|
Wanawazuoni wa fani hii ya fiq-hi (Mafaqihi) wamekongamana na kuwafikiana kwamba
kila lenye kutengua na kubatilisha udhu pia hubatilisha upakazaji juu ya khofu. Kwa nini?
Hi ni kwa sababu upakazaji juu ya khofu ni sehemu ya udhu na ni badali ya kuosha miguu.
Kwa mantiki hiyo kinachotengua na kubadilisha asli (udhu) hubatilisha pia tanzu/tawi
(upakazaji juu ya khofu). Mbali na hili, huongezeka pia mambo mengine matatu, ambayo ni:-
- Kuisha/kumalizika muda wa upakazaji ulioruhusiwa kisheria kwa mkazi na msafiri.
Muda huo utakapomalizika, mpakazaji anatakiwa kwa mujibu wa sheria azivue khofu zake,
kisha atawadhe udhu kamili, hapo ndipo anaweza kuzivaa tena kwa twahara hii mpya na kupata
ruhusa ya kupakaza juu yake atakapotawadha tena, pia muda mpya utaanzia hapo.
- Kupatikana kwa jambo linalowajibisha josho kama vile janaba, hedhi au nifasi.
Katika hali hii imempasa na kumlazimu mpakazaji kuzivua khofu, akoge josho
lililomuwajibikia, kisha ndipo anaruhusiwa kuzivaa tena ikiwa anaona kuna haja ya kufanya
hivyo. Imepokelewa hadithi na Swafwaan Ibn Assaali Allah amuwiye radhi
amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu alikuwa akituamrisha tunapokuwa safarini tupakaze
juu ya khofu zetu na wala tusizivue kwa muda wa siku tatu kutokana na kukidhi haja
kubwa/ndogo na kulala ila kutokana na janaba (tu)". Tirmidhiy na Nasaai.
- Mtu kuzivua khofu zote mbili au mojawapo hata kama ikiwa uvuaji huo ni kwa kutoa
sehemu kubwa ya mguu bila ya kuutoa mguu wote. Au kwa kutoboka khofu kiasi cha kuuonyesha
mguu. Katika hali zote hizi imempasa mpakazaji kuzivua.
ix: KUPAKAZA MAJI JUU YA SOKSI
Naam, kunajuzu kupakaza maji juu ya soksi pale zitakapokuwa zimekamilisha soksi
hizo masharti yote ya upakazaji juu ya khofu, kama yalivyoelezwa katika darasa
zilizotangulia. Sheykh Abdurahman Al-Jasiyriy Allah amrehemu amesema katika kitabu
chake kiitwacho "AL-FIQ-HU ALAL-MADHAAHIBIL ARBAA." Juzuuu ya I, ukurasa
113, chapa ya DAARUL-HADITH Cairo ambayo mukhatasari wake ni kwamba wala hakuna
tofauti baina ya kuwa khofu imetengenezwa kwa ngozi, au sufi nzito au pamba, na huitwa
kilichotengenezwa kutokana na malighafi hizi (sufi/pamba) JAURABU (soksi) na jaurabu
(maana yake) ni kile kivaliwacho mguuni kama ilivyo maarufu katika zama zetu hizi. Basi,
hakika inaswihi kupakaza juu yake (jaurabu) wakati zitakapokuwa ni ngumu na imara.
Haiswihi kupakaza juu ya soksi nyepesi ambazo haziwezi kuzuia maji kupitia ndani.
.." Mwisho wa kunukuu. Kisha akaendelea kusema tena: Kupakaza juu
ya khofu kumethibiti kwa riwaya iliyopokelewa na Mughiyrah Ibn Shubah Allah
amuwiye radhi "kwamba mtume Rehema na Amani zimshukie alipakaza
juu ya soksi na makubadhi."
X: KUPAKAZA MAJI JUU YA VICHACHA (P.O.Ps) NA UTEPE (BANDAGE)
Ni vema kabla hatujaanza kuelezea hukumu na namna ya upakazaji juu ya vichacha na
utepe, tukabainisha kichacha na utepe ni nini? Tuanze na kichacha, hiki ni kiungio
kinachofungwa juu ya kiungo kilichovunjika ili kipate kuungana. Kiungio hiki kinaweza kuwa
ni aina Fulani ya mbao au chenye kufanana na mbao kama vile P.O.P maarufu
"muhogo" zinazotumika mahospitalini leo. Tukija katika utepe, tunaweza kusema
utepe ni aina Fulani/maalumu ya kitambaa kinachowekwa juu ya jeraha ili kulihifadhi
kutokana na vumbi,wadudu kama inzi na vitu vingine vyenye madhara mpaka jeraha lipone. Kwa
kuuzingatia ule ukweli kwamba uislamu ni dini ya maumbile, dini iliyojengwa katika misingi
ya wepesi, tusome sote kwa pamoja: "
ALLAH ANAKUTAKIENI YALIYO MEPESI WALA
HAKUTAKIENI YALIYO MAZITO..." (2:185) Ndipo tunaona uislamu ukiyazingatia maumbile na
hali zinazomsibu na kumtokea binadamu katika maisha yake ya kila siku, ikiwa ni pamoja na
matukio ya kuvunjika baadhi ya viungo au kupatwa na majeraha. Majanga yote haya
yanapompata binadamu, hana budi kuirekebisha hali hiyo kwa kujitibu na kufanya dawa, jambo
ambalo limeruhusiwa na sheria. Katika hali hii binadammu huyu anakabiliwa na mambo mawili
kwa pamoja ambayo yote yamempasa kuyatekeleza; moja lilnahuhusu mwenyewe pekee (kujitibu)
na jingine linamuhusu yeye na Mola wake (ibada). Ni kwa kulizingatia hili ndipo
sheria/uislamu ukamuwekea binadamu huyu mazingira mazuri ya utekelezaji wa ibada sambamba
na kujitibia kwa kumuwekea sheria hii ya upakazaji maji juu ya vichacha na utepe, sheria
na kanuni ambazo zitadhamini mambo yote mawili; utekelezaji wa ibada na kuhifadhi afya na
usalama wa mwili wa binadamu. Baada ya kuwazihisha (kuweka wazi )maana ya vichacha na
utepe, hebu sasa kwa msaada wa Allah, tuziangalie:-
HUKUMU ZA VICHACHA NA UTEPE
Mgonjwa aliyepatwa na jeraha au mvunjiko, huweza kuhitajia kufunga kichacha/utepe
na kuweka dawa juu ya jeraha hilo au mvunjiko na wakati mwingine asihitajie kabisa. Iwapo
atahitajia kuweka kichacha au kufunga utepe, basi imemlazimu katika hali hii mambo matatu
yafuatayo;
- Wakati wa kutawadha/kuoga ni lazima aoshe ile sehemu nzima ya kiungo kisichopatwa
na masaibu (jeraha/mvunjiko)
- Apakaze maji juu ya kichacha chenyewe au utepe wote.
- Atayamamu badala ya kuosha kiungo kigonjwa atakapokifikia wakati wa kutawadha.
Kutokana na mambo matatu hayo tuliyoyataja hapo juu tutafahamikiwa kwamba mtu
atakapoweka kichacha au kufunga utepe itamlazimu:
(i) Kuosha (ii) Kupakaza na (iii) kutayamamu.
Sasa, ni wapi ataosha, atapakaza na kutayamamu yarejee vema maelezo hayo hapo juu.
Ikiwa mtu hahitaji kufunga kichacha juu ya kiungo kilichovunjika au utepe juu ya jeraha,
itamuwajibikia kuosha kiungo kilicho kizima na kutayamamu kwa sababu ya jeraha iwapo
hawezi kuosha mahala palipo pagonjwa. Kadhalika itamuwajibikia kurudia kutayamamu kila
anapotaka kuswali swala ya faradhi hata kama hakuhuduthi na wala si wajibu kuosha viungo
vyake vingine vilivyosalia ila atakapohuduthi.
DALILI NA USHAHIDI WA KUWEKWA SHERIA HII YA UPAKAZAJI JUU YA VICHACHA.
Ushahidi wa kuwekwa sheria hii ni riwaya iliyopokelewa na Jaabir-Allah amuwiye
radhi amesema: Tulikwenda safarini, mwenzetu mmoja akapatwa na jiwe likampasua
kichwani, kasha (usiku alipolala) akajiotelea, akawauliza wenzake: Je, mnanipatia rukhsa
ya kutayamamu? Wakamjibu; Hatukupatii rukhsa na il-hali unaweza (kutumia) maji. Basi
akakoga, akafa ( kutokana na maji kuingia katika jeraha). Tuliporudi kwa Mtume
Rehema na Amani zimshukie alieleza khabari hizo, akasema: "Wamemuua, Mwenyezi
Mungu awauwe na wao, kwanini wasiulize waliokuwa hawajui? Bila shaka dawa ya ujinga ni
kuuliza, hakika si vinginevyo ilikuwa inamtoshea kutayamamu na kufunga juu ya jeraha lake
kitambaa (utepe) kisha akapakaza maji juu yake na kuosha viungo vingine." Abuu
Daawoud. Kadhalika ushahidi mwingine ni ile riwaya ya Imamu Aliy Ibn Abiy Twaalib
Allah amridhie amesema: Kilivunjika kiwiko cha mkono wangu (nikafunga kichacha)
nikamuuliza mtume Rehema na Amani zimshukie akaniamrisha nipakaze maji juu
ya vichacha.."
MUDA WA UPAKAJI JUU YA KICHACHA NA UTEPE
Upakaji maji juu ya kichacha na utepe haukuwekewa muda maalumu na sheria. Mtu
ataendelea upakaza mpaka pale udhuru utakapoondoka, kiungo kilichovunjika kiunge au jeraha
lipone hapo ndipo ruhusa ya upakaji itakuwa imemalizika na kumuwajibikia sasa kuosha.
Hukumu ya vichacha ni moja tu, ni mamoja ikiwa twahara hiyo (pamoja na vichacha) ni kwa
sababu ya hadathi ndogo au kubwa. Isipokuwa katika hadathi kubwa, upakaji utakapobatilika
itamuwajibikia kuosha mahala palipokuwa na kichacha au tepe tu na wala si wajibu kuosha
sehemu nyingine ya mwili zaidi ya hiyo.
MAS-ALA: Itamuwajibikia mfungaji wa kichacha kukidhi swala katika maeneo au
mazingira yafuatayo:
- Atakapokiweka bila ya kuwa na twahara na ikashindikana kukivua.
- Au kichacha kilikuwa katika viungo vya tayamamu ambavyo ni uso na mikono.
- Au kichacha kitakapochukua sehemu kubwa ya mahala palipo pazima.
|