Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

II) FALSAFA YA SWALA

Faida

Ndugu zanguni Waislamu, jamii yoyote ya wanadamu inahitaji sera na utaratibu maalumu wa malezi ili kupata kizazi na jamii njema itakayoufanya ulimwengu huu kuwa ni kisiwa cha amani. Sera utaratibu huu na malezi ni lazima ujengwe juu ya nguzo tatu zifuatazo:-

1.    Nguvu

2.    Upendo, na

3.    Unyenyekevu.

 Tunakusudia nini tunaposema nguvu? Nguvu zikusudiwazo hapa ni nguvu za mwili, roho na akili, ama mradi wa upendo ni kuiangalia jamii ya kiislamu, kwa jicho la rehema na upole na kuitazama jamii ya wanadamu kwa ujumla mtazamo wa kusaidiana na kufahamiana. Kwa neno unyenyekevu hatukusudii kingine zaidi ya kuondosha tofauti na matabaka katika jamii ya kiislamu (Umma). Tajiri asijikweze juu ya fakiri kwa sababu tu ya utajiri wake, wala watu waliobeba dhamana mbalimbali serikalini wasijione kuwa ni bora kuliko wananchi wa kawaida eti kwa sababu tu ya nyadhifa zao. Kadhalika watu wasijifakharishe na kujivuna kwa nasabu, mavazi, na mali zao, bali kigezo chao cha ubora, heshima na  utukufu kiwe ni ucha-Mungu (Taq-wa) tu basi. Tusome na tuwaidhike’…..HAKIKA AHISHIMIWAYE SANA MIONGONI MWENU MBELE YA ALLAH NI YULE AMCHAYE ALLAH ZAIDI KATIKA NYINYI…….” (49:13) Bahati kubwa na sudi njema waliyonayo Waislamu ni kuwa na sheria bora na kamilifu kuliko sheria zote zilizobaki kuwepo, zilizopo na zijazo. Sheria ambayo imehodhi sera/utaratibu huu wa malezi, sera ambayo imewafanya watu wote kuwa ni sawa. Kigezo na dalili kubwa juu ya hili ni ibada kama vile swala, swaumu n.k. kitu ambacho Uislamu umekifanya kuwa ndio msingi na nguzo yake madhubuti. Hebu sasa na tupekue na kubahithi kwa pamoja ili tuone ni vipi tunavyoweza kuipata misingi ile mitatu  ya malezi katika ibada ya swala. Tuanze na ule msingi wa kwanza.

 1.          NGUVU

Hivi huoni kuwa udhu ambao ndio msingi wa ibada nzima ya swala kuwa ni NGUVU ya mwili, NISHATI ya roho na ni NADHAFA ya kiwili wili kwa ujumla ? Je, huoni kuwa kuifungua swala kwa tamko lenye kudumu milele “ALLAHU AKBAR” ni nguvu ya roho inayomfanya mtu ahisi kuwa Allah ni Mkubwa kuliko wakubwa wote? Allah ni  Mtukufu  kuliko watukufu wote? Hakuna Mkubwa wala Mtukufu mbele yake ila ni yeye tu. Ni hisia hizi ndizo zilizowafanya wachawi kutotetereka na kurudi nyuma mbele ya mabavu, nguvu na vitisho vya Mungu mtu- Firauni  Tujikumbushe hali ilivyokuwa: (Firauni) AKASEMA: OH! MNAMUAMINI KABLA SIJAKUPENI RUHUSA! BILA SHAKA YEYE NDIYE MKUBWA WENU ALIYEKUFUNZENI UCHAWI. KWA HIVYO NITAKUKATENI MIKONO YENU NA MIGUU YENU KWA KUTAFAUTISHA (mkono wa kulia na mguuu wa kushoto na mkono wa kushoto na mguu wa kulia ) NA NITAKUSULUBINI KATIKA MASHINA YA MITENDE, NA BILA SHAKA MTAJUA (wakati huo) NI NANI KATIKA SISI (mimi au Mungu wake Musa) ALIYE MKALI WA KUADHIBU NA KUJIENDESHA (kuindeleza adhabu yake) “ WAKASEMA : “HATUTAKUKHITARI WEWE KULIKO ZILE ISHARA WAZIWAZI (za haki) ZILIZOTUJIA. TUNAAPA KWA YULE ALIYETUUMBA. BASI FANYA UNAVYOTAKA KUFANYA, WEWE UNAWEZA KUTOA HUKUMU INAYOHUSIANA NA MAISHA HAYA YA DUNIA TU” (20: 71-72).

