Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Fiqh na Sheria  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

VI /. SABABU ZA  SIJIDA YA KUSAHAU :

 

3. Kutenda kitendo kilichokatazwa  kwa  kusahau,  ikiwa  makusudi  yake   hubatilisha  swala. Mithili  ya mwenye kuswali kuzungumza maneno   machache au kuongeza rakaa moja kwa  kusahau. Kisha akazinduka na kutambua  kuwa yumo ndani  ya swala, huyu katika  mazingira haya  ataleta  sijida mbili za  kusahau.

4.Kugurisha/kuhamisha kitu miongoni mwa  matendo ya swala kukipeleka mahala si  pake. Kikiwa kitu hicho ni nguzo/faradhi au  ni suna ya “Ba’adh”.  Mfano wa haya  ni mtu  kusoma  Suuratil–Faatihah   (Al-hamdu) katika  kikao (mkao) cha Tashahudi badala  ya  mahala  pake ambapo ni katika Qiyaamu (kisimamo  cha   swala). Au mtu kusoma Qunuut katika  rukuu badala ya mahala  pake ambapo ni  katika  Itidali ambayo huja baada ya kurukuu.  Au mtu kuisoma  sura ambayo ni suna, kuisoma  baada ya Al-hamdu katika Itidali badala ya  mahala pake  ambapo ni katika  Quyaamu. Ni suna kwa mtu huyu kusujudu sijida mbili za kusahau mwishoni mwa swala yake  kutokana  na kuyafanya haya.

 

vii/. NAMNA  YA KUSUJUDU SIJIDA ZA KUSAHAU  NA MAHALA PA KUSUJUDU:

          Kusujudu kwa kusahau   ni sijida mbili kama  sijida nyingine za swala. Mwenye  kuswali atanuia kwa sijida mbili hizo kusujudu  kwa kusahau. Na mahala pa kusujudu ni  mwishoni mwa  swala yake  kabla ya  kutoa  salamu. Angalia  lau mwenye kuswali  atatoa salamu kabla ya  kusujudu kwa  makusudi  au  kwa kusahau na muda (kitambo) ukarepa  (ukarefuka), itafutu sijida  hiyo. Kama  utakuwa  haukupita muda mrefu, itamuelea  kuidiriki  sijida  ya kusahau kwa kusujudu  mara mbili kwa nia ile ile ya kusahau,  kisha atoe salamu kwa mara nyingine tena.

 

TANBIHI:

1.Kama  mwenye   kuswali hakuleta sijida ya  kusahau ambayo hukumu yake  ni suna,  swala yake haitabatilika. Hii ni kwa  sababu  sijida ya kusahau  haikuwekwa  kwa ajili ya  kuacha tendo la wajibu.

2. Ama mwenye  kuswali atapoacha mojawapo ya  nguzo  za swala  kama rukuu au kusoma  Al-hamdu. Basi hana budi  kuileta nguzo hiyo aliyoiacha wala kusujudu kwa kusahau  hakutakuwa kiungo cha  nguzo hiyo. Bali  sijida mbili za kusahau zitakuja baada  ya  kuileta hiyo   nguzo  aliyoisahau.

KIAMBATISHI

SIJIDA ZA MSOMO.

Ni suna thabiti kutoka kwa Bwana  Mtume–Rehema na Amani zimshukie–kusujudu  sijida ya msomo. Suna hii inawahusu wote  wawili; msomaji wa Qur-ani na msikilizaji, iwe ni ndani ya  swala au nje ya swala.

 

I/. SABABU YA  KUSUJUDU SIJIDA YA MSOMO:

    Suna ya sijida ya msomo inapatikana kwa moja ya mambo mawili haya:-

1.Kusoma aya ya Qur-ani ambayo ndani yake  kuna paliposuniwa kusujudu, au

2.Kuisikia aya hiyo ikisomwa na mtu mwingine.

 

II/. DALILI/USHAHIDI   WA SIJIDA YA MSOMO:

          Kama tulivyokwishaeleza kwamba     sijida ya msomo ni suna iliyothibiti kutoka  kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Na  ushahidi ni hadithi zifuatazo:-

  • Imepokelewa kutoka kwa Ibn Umar–Allah awawiye radhi– amesema: Alikuwa Mtume wa Allah–Rehema  na Amani zimshukie –akitusomea sura ambayo ndani yake kuna sijida. Basi (hapo) husujudu nasi husujudu (pamoja  nae) kiasi  hata mmoja wetu hapati mahala pa kuliweka paji lake la uso (kutokana na  wingi wa watu)”.

  • Na katika riwaya iliyopokelewa na Abuu  Daawoud: “Mtume– Rehema  na Amani  zimshukie-alikuwa akitusomea Qur-ani. Anapoipitia (aya ya) sijida  hukabiri na  kusujudu, nasi  tukasujudu pamoja nae”.

 

III/. FADHILA  ZA SIJIDA YA MSOMO:

          Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema  na Amani zimshukie–amesema: “Mwanadamu ataposoma aya ya sijida na  akasujudu, shetani hujitenga na kulia akisema:  Ee ole wangu, mwanadamu ameamrishwa  kusujudu  akasujudu, basi yamuelea kupata    pepo ya  Allah.Nami  nimeamrishwa kusujudu  nikakhalifu amri ya (Mola  wangu ), basi nitaingia motoni”. Muslimu.

 

IV/. HUKUMU  YA  SIJIDA YA MSOMO:

          Sijida ya msomo hukumu yake ni  suna ambapo mtu akisujudu hupata thawabu  na akiacha kusujudu hapati dhambi. Lakini  tu atakuwa amejidhulumu mwenyewe fursa  ya kujaza na kuithakilisha  mizani yake ya kheri. Dalili ya  haya ni hadithi zifuatazo:-

  • Imepokelewa  na Sayyidna Umar–Allah  amuwiye  radhi–amesema Mtume wa Allah–Rehema na  Amani zimshukie: “Enyi watu hakika sisi (tunaposoma Qur-ani) tunazipitia aya  za sijida. Atakayesujudu (mahala  hapo) hakika atakuwa  amesibu (amepatia )  na asiyesujudu, basi hapana  dhambi juu yake”.  Bukhaariy

  • Na  imekuja katika riwaya ya Ibn Umar–Allah awawiye  radhi:   “Hakika hakutufaradhishia  kusujudu ila tutakapo”.

 

V/. SHARTI ZA SIJIDA  YA MSOMO:

          Sharti zilizoshurutizwa katika sijida ya msomo ni nafsi  ya  sharti  zilizoshurutiziwa swala. Sharti hizo  ni pamoja  na

  • twahara ya hadathi ndogo na kubwa.

  • Kuelekea Qiblah wakati wa   kusujudu, na

  • Kusitiri tupu.

Na baki ya sharti nyingine zilizotajwa katika kusihi kwa swala.

 

VI/. NAMNA  YA KUSUJUDU SIJIDA YA MSOMO.

          Ni kusujudu  msomaji na msikilizaji wa Qur-ani anapoifia    aya  ya  sijida. Kusujudu sijida moja iliyo baina ya takbira mbili,  takbira ya kuliweka paji la uso juu ya  ardhi  na  takbira ya  kuliinua kutoka hapo. Kisha  hutoa salamu na wala hasomi Tashahudi.  Imependelewa kwa mtu mwenye kusujudu sijida  ya msomo amuombe Allah kwa dua njema, hii  ni kwa sababu katika sijida ndipo mahala   mja huwa karibu zaidi na Mola  wake. Kwa mantiki hii na kujibiwa dua  akiomba pia huwa karibu zaidi mahala hapo kuliko mahala pengine.

 

VII/. MAHALA ZILIMO SIJIDA ZA MSOMO:

          Jumla ya sijida za msomo ndani ya Qur-ani  Tukufu ni kumi na tano kama ifuatavyo:-

          SURA                       AYA

  1. Al-a’araaf                  (7)      :206

  2. Ar–ra’ad                   (13)    :15

  3. An-nahl                     (16)    :49

  4. Bani  Israil                 (17)    :107

  5. Maryam                    (19)    :58

  6. Al–Hajj                     (22)    :18

  7. Al–Hajj                     (22)    :77

  8. Al–Furqaan               (25)    :60

  9. An–naml                   (27)    :25

  10. As-sajdah                 (32)    :15

  11. Swaad                      (38)    :24

  12. Fuswilat                    (41)    :37          (Ha-Miym–sajdah)

  13. An–najm                   (53)    :62

  14. Al-inshqaaq              (84)    :02

  15. Al-alaq                     (96)    :19

 


 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |