|
4.
KUELEKEA QIBLAH.
Hii
ndio sharti ya nne na ya mwisho miongoni mwa sharti za kusihi swala.
Makusudi ya Qiblah ni Alka’aba tukufu; yaani Qiblah kiwe mbele yake
makati wa kusali akielekee.
Mafaqihi;
wataalamu wa fani ya fiqhi, wamekongamana na kuwafikiana kuwa
inamuwajibikia mwenye kutaka kuswali kuuelekea msikiti mtukufu wa makkah
ambamo humo ndimo ilimo Al-ka’aba. Kongamano hili linatokana na kauli ya
Mwenyezi Mungu mtukufu ndani ya Qur-ani: “KWA YAKINI TUKIONA
UNAVYOGEUZAGEUZA USO WAKO MBINGUNI. BASI TUTAKUGEUZA KWENYE KIBLA
UKIPENDACHO BASI GEUZA USO WAKO UPANDE WA MSIKITI MTAKATIKFU (Al-Ka’aba)
NA POPOTE MNAPOKUWA ZIELEKEZENI NYUSO ZENU (wakati wa swala) ULIKO
(Msikiti huo) ---“ [2:144]
Dalili
na ushahidi wa kuelekea Qiblah ndani ya Sunnah kwamba Mtume Rehema na
Amani zimshukie alimwambia swahaba aliyekuwa akimfundisha namna ya
kuswali: “Unapotaka kuswali, eneza udhu (tawadha udhu kamili), kisha
elekea Qiblah na ulete takbirah”. Bukhaariy na Muslim.
Muradi
wa “mtakatifu” uliotajwa katika aya na “Qiblah” katika hadithi ni
Al-Ka’abah. Mtu mwenye kuiona Al-Ka’abah hii hapa mbele yake
inamuwajibikia aielekee dhati yake na asiyeiona yuko mbali
kinachomuajibikia ni kuelekea tu upande iliko Al-Ka’abah kama
ilivyoelezwa na aya. Mtu asiyejua upande kilipo Qiblah na asimpate mtu wa
kumuuliza kutamuwajibikia kujitahidi ndipo aswali kuelekea upande
anaodhania kuwa ndio upande wa Qiblah na swala yake itakuwa ni sahihi.
Lakini itakapombainikia ndani ya swala kwamba amekosea, kwa yakini upande
ule sio upande wa Qiblah pale pale swala yake itabatilika na itampasa
aianze swala yake upya kwa kuelekea upande ambao ana yakini kuwa ndio
Qiblah. Hukumu itakuwa ni hii hii. Pia kama atakuwa na yakini ya kukosea
hata baada ya kumaliza kuswali. Ama kosa lenyewe likiwa linatokana na
dhana tu na sio yakini, basi hapana kurejea swala.
IX/.
NGUZO ZA SWALA.
Maana
ya nguzo.
Kabla hatujaanza kuzielezea na kuzichambua nguzo za swala moja baada
ya nyingine ni vema kwanza tukajua nguzo ni nini nguzo ya kitu ni ile
sehemu ya msingi ya kitu hicho kama vile kuta na msingi katika nyumba. Kwa
hivyo basi nguzo ni kile kitu cha msingi ambacho upatikanaji wa jambo/kitu
Fulani unakitegema. Rukuu na sijida, hizi ni baadhi ya sehemu za msingi
zinazoijenga swala, nazo ndizo zinazoitwa nguzo za swala, swala
haikamiliki wala kusihi ila kwa kutimia nguzo zake zote kwa namna na
utaratibu uliopokewa kutoka kwa mtume wa Allah Rehema na Amani zimshukie
kama nae alivyopokea kutoka kwa Jibril Amani ya Allah imshukie. Kwa
kufupi, nguzo za swala ni kumi na saba, kama ifuatavyo.
1.
NIA.
Hii
ndiyo nguzo ya kwanza ya swala.
Maana
ya nia kwa ujumla.
Hili ni kusudio la kutenda jambo/kitu Fulani hali ya kulikutanisha kusudio
hilo na kitendo makusudi (kilichokusudiwa)
Maana
ya nia katika swala.
Ni katika swala ni kuhudhurisha mwenye kuswali moyoni mwake kuingia ndani
ya swala anayotaka kuiswali.
Mahala
pa nia ni moyoni na wala haikushurutizwa kuitamka kwa ulimi katika
kuithibitisha nia ijapokuwa ni bora zaidi
kukitamka kile anachokinuia, kwa mfano atasema anapotaka kuswali
swala ya Ishaa.
USWALLIY
RBAA RAKAAT FARDWHWAL ISHAAI LILLAAHI TAALA.
Akiwa anamfuata Imam atasema
MAAMUMA
Na
iwapo yeye ndiye Imam aseme
IMAAMA
Miongoni
mwa dalili zinazothibitisha kwamba nia ni nguzo ya swala ni kauli yake
Bwana Mtume Rehema na Amani zimshukie: bila ya shaka kusihi kwa matendo
yote kumefungamana na nia ---” Bukhaariy na Muslim.
Ili
nia isihi ni lazima ikutanishwe na “Takbiyratul-Ihraam” – Takbira ya
kuhirimia swala.
TANBIHI:
Haitoshi tu ile nia anayotoka nayo mtu nyumbani kwenda msikitini
kuswali. Hii kwa yakini si nia
bali ni AZIMIO kwa kuwa bado haijakutanishwa na kitendo chake ambacho ni
swala yenyewe ambayo haianzii nyumbani kwake mtu. Mwenye kuswali inampasa
asite kidogo kabla ya kuleta Takbiratul - Ihraam aihudhurishe nia ya swala
anayotaka kuiswali kwa kuyatamka moyoni au moyoni na ulimini mfano wa
maneno tuliyoyataja hivi punde tu. Hii ni kwa sababu nia aliyotoka nayo
mtu nyumbani kuja msikitini ina kazi nyingine maalum ambayo sio ile ya
wajibu wakati wa kuleta Takbiyratul-Ihraam. Hivyo ndiyo inavyofahamisha
hadithi sahihi ya Bwana Mtume - Rehema na Amani zimshukie
“Atakayejitwaharisha nyumbani kwake, kisha akaenda katika nyumba
mojawapo miongoni mwa majumba ya Mwenyezi Mungu. Zitakuwa Khatua zake
mbili, moja inaporomosha dhambi moja na ile nyingine inainua daraja
moja”. Bukhaariy na Muslim.
Hii
ndiyo kazi ya nia anayotoka nayo mtu nyumbani kwake kwenda msikitini
kuswali . Nia ya swala inayozingatiwa kisheria ni ile inayokutanishwa na
Takbria ya kuhirimia swala.
2.
KUSIMAMA KWA MWENYE KUWEZA KATIKA SWALA YA FARDHI.
Kuswali kwa kusimama katika swala ya fardhi ndiyo nguzo ya pili ya
swala. Nguzo hii inamuhusu mtu aliye mzima, anayeweza kusimama bila ya
taabu. Haya ni kwa mujibu wa
kauli tukufu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ndani ya Qur-ani Tukufu.
“ANGALIENI SANA SWALA (Zote kuziswali, khasa jamaa) NA (khasa) ILE SWALA
YA KATI NA KATI NA SIMAMENI KWA UNYENYEKEVU KATIKA KUMUABUDU ALLAH”
(2:238).
Mradi na mapendeleo ya kauli
(NA SIMAMENI KWA UNYENYEKEVU) ni kisimamo cha ndani ya swala.
Dalili ya nguzo hii katika sunna. Imepokelewa na Imraan Ibn
Huswayn-Allah amuwiye radhi - amesema: Nilikuwa na maradhi ya Bawasiri,
nikamuuliza Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie - juu ya swala
(niswali vipi)? Akanijibu” Swali kwa kusimama, ikiwa hauwezi (kusimama)
swali kwa kukaa na kama hauwezi (kukaa) basi swali kwa kulalia ubavu”.
Bukhaariy
Mtu atazingatiwa kuwa amesimama pale atakapokuwa
amenyooka wima, hakuinamia mbele au nyuma, kuliani na kushotoni.
Akisimama kwa kupinda/kuinama japo kidogo bila ya udhuru kama uzee au
maradhi swala yake itabatiklika, kwa sababu ya kukosekana nguzo ya
kusimama ambayo ni sehemu inayounda swala.
Mtu akiweza kuswali kwa kusimama katika baadhi ya swala na
kushindwa katika baadhi nyingine, huyu atasimama pale awezapo kusimama na
atakaa pale asipoweza.
Ama kwa upande wa swala za sunnah, inajuzu mtu kuziswali akiwa
amekaa hata kama anaweza
kusimama. Lakini atambue kuwa thawabu
anazozipata kwa kuswali akiwa amesimama ni nyingi zaidi kuliko zile
atakazozipata kwa kuswali akiwa amekaa. Haya yanatokana na kauli ya
Bwana Mtume - Rehema na Amani zimshukie: “Atakayeswali kwa
kusimama ndio bora, na atakayeswali kwa kukaa ana nusu ya ujira wa
aliyesimama , na mwenye kuswali kwa kulala ana nusu ya ujira wa
aliyekaa” Bukhaariy.
TANBIHI:
Atakayeshindwa kusimama katika swala ya fardhi na akaswali kama awezavyo
kwa kuwa “ALLAH HAIKALIFISHI NAFSI YOYOTE ILA YALIYO SAWA NA UWEZA
WAKE.........” (2:286) atapata ujira
wake kamili sawa na yule aliyesimama. Hivyo ndivyo inavyosema
hadithi iliyopokelewa na Abu Muusa Al-ash-ariy-Allah amuwiye radhi -
kwamba Mtume–Rehma na amani zimshukie - amesema .”Mja atakapoumwa au
kusafiri, Mwenyezi Mungu atamuandikia (thawabu) za aliyokuwa akiyatenda
naye mzima mkazi (haumwi na hayuko safarini] “ Bukhaariy.
|