 Ni hisia hizi hizi zitokazo na nguvu ya kiroho izalishwayo na kukuzwa siku hata siku ndani ya swala iliyomfanya Mtume Mussa – Amani ya Allah imshukie – kutobabaika wala kuyumba wakati wafuasi wake (bani Israil ) walipokata tamaa kabisa na kuona kuwa mwisho wao umefika. Hawana kitakachowaokoa na jeshi kubwa la Firauni linalowafukuza na mbele yao kuna habari nyekundu (Red sea). Tuitegee sikio Qur-ani ikituelezea hali ilivyokuwa . “NA YALIPOONANA MAJESHI MAWILI (haya , watu na Nabii Musa wanakimbia, na Firauni na watu wake wanawafuatia) WATU WA MUSA WALISEMA “ HAKIKA TUTAKAMATWA” (Musa) AKASEMA: “ LA, KWA YAKINI MOLA WANGU YU PAMOJA NAMI, BILA SHAKA ATANIONGOZA (tuokoke sote)”…………….NA TUKAMUOKOA MUSA NA WALE WALIOKUWA PAMOJA NAYE WOTE” ( 26:61-62, 65). Ni hisia hizi pia ndizo zilizomtia nguvu na kumuondolea wasiwasi Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alipokuwa pangoni na swahibu yake Abu Bakri – Allah amuwiye radhi. Makurayshi wamesimama mdomoni mwa  pango, miguu yao inaonekena na waliomo ndani kama yanavyosikiwa maneno yao. Hapo Abuu Bakri akitetemeka kwa khofu kuu anamnong’oneza Mtume –“ Ewe Mtume wa Allah, lau mmoja wao atatazama chini ya miguu yake bila shaka atatuona (Mtume) akamwambia, “ Nini dhana yako we Abu Bakri kwa wawili ambao Allah ni watatu wao?! “ Bukhariy na Muslim.

 Hebu tuipe nafasi Qur-ani Tukufu: “KAMA HAMTAMNUSURU (Mtume ) BASI ALLAH ALIMNUSURU WALIPOMTOA WALE WALIOKUFURU, ALIPOKUWA (mmoja tu  na mwenziwe) WA PILI WAKE (peke yao) WALIPOKUWA WOTE WAWILI KATIKA PANGO, (Mtume) ALIPOMWAMBIA SAHIBU YAKE, “ USIHUZUNIKE KWA YAKINI ALLAH YU PAMOJA NASI” ………….”  (9:40).

 Ni hisia hizi ndizo zilizompa Bwana Mtume ushujaa na kutokubabaika mbele ya upanga wa Daathuuri katika vita vya Ghatwafaani. Waislamu walipiga kambi, Mtume akawa amejitenga jpembeni amepumzika chini ya mti akiwa ameanika nguo zake zilizoloa kutokana na mvua iliyowapata. Hapo ndipo Daathuuri mmoja wa maadui akaona amepata fursa nzuri ya kummaliza Mtume. Akamuendea Mtume mpaka akamsimamia kichwani, upanga mkononi, Akamuamsha, Mtume na kumwambia: ni nani atakayekuzuia nisikuue, ewe Muhammad? Mtume akamjibu: Allah! Pale pale mtu yule akapatwa na kitisho na woga uliomtambaa mwili mzima na kutetemesha kiasi cha kuacha upanga umuangukie Mtume akauokota na kumuuliza  hasimu yake swali lile lile: Ni nani atakayenizuia nsikuue, ewe Daathuiru? Akajibu: Hapana ye yote. Mtume akamsamehe. Rejea vitabu vya sira kwa ukamilifu wa kisa hiki, ukitaka safu zilizonyooka na kukamatana nyuma ya Imam mmoja, zikisikiliza kisomo chake (Qur-ani aisomayo), zikiunyenyekea waadhi upatikanao ndani ya kisomo hicho, zikimfuata Imam wao katika harakati na vitulizano vyake. Huoni kuwa nidhamu hii inaonyesha nguvu ya jamii iliyoungana pamoja na yenye lengo moja? Kuna nguvu ipi ulimwenguni iliyo bora ziadi inayoweza kuilea jamii kuliko nguvu hii inayopandikizwa na swala katika nafsi ya muislamu?

 2.          UPENDO:

Hebu sasa tuingalie swala ni kwa kiasi gani inaweza kuwa ni kiwanda kinachozalisha bidhaa adimu na muhimu “Upendo”. Hebu itazameni swala wakati waislamu wanapokusanyika mahala pamoja mbele ya Bwana Mlezi wa viumbe wote, sio Bwana wa uma mmoja, Taifa moja wala dini/mfumo mmoja wa maisha bali ni Bwana Mlezi wa viumbe wote Mwingi wa Rehema Mwenye kurehemu. Ambaye huwabubujishia na kuwamiminia rehema yake woote, waislamu na wasio waislamu (makafiri) watiifu na waasi, wema na waovu, wadogo na wakubwa kisha angalia namna muislamu anavyoikhitimisha swala yake kwa kusema, Amani iwe juu yetu na juu ya waja wema wa Allah! Hapa anawakumbuka ndugu zake waliotapakaa mashariki na magharibi ya ardhi. Kisha anatoka ndani ya swala kwa REHEMA na AMANI, husema Amani na Rehema ya Allah iwe juu yenu.

