Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

UISLAMU NA SUALA LA HIJABU-II

 

Hijabu ambayo Uislamu umeifaradhisha na kumuwajibisha mwanamke, hamtakii mwanamke huyu ila kulinda na kuchunga heshima yake na utu wake kupitia uvaaji, sauti na kuchanganyika kwake na jinsia ya kiume ili asibughudhiwe na jinsia hiyo  na asiwe yeye ndio  kichocheo cha fitina na fisadi katika jamii.  Kwa mantiki hii tunaruhusika  kusema  kwa kinywa kipana kabisa kwamba hijabu ya Kiislamu ni HIFADHI  na HIMAYA kwa wanawake na wala sio KIFUNGO AU KIPINGAMIZI cha kusitisha na kuzuia harakati za mwanamke katika kuchangia maendeleo yake binafsi na yale ya jamii kwa ujumla.  Kama ambavyo Hijabu isivyomzuia mwanamke kufanya shughuli za ndani ya  nyumba yake ndivyo hivyo hivyo haimzuii kufanya kazi nje ya nyumba yake ingawa kubakia nyumbani ni bora zaidi kwake kuliko huko kutoka, kutoka kwake nje ya nyumba yake ni pale atakapokuwa na haja ya kufanya kazi ili kujikimu kimaisha au kazi hiyo inamuhitajia  yeye kwa maana kuwa hakuna afaaye kwa kazi hiyo ila ni yeye tu.   Ni katika mazingira haya na yenye ndio mwanamke wa Kiislamu mwenye kumuamini ALLAH na siku ya mwisho anaweza kutoka nje ya nyumba yake.  Sheria inaliweka na kulirejesha suala hili katika maafikiano na  mapatano baina ya mke na mumewe au binti na walii wake lakini chini ya msingi ya sheria na sio chini ya matashi na matakwa yao.  Hali kadhalika linarejea kushabihiana nayo katika wajibu na majukumu ya kila mmoja wao yaani mke  na mume katika nyumba na maisha kwa ujumla.

Ama suala la kufanya kazi kisheria ni haki na wajibu wa  kila mtu bila ya kujali jinsia yake muda wa kuwa kazi/shughuli hiyo:-

  • Anaiweza na kuimudu

  • Inalingana na maumbile yake ya asili

  • Inampa maslahi sambasamba na kuchunga utu na heshima yake.

  • Haina madhara kwake wala kwa jamii

Mwenyezi Mungu Mtukufu anatuambia kuhusiana na amali njema na kazi ikiwa ni miongoni mwa hizo amali njema, tusome na tujifunze: “WAFANYAJI MEMA, WANAUME AU WANAWAKE HALI YA KUWA NI WAISLAMU, TUTAWAHUISHA MAISHA MEMO, NA TUTAWAPA UJIRA WAO (Akhera)  Mkubwa  (16:97).

Tujifunze kupitia aya hii:-

  • Usawa wa Mwanamume na mwanamke katika kutenda amali njema (pamoja na kazi)

  •  Kufanya kazi ni katika jumla ya matendo ya dini kama mfumo sahihi na maisha .

  •  Kufanya kazi katika misingi na mazingira ya Kiislamu.

  •  Kazi ni sababu (wasila) ya kupatia maisha mema leo duniani na kesho akhera.

Tuendelee kuogelea katika bahari ya kazi ndani ya Qur-ani Tukufu “MOLA WAO AKAWAKUBALIA”  ( Maombi yao kwa kusema )  “HAKIKA MIMI SITAPOTEZA JUHUDI” (Amali) YA MFANYA JUHUDI MIONGONI MWENU, MWANAUME AU MWANAMKE, NYINYI  KWA NYINYI

Tumefahamu kupitia aya hii:-

  •  Juhudi (amali)/kazi) ya mwanamume na mwanamke ni sawa katika mizani ya Allah.

  • Ahadi ya Allah kuilipa juhudi ya kila mfanya juhudi bila ya kuangalia jinsia yake.

