|
22. ADABU/UTARATIBU WA
MAJADILIANO/MIDAHALO KATIKA UISLAMU.
Utanngulizi:
KWA JINA LA ALLAH MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.
Sifa zote njema ni za Allah, Mola Mlezi wa viumbe vyote. Na
Rehema na Amani zimshukie Bwana wetu; Mtume wa Allah na wote walio
mkubali na kumfuata mpaka siku ya Kiyama.
Msomaji
mwema
Assalaam Alaykum Warahmatullah Wabarakaatuh!
Baada
ya kukamilika na kutamatia kwa mfululizo wa makala zetu zilizo kuwa
zikikujia chini ya anuani: DA’AWAH (MLINGANO) TIMILIFU NA UKUMBUSHO
ENEVU. Leo tena kwa auni na iraada yake Maulana, mtumishi wa uma;
Website Uislamu, anakuletea mfululizo wa makala mpya, zitakazo kujia
chini ya anuani: ADABU/UTARATIBU WA MAJADILIANO/MIDAHALO KATIKA UISLAMU.
Tunataraji kwa taufiq yake Allah, makala hizi zitakunufaisha,
kukuelimisha na kukufundisha khususan katika kipindi hiki ambacho
kimesheheni mihadhara, midahalo na majadiliano baina ya ama waumini wa
dini moja wao kwa wao au baina ya dini mbili tofauti. Au hata baina ya
waumini wa dini na wale wasio waumini wa dini yoyote kama wanavyo dai,
ingawa huko kutokuwa na dini ndio dini yao.
Tunasema hali ya kutaraji msaada wa Allah na hali ya kuwa Yeye ndiye
Mjuzi mno:
Katika
jumla ya njia/miundo hekima iliyo enda kina kimaana ambayo Qur-ani
Tukufu imeitumia katika kujenga/kusimamisha hoja/dalili juu ya
umoja/upweke wa Allah Ataadhamiaye. Na juu ya ukweli wa mitume watukufu
katika ule ujumbe wanao wafikishia kaumu zao kutoka kwa Mola Muumba wao.
Ni njia/miundo ya majibizano/mijadala/midahalo na mahojiano kwa lengo la
kuifikia na kuidhihirisha haki kwa njia ya ukinaishaji akili na ubaridi
nafsi. Njia ambayo humfanya mdau wake kuishi maisha yake hali ya kuwa yu
thabiti/imara juu ya kile alicho kiamini, uthabiti usio kinzwa na shaka,
wala kuzongwa na fikra dhanifu zisizo na mashiko.
Na
pengine huenda mzizi “KAULI” na maneno (vitenzi/viarifa) vichimbukavyo
katika mzizi huo, mithili ya viarifa: “amesema/alisema”, “anasema”,
“sema”, “wamesema/walisema”, wanasema”, “semeni” na kadhalika. Mzizi
huu wa maneno ambayo unafahamisha juu ya kujibizana/kujadiliana na
kuhojiana na kuhadhirisha baina ya watu katika mambo/masuala maalumu.
Umekaririka na kujirudia rudia mzizi huo na vinyambuliko vyake kwa zaidi
ya mara alfu moja na mia saba. [Rejea AL-MU’UJAMUL-MUFAHRASA
LIAL-FAADHWIL-QUR’AANIL-KARIYM, sahifa 554-578 ya Ustaadh Muhammad Fuad
Abdul-Baaqiy-Allah amrehemu].
Kwa
mfano, tamko “amesema” limekaririka zaidi ya mara mia tano,
miongoni mwa mara hizo ni kauli yake Atukukiaye: “HUKUMWONA YULE ALIYE
HOJIANA NA IBRAHIM JUU YA MOLA WAKE MLEZI KWA SABABU ALLAH ALIMPA
UFALME? IBRAHIM ALIPO SEMA: MOLA WANGU NI YULE ANAYEHUISHA NA
KUFISHA. YEYE AKASEMA: MIMI PIA NAHUISHA NA KUFISHA. IBRAHIM
AKASEMA: ALLAH HULICHOMOZESHA JUA MASHARIKI, BASI WEWE LICHOMOZESHE
MAGHARIBI. AKAFEDHEHEKA YULE ALIYE KUFURU; NA ALLAH HAWAONGOI WATU
MADHAALIMU”. [02:258]
Na
tamko “walisema” limekaririka ndani ya Qur-ani Tukufu zaidi ya
mara mia tatu, miongoni mwake ni kauli yake Atukukiaye: “NA WALISEMA:
HAUTATUGUSA MOTO ILA KWA SIKU CHACHE TU. SEMA: MMECHUKUA AHADI KWA
ALLAH? KWELI ALLAH HATOKWENDA KINYUME NA AHADI YAKE. AU MNAMSINGIZIA
ALLAH MAMBO MSIYO YAJUA?” [02:80]
Na
tamko “anasema/alisema” limekaririka katika Qur-ani Tukufu mara
themanini na sita, miongoni mwazo ni kauli yake Ataadhamiaye: “ILE SIKU
AMBAYO ALLAH ATAKAPO WAKUSANYA MITUME AWAAMBIE: MLIJIBIWA NINI?
WATASEMA: HATUNA UJUZI, HAKIKA WEWE NDIYE MJUZI MKUBWA WA YOTE YALIYO
FICHIKANA”. [05:109]
Na
tamko “sema” limekaririka ndani ya Qur-ani Tukufu kwa zaidi ya
mara mia tatu, miongoni mwa hizo ni kauli yake Atukukiaye: “SEMA:
KITU GANI USHAHIDI WAKE MKUBWA KABISA? SEMA: ALLAH. YEYE NDIYE
SHAHIDI BAINA YANGU NA NYINYI. NA NIMEFUNULIWA QUR’ANI HII ILI KWAYO
NIKUONYENI NYINYI NA KILA INAYO MFIKIA. ATI KWELI NYINYI MNASHUHUDIA
KUWA PAMOJA NA ALLAH WAPO MIUNGU WENGINE? SEMA: MIMI SISHUHUDII
HAYO. SEMA: HAKIKA YEYE NI MUNGU MMOJA TU, NAMI NI MBALI NA MNAO
WASHIRIKISHA”. [06:19]
Namna/muundo wa majadiliano/mdahalo katika Qur-ani Tukufu ni wa pekee
kutokana na ukunjufu wa wigo wake na uwazi wa kadhia/masuala yake na
uenevu wake wa mas-ala mengi yasiyo dhibitika na mtu akayesha. Yamo
mazungumzo/majadiliano baina ya Muumba Mtukufu na viumbe wake miongoni
mwa mitume watukufu, malaika wakurubishwa na shetani mrujumiwa. Na yapo
mahojiano au mazungumzo yanayo jiri kuhusiana na umoja/upweke wa Allah,
au kuhusiana na Qur-ani Tukufu. Au kuhusiana na siku ya mwisho na
yaliyomo ndani yake miongoni mwa thawabu na adhabu. Hali kadhalika yako
mazungumzo/mahojiano baina ya mitume na kaumu zao, au baina ya wema na
waovu, au baina ya wema wao kwa wao, au baina ya waovu na waovu
wenziwao. Kama ambavyo yapo mahojiano/mazungumzo pamoja na watu wa
kitabu (Mayahudi/Manaswara) au pamoja na wanafiki. Au pamoja na
wageza/wafuataji wa wahenga/viongozi wao katika batili/upotofu au pamoja
na wenye kumuuliza Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Na hali
kadhalika yako mazungumzo au maelezo yanayo fungamana moja kwa moja na
shaksiya (dhamira/dhati) ya Mtume au risala (ujumbe) yake. Au na vile
alivyo vihalalisha au kuviharimisha Allah miongoni mwa vyakula, vinywaji
na vinginevyo.
Na
madhumuni/lengo/makusudio ya muhadhara/mdahalo/majadiliano na mazungumzo
kwa mujibu wa Qur-ani Tukufu, ni:
1.
Kuifikia haki na ilivyo
ndivyo/sawa katika maudhui/mada ambayo mitazamo ya watu imetofautiana
ndani yake.
2.
Kumganda hasimu/mpinzani na
kumshinda kwa njia ya kusimamisha nguvu ya hoja na kuleta dalili ya wazi
na ushahidi enevu.
Na
tutaona katika mfululizo wa makala hizi kwa taufiq yake Allah, kwamba
Qur-ani Tukufu katika kuithibitisha haki ambayo Allah amewaamrisha waja
wake kuifuata. Katika hili imetumia miundo/maelezo busara toshelezi,
dalili za wazi wazi kabisa na hoja zenye nguvu zisizo wezwa kukengeukwa
na asiye mlemavu wa akili. Vyote hivyo kwa pamoja vinaikinaisha akili
yenye siha, matashi mema na nyoyo toharifu.
Pia
tutaona kwa auni na iraada yake Allah Ataadhamiaye, ya kwamba Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alivyo fuata nyayo za Qur-ani Tukufu.
Katika kujadiliana na kuzungumza kwake na wafuasi wake wema pia
walikivaa kiatu hicho hicho alicho kivaa yeye na wakaifuata njia yake
kwa kuitendea kazi kauli yake Allah Ataadhamiaye: “HAKIKA NYINYI MNAYO
RUWAZA NJEMA KWA MTUME WA ALLAH KWA ANAYE MTARAJI ALLAH NA SIKU YA
MWISHO, NA AKAMKUMBUKA ALLAH SANA”. [33:21]
Tunamuomba Allah Atukukiaye atuwafikishe kuyatenda yale ayapendayo na
kuyaridhia na aturuzuku unyoofu na utakasifu wa nia katika kauli na
matendo yetu. Hakika Yeye ni Muombwa Mtukufu mno na Mtegemewa bora mno.
|