 Aliianza swala yake kwa tuamko la “ALLAAHU AKBAR!”
Allah ni Mkubwa kuliko wakubwa wote, na sasa anaikhitimisha kwa tamko la Amani na Rehema. Haya yote ni vigezo na vielelezo tosha kwamba nguvu ya Uislamu ni nguvu inayokomelea na Rehama na Amani vitu ambavyo ndio chemchem ya upendo. Hivi ndivyo swala inavyoweza kupandikiza nguvu ya upendo na moyo wa kuzoeana na kupendana baina ya waislamu khasa khasa katika swala za jamaa,

 

3.        UNYENYEKEVU

Unyenyekevu unapatikanaje ndani ya swala? Huoni kuwa ni upeo wa unyenyekevu usio ni mithali pale muislamu anapokiweka mavumbini kiungo chake kitukufu “Uso” kumsujudia Mola wake. Tena wakalingana sawa katika unyenyekevu huu watu wote, wakubwa kwa wadogo, wanaume na wanawake, mabwana na watwana. Hapana kichwa cho chote kinachoweza kuwa juu ya kichwa kingine katika rukuu na sujudi. Ndani ya swala katika majumba ya Allah (Misikiti) mwanadamu hupata heshima na utukufu kuangalia matabaka na nyadhifa zao. Swala kuwakumbusha viongozi/watawala usawa wao na wananchi wa kawaida pale wanaposimama safu moja, bega kwa bega, mguu kwa mguu, wakiwa nyuma ya Imamu mmoja.

 Mbali na nguzo tatu hizo, nguvu, upendo na unyenyekevu, swala ina hekima na manufaa mengi yasiyomalizwa kuzungumzwa na maneno ya kinywa cha binadamu mpungufu. Katika jumla ya falsafa ya swala ni kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu juu ya neema zake zisizodhibitika alizotuneemesha : “…………NA KAMA MKIHISABU NEEMA ZA ALLAH, HAMTAWEZA KUZIHISABU BILA SHAKA MWANADHAMU NI DHALIMU MKUBWA ASIYE SHUKRANI (mwizi wa fadhila) “ (14:34). Pia swala hujenga mahusiano na mawasiliano mazuri baina ya kiumbe (mja) na Muumba wake kwani mja huwa karibu zaidi na Mola wake anapokuwa ndani ya swala, ambamo humo hupata raha na utulivu wa moyo.

 Kadhalika swala humfinyanga muislamu kuwa ni mtu mwenye nidhamu. Hii ni kwa sababu ndani ya swala muislamu hulazimika kumfuata Imamu wake kwa utaratibu maalumu ili swala yake ikubaliwe kitendo cha kurudiarudia utaratibu huu ndio humjengea muislamu tabia ya kuwa na nidhamu.

 Katika jumla ya mambo yanayoonyesha kwamba swala ina athari kubwa na nzuri katika kuwalea wanadamu na kudumisha tabia na maadili mema ni kitendo cha Nabii Ibrahim-Allah amshushie Amani- kumuomba Mola wake amjaalie yeye na kizazi chake kuwa ni wasimamishaji wa swala, aliposema: MOLA WANGU! NIJAALIE NIWE MSIMAMISHAJI SWALA, NA KIZAZI CHANGU (pia  kiwe hivi) MOLA WETU ! NA UPOKEE MAOMBI YANGU”  (14:40).

 Swala ndio zana ya kumkumbusha mwanadamu hakika na ukweli kuwa yeye ni mja na mtumwa anayemilikiwa na Allah. Aendelee kuukiri ukweli huu usio na mjadala, kila harakati na mishughulisho ya maisha inapomsahaulisha ukweli huu, swala hujitokeza na kumkumbusha tena, naye husema awapo ndani ya swala! ‘ WEWE TU NDIYE TUNAYEKUABUDU NA WEWE TU NDIYE TUNAYEKUOMBA MSAADA’ (1:5). Kwa hiyo, swala humfanya mwanadamu kuyakinisha kuwa hakuna msaidizi wala mneemeshaji wa kweli ila ni Allah pekee. Hata kama ataona katika maisha yake ya kila siku vitu/mambo/sababu ambazo kwa sura ya nje huonekana kuwa ndizo zinazomsaidia na kumneemesha. Lakini ukweli unabakia pale pale  kwamba ni Allah pekee ndiye aliyemuumbia vitu, mambo au sababu hizo zote.

 Kazi inaposahaulisha mwanadamu na kumfanya aamini kuwa kazi ndio inayompatia riziki na kuisahau nguvu iliyo nyuma ya kazi, hapo ndipo huja swala na kufanya kazi yake. Ikamkumbusha kuwa msababishaji na muunganishaji wa riziki na kazi ni Allah pekee ambaye ni yeye tu ndiye mpaji riziki, Mneemeshaji, Msaidizi, Mwenye kudhuru na kunufaisha, Mtoa uhai na Mfishaji, KWA YAKINI ALLAH NDIYE MTOAJI WA RIZIKI MWENYE NGUVU, MADHUBUTI “ (51:58).


TUJIFUNZE NA TUKUBALI kuwa SWALA ndio mbolea na chakula cha imani ya Muislamu Bila ya chakula hicho, Uislamu haumei na kuota katika moyo wa mtu huyo.  


Forum | Guestbook | Tuandikie |