|
SURA YA KWANZA
Sababu za Ikhtilafu/kutofautiana maoni baina ya watu:
Ikhtilafu/tofauti baina ya watu katika mambo/masuala ya dini
yao na katika kadhia za Dunia yao, ni suala kongwe, la tangu na tangu.
Na tofauti hizi zitaendelea kuishi na kusalikia miongoni mwao mpaka
kumalizika kwa Dunia na vyote vilivyomo humo. Ukweli huu usio kanushika
na akili pevu na hakika hii isiyo katalika, imekokotezwa na kusisitizwa
na Qur-ani Tukufu kupitia aya zake nyingi tu. Miongoni mwa hizo ni kauli
yake Ataadhamiaye: “NA MOLA WAKO MLEZI ANGELI PENDA ANGELI WAFANYA WATU
WOTE WAKAWA UMMA MMOJA. LAKINI HAWAACHI KUKHITALIFIANA ISIPO KUWA WALE
AMBAO MOLA WAKO MLEZI AMEWAREHEMU. NA KWA HIYO NDIO ALLAH AMEWAUMBA...”
[11:118-119]
Yaani –
Ewe Mtume! Mwenye pupa ya kutaka kaumu yako iamini! Lau Mola wako Mlezi
angeli taka kuwafanya watu wote kuwa umma mmoja, wenye kukusanyika juu
ya dini ya haki, basi angeli wafanya kuwa hivyo. Hashidwi, kwani matashi
yake hayana wa kuyazuia, lakini Yeye kutakata na mawi (makosa) ni kwake,
hakulitaka hilo ili falsafa ya kibaya/kiovu kupambanuka na kizuri/chema
idhihiri na kuonekana. Na kwa sababu hiyo basi, watu muda wa kudumu kwa
Dunia hawataacha kukhitalifiana katika fikra zao, mielekeo yao, malengo
yao, matarajio yao, na.......... na.......... Watakao salimika na wimbi
hili la Ikhtilafu, ni wale tu walio patwa na Rehema za Bwana Mlezi wako.
Basi hao wakaiongokea njia ya haki, hakika hao hawajapata kukhitilafiana
katika msingi/shina lolote la dini ya haki, bali huijua njia ya haki
wakaifuata.
Na
tambua na ufahamu ewe ndugu mwema-Allah akurehemu-kwamba hekima ya
Kimungu imetaka watu wawe ni wenye kukhitalifiana. Na kwamba rehema ya
Mola Mlezi wako ambayo imekienea kila kitu, itawakusanya maadam
ikhtilafu zao hizo ni kwa ajili/lengo la kuifikia haki na ilivyo ndivyo.
Na
ifananayo na aya tuliyo tangulia kuinukuu, ni kauli yake Atukukiaye:
“...NA LAU KUWA ALLAH ANGEPENDA, ANGELI WAKUSANYA KWENYE UWONGOFU, BASI
USIWE MIONGONI MWA WASIO JUA”. [06:35] – Yaani – Lau Allah Ataadhamiaye
angeli taka kuwakusanya watu wote katika dini ya haki, angeli wakusanya.
Lakini Yeye kutakata na mawi ni kwake, hakulitaka hilo ili apate
kuwalipa wale walio tenda uovu kwa jinsi ya waliyo yatenda na awalipe
mema wale walio tenda mema. Basi ewe Mtume usiwe miongoni mwa walio
jingikiwa na suna/utaratibu na kanuni za Allah kwa viumbe wake.
Bali
hakika Qur-ani Tukufu inaashiria kwamba kukhitalifiana watu kwa ajili ya
kuinusuru haki na kueneza uadilifu, hilo ni jambo linalo lazimishwa na
maslahi ya watu. Na linapelekewa na hali zao na manufaa yao. Allah
Ataadhamiaye amesema: “...NA LAU KUWA ALLAH HAWAPAMBANISHI WATU KWA WATU
BASI DUNIA INGELI HARIBIKA. LAKINI ALLAH NI MWENYE FADHILA JUU YA
WALIMWENGU WOTE”. [02:251] – Yaani – Lau si kuwa Allah anawapambanisha
wadau wa batili na wale wadau wa haki, basi bila ya shaka Dunia ingeli
fisidika na ingeli enewa na maharibiko. Hii ni kwa sababu wadau wa
batili watakapo achwa bila ya kupingwa, shari yao itatapakaa kote.
Lakini Allah Ataadhamiaye; Mwenye fadhila kuu kwa watu wote, rehema zake
zimepelekea kuwawafikisha watengenevu kupambana na mafisadi waharibifu.
Na kuwapa hoja na nguvu ambazo kwa msaada wake ushindi unakuwa ni fungu
la wadau wa haki dhidi ya wadau wa batili.
Twendapo sanjari na aya tukufu tuliyo inukuu, tunaikuta inawaamrisha
wema katika kila zama na mahala popote, kusimama imara mbele ya waovu;
wajaa shari. Na wapambane nao kwa njia yoyote ambayo dhima yake ni
kuweka ukuta baina yao na fisadi na dhuluma.
Na
miongoni mwa aya tukufu zilizo katika maana hii, ni kauli yake
Atukukiaye: “...NA LAU KUWA ALLAH HAWAKINGI WATU KWA WATU, BASI HAPANA
SHAKA ZINGELI VUNJWA NYUMBA ZA WAT’AWA, NA MASINAGOGI, NA MISIKITI,
AMBAMO NDANI YAKE JINA LA ALLAH LINATAJWA KWA WINGI. NA BILA YA SHAKA
ALLAH HUMSAIDIA YULE ANAYE MSAIDIA YEYE. HAKIKA ALLAH NI MWENYE NGUVU
MTUKUFU”. [22:40]
Yaani –
Lau kuwa si Allah Atukukiaye amewapa idhini wadau wa haki kupambana na
wadau wa batili, basi bila ya shaka wadau hao wa batili wangeli eneza
fisadi/maharibiko katika ardhi. Na wangeli vunja katika zama za Nabii
Musa na Isa-Amani iwashukie-sehemu (nyumba) za ibada za wafuasi wao. Na
wangeli vunja katika zama za Nabii Muhammad-Rehema na Amani
zimshukie-misikiti ambayo humo husimamishwa swala kwa Waislamu.
Kukhitilafiana baina ya watu katika masuala ya kidini na kidunia, kuna
sababu nyingi na vipelekeshi vya aina mbali mbali. Miongoni mwa
sababu/vipelekeshi hivyo viko vilivyo dhaahiri shahiri na ambavyo viko
batini ilo fichikana. Na viko ambavyo kipelekeshi chake ni kuijua hakika
kwa njia ya ukamilifu na kusimamisha hoja na dalili juu ya hilo. Na aina
hii ndio inayo julikana katika Istilahi za wanazuoni wa bahathi
(utafiti) kama mjadala au mdahalo.
Na
katika jumla ya sababu za Ikhtilafu baina ya watu, ni kutokuwa na uwazi
wa maono ya maudhui kwa pande zake zote. Huyu ufahamu na uelewa wake uko
katika upande maalumu na yule ufahamu wake uko katika upande mwingine
usio ule wa mwezake. Na yule wa tatu ufahamu na uelewa wake
unatofautiana na ule wa mtu wa kwanza na wa pili.
Wamekwisha sema watu wenye busara zamani: Hakika haki watu hawajapata
kuipatia ilivyo kwa njia zake zote na hawajapata kuikosea kwa njia zake
zote. Bali baadhi yake walipatia sehemu/upande wake (hiyo haki) na
wengine wakapatia upande mwingine. Wakaupigia mfano msemo wao huu, kwa
hadithi ya vipofu walio muondokea tembo mkubwa. Kila mmoja kati yao
akampapasa kwenye sehemu ya mwili wake na kumsifia kwa taswira aliyo
isawirisha. Basi akasema yule aliye upapasa mguu wa tembo huyo mkubwa:
Hakika mnyama huyu ni kama mtende mrefu. Na akasema yule aliye upapasa
mgongo wa tembo huyo mkubwa: Hakika umbile lake linafanana mno na kilima
kilicho inuka. Na mwingine..... na mwingine........ Namna hivi kila
mmoja wao amemuelezea tembo kwa wasifu ulio guswa na mkono wake. Kwa
upande huu yeye ni mkweli, lakini yeye huyo huyo kwa upande mwingine
anakosea kwa kumkadhibisha mwenzake kwa wasifu alio utoa yeye ambao
unakhalifiana na ule alio utoa yeye. Allah amrehemu Sheikh wetu Muhammad
Abu Zahrah, hakika yeye alisema baada ya kuupiga mfano huu: “Basi
angalia ni namna gani ukweli ulivyo wakusanya pamoja na angalia uwongo
na makosa namna yalivyo waingia mpaka yakawatawanya”. [Rejea
TAARIKHUL-JADAL, Sahifa 8, chapa ya DAARUL-Fikri AL-ARABIY, mwaka 1980]
Na aina
hii ya ikhtilafu pengine ndio nyepesi kuliko zote, kwa sababu hii
inatazamiwa kuondoka au kumalizika yenyewe baada ya kuijua hakika kwa
ukamilifu. Na baada ya kuyajua mas-ala kwa njia zake zote na baada ya
kufunguliwa mahala pa mzozo. Ni kwa ajili hii ndipo Wanazuoni wakasema:
Patakapo julikana mahala pa mzozo, tofauti zote hubatilika.
Kadhalika katika jumla ya sababu za Ikhtilafu baina ya watu, ni
kushikilia kumfuata mtu bila ya dalili madhubuti au hoja yenye mashiko.
Na ilhali wewe unaisoma Qur-ani Tukufu na unazikuta aya zake nyingi
zinawatangazia kifo waghafilika, majaahili na wapotea kwa kushikilia
kwao kuwafuata na kuwaiga wahenga wao au viongozi wao. Na miongoni mwa
aya zilizo pokelewa katika kulizungumzia hili, ni kauli yake Atukukiaye:
“NA WANAPO AMBIWA: FUATENI ALIYO YATEREMSHA ALLAH; WAO HUSEMA: BALI
TUTAFUATA TULIYO WAKUTA NAYO BABA ZETU. JE, HATA IKIWA BABA ZAO WALIKUWA
HAWAELEWI KITU, WALA HAWAKUONGOKA?” [02:170] – Yaani wanapo ambiwa wale
walio upendelea upotofu juu ya uwongofu: Fuateni yale Allah Ataadhamiaye
aliyo yateremsha kwa Mtume wake-Rehema na Amani zimshukie-yaani Qur-ani
inayo ongozea kwenye haki. Hupuuza kusikiliza nasaha na wakafikia kusema
kwa inadi na upumbavu: Bali tutafuata ibada ya masanamu na kuwanyenyekea
viongozi, itikadi tuliyo wakuta nayo baba zetu. Qur-ani inawarudi kwa
muundo sakhiri: “...JE, HATA IKIWA BABA ZAO WALIKUWA HAWAELEWI KITU,
WALA HAWAKUONGOKA?” – Yaani hawa majaahili wanawafuata baba zao na
kuwaiga katika ukafiri, ufasiki na uasi hata kama baba zao hao walikuwa
hawajui chochote katika masuala ya dini sahihi?! Na wala hawakuongozea
kwenye njia ya haki na iliyo sawa?!
Kisha
tena Qur-ani inapiga mfano wa watu hawa majaahili katika ubaya wa hali
yao, inasema: “NA MFANO WA WALIO KUFURU NI KAMA MFANO WA ANAYE MPIGIA
KELELE ASIYE SIKIA ILA WITO NA SAUTI, NI VIZIWI, MABUBU, VIPOFU, KWA
HIVYO HAWAELEWI”. [02:171] – Yaani na mfano wa mtu anaye waita makafiri
kuja kwenye njia ya uwongofu, ilhali wao wanampuuza na kujitenga mbali
nae. Ni kama mfano wa mchungaji anaye wapigia kelele mbuzi na kondoo
wake kuwakemea. Basi wao wanaisikia sauti yake, lakini hawayaelewi
ayasemayo. Kwa mfano huu basi, hawa waghafilika ni viziwi wa kuusikia
wito wa haki, ni mabubu wasio weza kumuitika mlinganiaji wa haki, ni
vipofu wasio ijua njia nyoofu. Kwa hali yao hiyo basi, wao hawazielewi
nasaha na maongozi yanayo elekezwa kwao.
Na
mfano wa aya hii, ni kauli yake Atukukiaye: “BALI WANASEMA: HAKIKA SISI
TULIWAKUTA BABA ZETU WANASHIKA DINI MAKHSUSI, BASI NA SISI TUNAONGOZA
NYAYO ZAO. NA KADHAALIKA HATUKUMTUMA MUONYAJI KWENYE MJI WOWOTE ILA WATU
WAKE WALIO DEKA KWA STAREHE WALISEMA: HAKIKA SISI TULIWAKUTA BABA ZETU
WANASHIKA DINI MAKHSUSI, NA SISI TUNAFUATA NYAYO ZAO” [43:22-23]
Na
mpetwa petwa wa maneno ni kwamba: Kuwafuata kiupofu na kibubusa mababa,
viongozi na wengineo, ni katika jumla ya sababu kubwa za ikhtilafu baina
ya watu. Khususan pale uigaji na ufuataji unapo kuwa ni kwa njia ya
inadi, kuikataa haki na kufuata matamanio maovu.
|