|
Iqaamah kama ilivyo adhana ni
suna muakadah (kokotezwa) katika swala za fardhi
zinazoswaliwa ndani ya wakati wake (Adaa) au
zinazoswaliwa nje ya wakati wake (Qadhwaa).
Iqaamah ni suna kwa jamaa na mwenye kuswali
pekee kwa watu wanamume na wanawake. Iqaamah ni
mithili ya adhana ila kwa tofauti chache
zifuatazo:-
Matamko ya adhana ni mara mbili
mbili wakati ambapo matamko ya Iqaamah ni mara
moja moja tu. Dalili juu ya hili ni hadithi ya
Anas-Allah amuwiye radhi: “Bilali aliamrishwa
kuifanya shaf-i adhana na kuiwitirisha iqaamah,
ila tamko la iqaamah (Qad Qaamatis-swalaah)”.
Bukhaariy & Muslim
Shaf-i ni hesabu iwezayo
kugawika kwa mbili, na witri ni ile isiyogawika
kwa mbili.
TAMKO LA IQAAMAH:
Lifuatalo ndilo tamko kamili la
iqaamah kama lilivyothibiti katika hadithi
nyingi sahihi zilizopokelewa na maimamu
Bukhaariy, Muslim na wengineo:
ALLAAHU AKBAR ALLAAHU AKBAR,
ASH-HADU AN LAA ILAAHA
ILLAL-LAAH,
ASH-HADU ANNA MUHAMMADAN
RASUULULLAAH,
HAYYA ALAS-SWALAAH, HAYYA
ALAL-FALAAH,
QAD QAAMATIS-SWALAAH, QAD
QAAMATIS-SWALAAH,
ALLAAHU AKBAR ALLAAHU AKBAR,
LAA ILAAHA ILLAL-LAAH.
Adhana hutolewa kwa sauti ya
taratibu (kuvuta kidogo) wakati ambapo iqaamah
hutolewa kwa sauti ya haraka kidogo. Hii ni kwa
sababu falsafa ya adhana ni kuwaita walio mbali,
kwa hiyo njia ya utuvu wa sauti (Tartiyl) ikawa
ndio ifikishayo zaidi wito. Na iqaamah
inakusudia kuwainua watu waliohudhuria mahala pa
swala kuswali, kwa hiyo ikawa kutolewa kwa sauti
ya haraka haraka mithili ya mtu aamrishaye ndio
kunanasibikiana zaidi na hali hii. Hivi ndivyo
Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-alivyomwambia Bilali-Allah amuwiye
radhi: “Utapoadhini fanya utuvu (taratibu) na
utapokimu fanya haraka”. Tirmidhiy
Mtu aliyepitwa na swala na
akataka kuzikidhi (kuziswali nje ya wakati
wake), ataadhini kwa ajili ya swala ya mwanzo tu
na atakimu kwa kila swala. Ushahidi wa hili ni
kwamba Mtume-Rehema na Amani zimshukie:
“Alijumuisha Muzdalifah baina ya swala ya
Maghribi na ile ya Ishaa kwa adhana moja na
iqaamah mbili”. Muslim
SHARTI ZA IQAAMAH:
Sharti za iqaamah ndizo zile
zile sharti za adhana, zirejee katika somo la
adhana utazikuta. Hakuna sababu wala dharura ya
kurudia kuzitaja tena hapa.
SUNA ZA IQAAMAH:
Hizi nazo ni zile zile suna za
adhana isipokuwa hapa katika iqaamah kuna ziada
kama ifuatavyo:-
MUADHINI KUTAWALIA IQAAMAH:
Ni bora mtu aliyeadhini ndiye
akimu swala kwa kufuata suna ya Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie:
“Atakayeadhini ndiye atakayekimu”. Lakini
akiadhini mtu mmoja na akakimu mwingine itajuzu.
KUJIBU IQAAMAH:
Kumesuniwa kwa mwenye kuisikia
iqaamah kusema: “AQAAMAHALLAAHU WA
ADAAMAHAA” Abuu Daawoud
KUBADILISHA MAHALA PA ADHANA NA
IQAAMAH:
Ni suna iqaamah isiwe mahala pa
adhana, yaani mtu akiadhini hapa basi akakimu
kule. Asiadhini na kukimu sehemu hiyo hiyo,
usuna huu haulengi kuibatilisha adhana na
iqaamah vilivyofanywa mahala pale pale. Bali
unakusudia kueleza ilivyo bora na suna ni vipi.
Na iqaamah iwe kwa sauti ya chini zaidi kuliko
ile ya adhana.
IDHINI YA IMAMU KATIKA IQAAMAH:
Muadhini hapaswi kukimu swala
ila kwa idhini ya imamu, kwani hivyo ndivyo
alivyokuwa akifanya Bilali; muadhini wa Mtume.
Katika hadithi ya Ziyaad Ibn Al-Haarith amesema:
“Nikawa ninamwambia Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-nikimu nikimu?”
Kadhalika amesema Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Muadhini
ndiye mwenye haki ya kumiliki adhana na imamu
ndiye mwenye kumiliki iqaamah”. Ibn Adiy
MAAMUMA WASIINUKE KABLA YA IMAMU
WAO:
Itapokimiwa swala, maamuma
wasiinuke mpaka ainuke imamu wao kwanza au
awaruhusu kuinuka kabla yake. Haya yanatokana na
kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie: “Itakapokimiwa swala, msiinuke
mpaka mnione mimi (nimeinuka)”. Bukhaariy
& Muslim
Maamuma wanatakiwa kuinuka
kuswali mara baada ya kumalizika kwa iqaamah,
hivi ni iwapo wamo msikitini pamoja na imamu
wao.
TANBIHI:
Kunashurutizwa kutokuwepo mwanya
mrefu baina ya iqaamah na swala, na mwanya
ukirepa (ukirefuka) au likapatikana tendo
linalohesabiwa kuwa ni mkata iqaamah. Tendo hili
ni kama vile mtu kula baada ya iqaamah, katika
hali na mazingira kama haya kutapasa kuirudia
tena iqaamah.
Ni suna imamu kuhirimia swala
mara tu baada ya kumalizika kwa iqaamah. Asiache
mwanya mrefu baina ya iqaamah na ihraamu ila kwa
kiasi cha kujishughulisha na jambo la suna.
Mithili ya imamu kuwaamrisha maamuma wake
kunyoosha safu zao, ageuke kuliani na kushotoni
kwake akisema: ISTAWUU RAHIMAKUMULLAAH. Maana:
Linganeni sawa, Allah akurehemuni. Katika suala
hili, Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alikuwa akisema kuwaambia maswahaba
wake: SAWUU SWUFUUFAKUM, FAINNA
TAS-WIYATIS-SWAFFI MIN TAMAAMIS-SWALAAH”.
Bukhaariy & Muslim.
Haijuzu iqaamah ya mwanamke kwa
mwanamume.
KIAMBATISHI
ADHANA ISIYO YA SWALA:
Kumesuniwa kutolewa adhana pindi
kutakapotokea katika jamii ya waislamu mambo
kadhaa mbali ya swala. Mambo hayo yaliyosuniwa
adhana ni pamoja na:-
Kumuadhinia mtoto katika sikio
lake la kulia mara tu baada ya kuzaliwa, kama
ambavyo ni suna kuleta iqaamah katika sikio lake
la kushoto. Suna hii inatokana na kitendo cha
Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-kumuadhinia sikioni mjukuu wake;
Hassan alipozaliwa na Bibi Faatimah (bintiye).
Riwaya hii ameipokea imamu Tirmidhiy
Adhana wakati linapotokea janga
la moto. Falsafa ya adhana hii ni kuwaita
waislamu kuja kutoa msaada wa uokozi na kuzima
moto.
Adhana wakati wa vita. Falsafa
ya adhana hii ni kuwakusanya waislamu kwa lengo
la kwenda vitani kuihami dini ya Allah.
Kumuadhinia mtu aliyeanguka
mweleka, mtu aliyeghadhibika mno, mtu mwenye
tabia mbaya na mtu aliyesibiwa/aliyekumbwa na
shetani wa kijini. Falsafa ya adhana hii ni
kuwaondoshea shari watu hawa kwa utajo huu wa
Allah, hii ni kwa sababu shetani hukimbia mbali
anapoisikia adhana.
b). WITO WA SWALA ZISIZO ZA
FARDHI:
Imethibiti kutokana na maelezo
yetu yaliyotangulia kwamba adhana na iqaamah ni
suna zilizokokotezwa (Muakadah) kwa swala za
fardhi. Ama swala nyingine zisizo za fardhi na
ambazo zimesuniwa kuswaliwa jamaa mithili ya
swala za Eid mbili (Eid ya mfunguo mosi baada ya
Ramadhan na ile ya mfunguo tatu baada ya
hijjah). Swala za jua kupatwa na mwezi na mwezi
kupatwa na jua na swala ya jeneza. Hizi
hazikusuniwa ndani yake adhana wala iqaamah,
bali wito wake ni mtu kusema: AS-SWALAATU
JAAMI’AH. Imepokewa kutoka kwa Abdullaah Ibn
Amrou-Allah amuwiye radhi-amesema: Wakati jua
lilipopatwa katika zama za Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-kulinadiwa: As-swalaatu
jaami’ah”. Bukhaairy & Muslim
Ichukuliwe swala hii ya kupatwa
kwa jua kama mizani ya kupimia swala nyingine za
suna zilizosuniwa kuswaliwa jamaa.
|