Kauli jumla ni kuwa hakuna aya ndani ya Qur-ani  Tukufu  au hadithi katika sunnah ya Mtume – rehema na Amani zimshukie – inyomnyima mwanamke haki yake ya kusoma na kufanya kazi.   Huu ndio ukweli na Historia inaukiri na kuukubali.  Hebu tuzipekue kwa pamoja kurasa za historia ziturejeshe katika zama za Bwana Mtume.  Tuione nafasi ya mwanamke na mchango wake katika jamii ile.   Kumbukumbu sahihi za kihistoria zinamuonyesha mwanamke wa Kiislamu zama za Mtume akibeba majukumu na kushiriki katika shughuli mbalimbali  za kijamii. Tunamkuta  mwanamke hata katika midani  ya vita kama  muuguzi akiwatibu majeruhi wa vita na yote  hii ni katika kutekeleza Uislamu kivitendo.

Lakini pamoja na ruhusa hii ya kutoka nje na  kufanya kazi aliyopewa mwanamke na Uislamu  bado hatuwezi kuukana  ukweli unaosisitizwa na Uislamu kuwa nafasi ya mwanamke  ndani ya nyumba yake ni bora zaidi kuliko nafasi yake ya nje  nyumba.Ukweli huu unadhihishwa na kujitokeza kupitia kauli ya Bwana  Mtume Rehema na Amani zimshukie: Wanawake ni vivutio, na hakika Mwanamke  hutoka nyumbani mwake bila ya kukusudia  ubaya  wowote. Basi Shetani humchomozea  na kumatangulia na kumwambia : Hakika  wewe humpitii yeyote ila atapendezwa  nawe. Na hakika mwanamke atavaa nguo  zake kisha aulizwe : Unakwenda wapi?  Aseme ( Ajibu ) Nakwenda  kumtazama mgonjwa, au nakwenda mazikoni, au nakwenda kuswali. Mwanamke   hakumwabudu  Mola  wake  kama anavyoabudu nyumbani mwake". Twabaraany.

Utokaji wa mwanamke nje ya nyumba yake  unaweza kuwa ni wajibu  kwa maana ya  wajibu. Vipi , maana inawezekana  kabisa Mwanamke  akawa hana mtu wa kumkimu kimaisha baada ya kufiwa na mumewe au Baba yake na pengine  ana watoto na wazazi wanaomtegemea. Hapa katika mazingira haya na yenye kushabihiana  nayo lazima bali ni wajibu kwake  atoke nje kufanya  kazi kwa ajili ya kujimu yeye mwenyewe a wanaomtegemea .

Imethibiti katika riwaya iliyopokelewa na  Imani Bukhaariy -Allah amrehemu kutoka  kwa Biaysha  amuwiye radhi – kwamba Bwana Mtume- Rehema na Amani zimshukie – aliwaruhusu /aliwapa idhini wakeze kutoka nje kwa ajili ya kudhi  haja zao ( mahitaji) mbali mbali. Kadhalika ni wajibu mwanamke  atoke nje kwenda kutafuata elimu ambayo  haipatikani ndani ya nyumba yake , hii ni kutokana na ukweli kuwa kutafuta elimu  ni faradhi ya lazima mno katika Uislamu.

Zama za Bwana Mtume wanawake walikuwa  wakitoka kwenda kumuuliza Mtume, mambo mbali mbali yahusianayo na dini  kutokana na kiu na pupa yao ya kutaka kuijua dini yao waliomba wapewe siku yao maalum ili waweze kumuuliza Mtume  mambo ya ndani yanayomhusu wanawake ambayo ni aibu kuyasema mbele ya wanaume. Hii ndio sababu Bwana Mtume aliwakataza  waume kutowazuia wake zao kwenda Msikitini watakapowaomba ruhusa . Kwa  sababu kwenda kwao Msikitini hakukuwa ni kwa ajili ya swala tu, kwani kama ni hivyo basi  kuswali kwao majumbani mwao ni bora na  na kuna thawabu zaidi kuliko Msikitini. Lakini  kwenda kwao Msikitini kulikuwa ni kwa  ajili ya kujifunza dini, kusikiliza wahyi (ufunuo) uliomshukia Mtume na kujifunza  swala Kivitendo nyuma ya mwenyewe Bwana Mtume .  Tumtegee sikio Bwana Mtume Rehema  na Amani zimshukie –akituambia watakapo kuombeni wake zenu ruhusa  ya kwenda  Msikitini basi waruhusuni Muslim. Hii ni kwa sababu ya Msikiti wakati wa  Mtume ulikuwa unamaanisha kila kitu ulikuwa ndio kituo cha kijamii Msikitini  ulikuwa ni:

  • Nyumba ya Ibada

  • Kituo cha elimu ( Shule

  • Idhaa ya Jamii ( Redio) Jengo la mawasiliano

  • Mahakama

  • Khazina ya Jamii

  • Makazi ya masikini na wasiojiweza

  • Bunge la Waisilamu

  • Mahala pa kuliandalia jeshi 

na …………………….na …………………….

Hali kadhalika ni wajibu kwa mwanamke kutoka kwenda kufanya kazi ambayo yeye ana ujuzi nayo na hakuna mtu mwingine anayeweza kuifanya vizuri zaidi ila ni yeye tu na kama hakwenda jamii itaathirika kwa kukosa huduma hiyo.  Kama ambavyo pia ni wajibu atoke kwenda kushiriki katika mambo mbalimbali ya kheri, kutoa msaada wa dharura katika majanga mbalimbali.  Pias mwanamke anaweza kumsaidia mumewe katika shghuli za kutafuta maisha kama inavyokuja katika riwaya ya Bi Asmaa Bint Abu Bakri – Allah awawiye radhi, kwamba Bi. Asmaa alimwambia baba yake; Unanioza Zuberi na il-hali yeye hana mali yoyote, hana mtumwa na wala hana chochote zaidi ya farasi na ngamia wake .   Asmaa anaendelea kusimuliwa (basi baada ya kuolewa) nilikuwa nikimtafutia na kumpa chakula farasi wake huyo na kumpondea na kumlisha tende ngamia wake (pia) na nilikuwa nikichota maji na kutengeneza vifaa vya kutunzia maji. (Pia) nilikuwa nakoboa nafaka na kubeba tende kichwani kutoka shambani.  Mpaka  Abubakri (baba yangu akanionea huruma) na kuniletea mfanyakazi akanisaidia kushughulikia farasi basi ikawa kama vile  amenikomboa.  Siku moja nilikutana na Mtume wa Mwenyezi Mungu Rehema na Amani  zimshukie akiwa na maswahaba wake, nami nikiwa nimejitwika tende kichwani akasema Ikh, ikh, ili amketishe ngamia wake na kunibeba nyuma yake.  Nikaona haya kwenda pamoja na wanamume (nikashindwa kupanda) nikamkumbuka Zuberi (mume wangu) na wivu wake kwani alikuwa na wivu kupindukia.  Bwana mtume akatambua kwamba mimi naona haya (akaenda zake)  Nikafika kwa Zuberi na kumuhadithia yaliyotokea, akaniambia  “WALLAH  Mzigo uliokuwa nao kichwani ulikuwa ni jambo zito zaidi kuliko huko kupanda kwako (ngamia) wake (Mtume) akimaanishia ungepanda tu – Bukhaariy na Muslum.

Tunachojifunza katika hadithi hii ni kwamba:-

  • Kazi ya mwanamke zama hizo ilikuwa ni ya muda (kipindi) maalum.

  • Ilikuwa ni kwa kiasi cha haja tu.

Pamoja na kufanya kwake kazi nje ya nyumba yake bado maswahaba walikuwa wakilichukia jambo hili kwa hoja kuwa linashusha hadhi ya mume machoni mwa jamii.   Kwa kuwa  hili halimaanishi zaidi kuwa yeye kashindwa kumkimu mkewe kwenye kufanya kazi, maadam  kuna haja ya kufanya hivyo.  Hii ni kutokana na ushahidi wa Mtume kumwona Bi. Asmaa akifanya kazi na asimkemee au kumkataza, kwa hivyo ni dhahiri kuwa Mtume alilikiri hilo.  Historia ya Uislamu imesheheni mifano mingi inayoonyesha kujuzu kufanya kazi kwa mwanamke, tuisome na tutaona.

 MADA INAENDELA :  INSHAALLAH !


 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |