Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

KWA NINI WAISLAMU WAMEGAWANYIKA PAMOJA NA KUWA UISLAMU UNATAKA WAWE WAMOJA?

Faida

Hakuna yeyote  awezaye kuthubutu kupinga kwa kinywa kipana kuwa kuna wa kiislamu ulimwenguni  kote hii leo haukumegeka na kugawanyika vipande vipande. Kuwa leo waislamu wamegawanyika katika makundi yenye kupingana na kushutumiana wao kwa wao, hili ni suala lililo wazi mbele ya kila mmoja wetu na wala halihitaji  hoja na ushahidi wa kuthibitisha kuwa lipo. Historia italishuhudia na kuliandika suala hili, nasi waislamu wa leo tutawajibika mbele ya Mola Muumba wetu kwa kuivunja amri yake ya umoja na mshikamano baina  yetu. Kama Ulaya imefanikiwa kuzishinda tofauti zao, ikaungana na kuwa kitu kimoja na hata kufikia kuwa na sarafu moja chini ya akili na fikra za binadamu. Ni kwa nini basi leo waislamu tushindwe kuungana, kushikamana na kuwa wamoja kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume na Makhalifa wake? Kwa nini fikra na akili za kibinadamu zimeweza kuwangunaisha watu, amri ya Allah ishindwe kutuunganisha waislamu na kuwa uma mmoja chini ya bendera ya “LAA ILAAHA ILLAL-LAAHU MUHAMMADUR- RASUULULLAAH” Naam zimekuwepo juhudi za makusudi za kutaka kuuondoa uma wa kiislamu katika janga hili la utumwa wa mfarakano na utengano, janga ambalo limewatumbukiza waislamu katika shimo la unyonge na  udhahili. Juhudi hizi nzuri zimeshuhudiwa katika pande mbalimbali za ulimwengu wa Kiislamu, dhima kuu ya umoja huu ni kuyaunganisha pamoja mataifa ya Kiislamu na zile nchi zenye waislamu wengi popote pale zilipo ulimwenguni. Mafundisho ya Uislamu yaanakiri kuwa umoja, mshikamano, kupendana na kuhurumiana ndio msingi na nguzo kuu ya mafanikio ya uma wa Kiislamu, bali uma wowote ule hata kama ni uma wa kikafiri, muda wa kuwa ni wamoja na wameshikamana, kufanikiwa ni tuzo na fungu lao. Hili li bayana katika historia, rejeeni mtaona na kuukiri ukweli huu.

Uislamu unalingania umoja na mshikamano na unatahadharisha utengano na mfrakano, tuitegee siko la usikivu wa kufuata kauli hii ya Allah ndani ya Qur-ani “NA SHIKAMANENI KWA KAMBA (dini) YA ALLAH NYOTE WALA MSIACHANE…………..” (3:103)

