mke mmoja wa baadhi ya watu majahili,
hauifuti hekima/falsafa ya Uislamu na wala Uislamu haubebi zigo la ujahili wa
majahili hao. Kwani Uislamu haukuruhusu kuoa zaidi ya mke mmoja ili iwe ni
silaha ya kujeruhia, kuchinjia au tangamano ovu. Hakika si vinginevyo, Uislamu
umelifanya hilo kuwa sharia kwa ajili ya kukidhi haja, kuilinda jamii, kumchunga
mtu mmoja mmoja na kundosha maovu/uchafu.
Kwa sababu zote
hizo pelekeshi na sharti hizo za kisharia, ndio Uislamu ukaruhusu kuoa zaidi ya
mke mmoja na wala haukuliwajibisha hilo kwa njia ya lazima. Na Uislamu
ukaizungushia ruhusa hiyo dhamana tabia za kihaki. Kwa maelezo haya, Uislamu
umefanana mno na duka la dawa lililo sheheni dawa zote zinazo kidhi haja za watu
wote. Kila mmoja anajitwalia dawa inayo wafikiana na haja na maradhi yake. Na si
jambo linalo ingia akilini kuruhusu dawa zote zilizomo humo kwa kila mtu hata
pasina haja.
|