|
Tatu: Posa.
Kukitimia na kuaminika na sifa njema na ikathibiti radhi na raghba, kwa
kuona/kuangalia, hapo ndipo inapo kuja zamu ya posa. Na posa maana yake ni zile
harakati na kitendo cha mwanaume (mposaji) kutaka ndoa kwa upande wa mwanamke
(mposwaji).
Ni wakati
gani kunahalalika kupeleka posa na wakati gani kunaharimika:
1.
Kunahalalika kuposa kwa ufumbulizo
(waziwazi) na kwa fumbo (ishara) pindi atakapo kuwa mwanamke anaye poswa hayuko
katika ndoa, eda na vizuizi vyote vya ndoa ambavyo tayari vimetajwa katika
kipengele cha “WANAWAKE WALIO HARAMU KUWAOA”.
2.
Kunahalalika kuposa kwa fumbo tu na si
kwa ufumbulizo, pindi atakapo kuwa mwanamke mlengwa yumo katika eda ya kufiwa au
talaka baini (tatu). Allah Ataadhamiaye amesema: “WALA SI VIBAYA KWENU KATIKA
KUPELEKA POSA KWA ISHARA TU KWA WANAWAKE WALIOMO EDANI AU MKADHAMIRIA KATIKA
NYOYO ZENU. ALLAH ANAJUA KWAMBA NYINYI MTAWAKUMBUKA. LAKINI MSIWAAHIDI KWA SIRI,
ILA MNENE MANENO MEMA. WALA MSIAZIMIE KUFUNGA NDOA MPAKA EDA IFIKE MWISHO WAKE.
NA JUENI KWAMBA ALLAH ANAJUA YALIYOMO KATIKA NAFSI ZENU. BASI TAHADHARINI NAYE.
NA JUENI KWAMBA ALLAH NI MWENYE KUSAMEHE NA MPOLE”. [02:235]
3.
Ni haramu kupeleka posa kwa fumbo na
ufumbulizo katika hali/mazingira ambayo hayakutajwa katika nambari moja na
mbili.
Kwa kuyajengea
hayo basi, ni haramu kumposa mwanamke ambaye bado yuko katika hifadhi ya mume
wake. Kama kunavyo harimika kumposa kila mwanamke aliye chini ya kipengele cha
“WANAWAKE WALIO HARAMU KUWAOA”. Ni mamoja umekuwa uharamu huo ni wa milele au ni
muda tu.
Na ni haramu
kumposa mwanamke aliye katika eda ya talaka rejea (moja/mbili). Ni mamoja
imekuwa posa hiyo ni ufumbulizo au fumbo, kwa kuwa bado ni mke au yumo katika
maana ya mke. Hii ni kwa sababu mume wake anayo haki ya kumrejea, Allah
Atukukiaye amesema: “...NA WAUME WAO WANA HAKI YA KUWAREJESHA KATIKA MUDA HUO,
KAMA WAKITAKA KUFANYA SULUHU...” [02:228] – Yaani na waume zao wanayo haki
kuwarejea katika ule muda wa eda. Na waume wanapo tumia haki hiko wakusudie
kupatana na si kudhuru.
Maana ya
kufumbuliza posa:
Ufumbulizo katika posa, maana yake ni: Kila tamko linalo tinda katika kuonyesha
waziwazi nia ya kuoa. Kama vile mwanaume kumwambia mwanamke: “Ninataka kukuoa”,
au “Eda yako itakapo malizika nitakuoa”.
Maana ya
kufumba/kuashiria posa:
Kufumba posa maana yake ni: Ni mwanaume kutumia tamko ambalo linalo beba kwa
pamoja dhamira ya kuoa na kitu kingine. Kama vile kumwambia mueda (mwanamke
aliye edani): “Wewe ni mrembo” au “Huenda yuko akutakaye” au “Nani atampata
mwanamke kama wewe” na mfano wa kauli kama hizi.
Posa juu ya
posa:
Ni
haramu mtu kupeleka posa juu ya posa ya ndugu yake (mwenzake) ikiwa amekwisha
pewa jibu la ufumbulizi, ila kwa idhini. Hivi ndio kusema kuwa, ikiwa mtu
ameposa mahala na ikawa amekwisha jibiwa, basi ni haramu mtu mwingine nae kwenda
kuposa mahala pale pale ila kwa idhini ya mtangulizi katika posa.
Angalia, ikiwa
hakujibiwa, basi si haramu mtu mwingine kupeleka posa. Na uharamu huu ulio tajwa
ni ule uharamu unao pasisha kupata dhambi na wala haupasishi kubatilika kwa
kifungo cha ndoa. Hii ni katika sura ambayo atakapo posa juu ya posa ya
mwenzake, akakubaliwa na akaoa.
Dalili ya
uharimisho huu, ni kauli ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie:
“Asipose mtu juu ya posa ya ndugu yake (muislamu mwenzake), mpaka aache mposaji
wa kabla yake au huyo mposaji ampe idhini”. Bukhaariy [4848] & Muslim
[1412]-Allah awarehemu.
Hukumu ya
kutaka ushauri katika kumjua mposaji au mposwaji:
Mtu
atakaye takwa ushauri utakao pelekea kumjua mposaji au mposwaji, kumemuwajibikia
kutaja aibu na mabaya anayo yajua kwa ukweli ili wapate kuchukua tahadhari.
Kufanya hivyo ni kutoa nasaha na wala hilo halihesabiki kuwa ni katika jumla ya
usengenyi ulio harimishwa. Hivi ni iwapo kutajitokeza haja ya kutaja
aibu/kasoro. Ama pakiondoshwa bila ya kuyataja hayo, mathalan mtu kusema:
“Mwanaume huyu hakufai” au “Mwanamke huyu hakufai”, kumewajibika kutosheka na
kauli hiyo.
Dalili ya
hukumu hii, ni hadithi ya Bi. Faatimah Bint Qays-Allah amuwiye radhi-kwamba yeye
alimwambia Mtume-Rehema na Amani zimshukie: Hakika Muawiyah Ibn Abu Sufyaan
na Abu Jahm, wote wawili wameniposa. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akasema: “Ama Abu Jahm, huyu yeye habandukani na fimbo yake (mkali) na
Muawiyah ni hohehahe; hana mali. Olewa na Usamah Ibn Zaid”. Sikumpenda (Usamah).
Kisha (Mtume) akasema: “Olewa na Usamah”. Basi nikaolewa nae. Allah akanijaalia
kheri nyinyi kwake...” Muslim [1480] & Tirmidhiy [1135]-Allah awarehemu.
Walii
kutangaza kuwa anaye binti wa kuolewa kwa watu wema wenye uchaMngu:
Kumesuniwa kwa walii wa mwanamke ambaye anataka kumuoza, kumtangazia kuolewa kwa
watu wema, wacha-Mngu. Kufanya hivyo ni kuiga na kufuata kile alicho kifanya
Mtume Shuaib kwa Mtume Musa-Rehema na Amani ziwashukie. Pale alipo mtangaza
binti yake kwake kwa sababu ya uaminifu wake na kujizuia kwake na machafu.
Amesema Allah Atukukiaye katika kukihadithia iisa hicho: “AKASEMA: MIMI NATAKA
KUKUOZA MMOJAWAPO KATIKA BINTI ZANGU HAWA WAWILI KWA KUNITUMIKIA MIAKA MINANE.
UKITIMIZA KUMI KHIARI YAKO; LAKINI MIMI SITAKI KUKUTAABISHA. INSHALLAH,
UTANIKUTA MIUONGONI MWA WATU WEMA. MUSA AKASEMA: HAYO YAMEKWISHA KUWA BAINA
YANGU NA WEWE. MUDA MMOJAPO NIKIUMALIZA SITIWI UBAYANI. NA ALLAH NI MLINZI JUU
YA HAYA TUNAYO YASEMA”. [28:26-28]
Na pia kwa
ajili ya kuiga alicho kifanya Sayyidna Umar Ibn Al-Khataab-Allah amuwiye
radhi-pale alipo mtangaza binti yake Hafsah kwa Sayyidna Uthman, kisha kwa
Sayyidna Abu Bakri-Allah awawiye radhi wote. Mwisho wa mzunguko huo akaja
kuolewa na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie.
|