Hii ni amri wa muongozo utokao kwa Mola Muweza, Muumba, wetu. Nani anaamrishwa, bila shaka, ni sisi waja wake, nani anaongozwa ni sisi viumbe wake. Itakuwaje kama hatukuamrika na kuufuata muongozo huu? Soma mwenyewe: (NA ATAKAYEJIEPUSHA NA MAWAIDHA YANGU, BASI KWA YAKINI ATAPATA MAISHA YENYE DHIKI, NA SIKU YA KIAMA TUTAMFUFUA HALI YA KUWA KIPOFU. ASEME” “EWE WANGU! MBONA UMEMFUFUA KIPOFU NA HALI NILIKUWA NIKIONA?” (Allah) ATASEMA: “ NDIYO VIVYO HIVYO ZILIKUJA AYA ZETU UKAZISAHAU (ukazipuuza) NA KADHALIKA LEO UTASAHAULIWA (utapuuzwa) “ (20:124-126). Hii ndio natija na mazao ya kukaidi na kupinga amri na muongozo wa Allah. Katika aya hiyo ya (103) iliyomo katika sura ya (3), Uislamu unatuamrisha waislamu tuungane, tushikamane na tuwe umma mmoja wa Kiislamu. Kigezo kikuu cha muungano kiwe ni dini ya Allah bila ya kujali rangi, lugha na mipaka  hii ya kisiasa. Ndugu zianguni waislamu, sote tunatambua na kukubali kuwa hakuna tofauti kubwa za msingi baina ya madhehebu ya kiislamu. Tofauti na ikhtilafu zilizokuwepo, zilizopo na zitakazoendelea kuwepo ni ndogo ndogo tu. Tofauti hizi zinatokana na juhudi njema za Maulamaa wema wa Kiislamu walioyatoa muhanga maisha yao yote katika kuulewa undani zaidi wa mafunzo ya dini yao. Allah awajaze kheri zote wanazozistahiki na ziada, Aamiyn. Ninasema kwa kinywa kipana kabisa kwamba tofauti zinazoishi ni ndogo ndogo tu kutokana na kujua na kuamini kuwa madhehebu yote ya kiislamu yanaunganishwa pamoja na kiungo madhubuti cha itikadi kuu za msingi. Ninaposema itikadi kuu za msingi simaanishi kingine zaidi ya zile nguzo tano za Uislamu, nguzo sita za Imani na nguzo mbili za Ihsaani. Madhehebu yote yanakiri na kuziamini nguzo zote hizi, ambazo hizi ndizo mashina na mizizi ya Uislamu. Nguzo hizi ndizo kamba au pingu inayotujumuisha pamoja kama uma mmoja kwa kuwa waislamu wote tunayaamini mashina haya ni dhahiri kuwa tofauti na ikhtilafu zetu ziko kwenye mambo madogo madogo tu ambayo tunaweza kuyamithilisha na vijitawi katika mti mkubwa au daga katika bahari ya chewa na nyangumi. Hapa ni vema tukajiuliza, iwapo sote kama waislamu tunang’ariwa na kuangaziwa na jua moja (Qur-ani) na  mwezi mmoja (Hadithi), hizi nyota zinatushughulisha? Tofauti na ikhtilafu katika matawi zilikuwepo hata wakati wake Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie, rejea historia utakubaliana nami. Hivi ndio kusema tofauti zilikuwepo, zipo leo na zitaendelea kuwepo mpaka kiyama. Tusijidanganye hatuwezi kuziondosha wala kuzizuia hata kidogi, lazima tukubaliane hivyo kwa sababu hayo ndio maumbile ya Mola wetu aliyotuumbia. (NA KAMA MOLA WAKO ANGALIPENDA, ANGALIWAFANYA WATU WOTE KUWA UMATI MMOJA (angaliwafanya wote kufuata kitu kimoja. Lakini amewapa akili na nguvu ya kutumia akili zao hizo watakavyo, ikiwa kwa wema au kwa ubaya (KWA HIVYO WATAENDELEA TU KUHITILAFIANA.ISIPOKUWA WALE AMBAO MOLA WAKO AMEWAREHEMU) NA KWA (rehema) HIYO ALLAH AMEWAUMBA (ila wenyewe tu hao wengine wamekhitari mabaya.) NA LITATIMIA NENO LA MOJA WAKO (la kuwa ) KWELI KWELI NATAIJAZA JAHANAMU KWA MAJINI NA BINADAMU WOTE (walio wabaya)  (11.118-119) la msingi na la kufuata baada ya kuukiri ukweli huu ni kuchukuliana, kuvumiliana na kuheshimu jitihada njema za kila upande. Tukiufuata kwa dhati ushauri nasaha huu, bila ya shaka mizozo, migongano na mifarakano inayoishi miongoni mwetu itakuwa imechimbiwa kaburi lisilofukulika hata na zana bora kabisa za kisasa. Nasi tutaishi chini ya anga la umoja na mshikamano wa kweli wa Kiislamu kama alivyoishi Bwana Mtume na maswahaba na makhalifa baada yake na bila ya kuwasahamu maimamu wetu wema. Basi ndugu zanguni, ninakunasihini na kuinasihi nafsi yangu kuwa ikhtilafu za madhehebu isiwe ndio chachu  ya kudharauliana, kuchukiana, kukufurishana na kutengana, Mwenyezi Mungu Mtukufu anatuasa na kutuonya: “NA MTIINI ALLAH NA MTUME WAKE, WALA MSIZOZANE (msigombane), MSIJE MKAHARIBIKIWA NA KUPOTEZA NGUVU ZENU, NA VUMILIENI (mstahamiliane). BILA SHAKA ALLAH YU PAMOJA NA WANAOVUMILIA” (8:46) Ndugu zanguni tusikubali kabisa kumpa adui mwanya na nafasi ya ushindi kwa sababu ya hii mifarakano na migongano inayotawala baina yetu leo.

Uislamu unatutaka tuhisi furaha na machungu ya waislamu wenziwetu popote pale walipo katika ardhi hii ya Allah, mashariki na magharibi. Sote tuwe mithili ya mwili mmoja kama anavyotuambia Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Mfano wa waumini katika kupendana kwao, kurehemeana kwao na kuhurumiana kwao ni kama mfano wa mwili mmoja kiungo kimoja chake (mwili) kikiumwa, mwili mzima hushirikiana nacho katika homa na kukesha” Bukhaariy na Muslim. Mshikamano huo wa mwili wakati sehemu yake inapoumwa ndio mshikamano na umoja unaotaka kujengwa na umma wa Kiislamu chini ya udugu wa Kiislamu. Qur-ani tukufu inatuambia: “KWA HAKIKA WAUMINI WOTE NI NDUGU…………  (49:10)

Katika kuifanyia kazi kauli hii ya Mola Mtukufu, tunamkuta Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alipohama Madina akiuunga udugu huu wa Kiislamu baina ya Muhajirina na Answaar. Wakawa ni ndugu wenye kupendana na kusaidiana katika shida na raha. Aya za Qur-ani na hadithi za Mtume juu ya udugu ni nyingi mno kuliko unavyoweza kufikiri: “NA AKAZIUNGA NYOYO ZAO (wakapendana wote hao maswahaba zako) HATA KAMA UNGALITOA VYOTE VILIVYOMO ARDHINI USINGALIWEZA KUZIUNGA NYOYO ZAO, LAKINI ALLAY NDIYE ALIYEWAUNGANISHA. HAKIKA YEYE NI MBORA NAMWENYE HIKIMA” (8: 63).

Kuna sababu nyingi za ndani na nje ya Uislamu zilizopelekea na zinapelekea kuvunjika kwa umoja na mshikamano baina ya  umma wa Kiislamu na kuufanya kuwa dhalili, mnyonge, usiokuwa na nguvu hata mbele ya taifa dogo dhalimu la Israel. Sehemu kubwa ya sababu hizi zinarejea katika kipindi kile cha ukoloni ambapo nchi nyingi za Kiislamu zilikuwa chini ya ukoloni wa nchi za Magharibi. Wakoloni walipotoa uhuru kwa nchi hizi na kurejea makwao waliacha matatizo mengi ya kiuchumi na kisiasa. Tumeyarithi matatizo haya ambayo yamekuwa ni sababu kuu ya kutugawa, khasa lile suala la kuwekwa kwa mipaka hii ya kisiasa tuliyonayo hivi sasa. Mipaka hii ni zao la siasa kuu ya wakoloni wale na hata wa leo, siasa ya “Divide and rule” yaani wagawe watu kwa misingi ya taifa/rangi/lugha ili watawalike kirahisi. Kwa kutumia saisa hii kama msingi, wakoloni hawa walianza kujenga matabaka baina ya watu katika makoloni yao. Wakawapandikizia fikra za kwenda na wakati, hizi zikamfanya kila aliyeshikamana na dini khasa Uislamu ajione kuwa amechelewa na yuko nyuma kimaendeleo. Natija ya fikra hizi ni kuupa kisogo Uislamu na kuuweka mbele ya macho usasa wa kwenda na wakati ambao umechangia kutufikisha hapa tulipo hii leo. Kwa upande mwingine, wakoloni hawa walihamisha utajiri wa nchi hizi kuupeleka kwao, wakavuruga uchumi na kuziacha katika hali ya ufakiri wa kutupwa unaorithiwa kizazi hadi kizazi, lengo likiwa ni kuzifanya nchi hizi kuwapigia magoti na kuwanyooshea mkono wa msaada wakoloni hawa. Msaada huu huambatana na masharti yenye madhara kwa nchi zetu hizi na manufaa kwao. Kwa kuwa tuna shida, basi tunakubaliana nao na kutufanya tusiwe na sauti wala uchaguzi mbele ya wakoloni hawa. Hatuna kinywa cha kusema hapana, bali ndiyo bwana. Hii ni miongoni mwa sababu za nje. Ama sababu  zilizomo ndani ya waislamu wenyewe ni kuyapuuza kwao mafundisho sahihi yenye kudhaminia mafanikio yao duniani na akheri. Haya si mengine bali ni mafundisho ya Qur-ani na suna ya Mtume wao.

Basi ndugu zanguni, zindukeni na itambueni mbini hii ya adui ya kutugawa ili atutawale atakavyo. Tuunganie na tuwe uma mmoja kama alivyotuagiza Allah. Tuelewe kuwa huku kuwa  makundi makundi ni sehemu ya adhabu ya Mola kwetu kwa sababu ya kuutupa kwetu muongoza wake, tusome sote na tutie akilini. (SEMA: “YEYE NDIYE MUWEZA WA KUKULETEENI ADHABU KUTOKA JUU YENU AU KUTOKA CHINI YA MIGUU YENU, AU KUKUVURUGENIVURUGENI (muwe) MAKUNDI (yasiyopatana) NA (muweza wa) KUWAONJESHA BAADHI YENU JEURI YA WENZAO” TAZAMA JINSI TUNAVYOELEZA AYA (kwa namna hii) ILI WAPATE KUFAHAMU (nao hawataki kufahamu)  (6:65).

Turudi ndugu zanguzi katika muongozo wa Allah, tushikamane, tupendane na tuwe wamoja, kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Tuzitupitie mbali tofauti ikhtilafu zetu tanzu na tukubaliane kutokukubaliana (lets’s agree to disagree). Allah anatuambia. (…….NA UKIKUFIKIENI KUTOKA KWANGU MUONGOZO, BASI ATAKAYEUFUATA MUONGOZO WANGU HUO HATAPOTEA WALA HATATAABIKA. NA ATAKAYEJIEPUSHA NA MAWAIDHA YANGU (hayo), BASI KWA YAKINI ATAPATA MAISHA YENYE DHIKI………”) (20: 123-124)


TUJIFUNZE NA TUKUBALI kuwa mshikamano wa dhati na umoja wa kweli ni ule utokanao na dini ya Allah na si vinginevyo, elewa ufahamu.

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |