|
Uhai
hautaendelea au kwa maneno mengine tunaweza kusema kwamba wanadamu
hawataendelea kuwepo katika ulimwengu huu kama hakutakuwepo kuzaliana. Huku
kuzaliana ndiko kutadhamini mfuatano wa kizazi (generation) baada ya kizazi
Wakati Mwenyezi Mungu Mtukufu alipompa mwanadamu dhima ya kuwa Khalifa
ulimwenguni hapa. Ukhalifa huu ni hadhi ya juu kabisa inayomfanya mwanadamu
kuwa ni bwana na mtawala wa ulimwengu huu kupitia muongozo wa Mola Muumba
wake. Sasa ili huyu mwanadamu aendelee kumtumikia Mola wake kupitia ukhalifa
alioumpa kama amana na dhamana, ndipo Mwenyezi Mungu akamuwekea utaratibu na
sheria ya ndoa. Jukumu la ndoa liwe ni kiwanda mama cha kuzalisha makhalifa
wa Allah katika ardhi hii. Kwa hivyo basi dhima kuu ya ndoa ikawa ni
kuhakikisha kuwa ukhalifa unaendelea kwa kuendelea kizazi kupitia ndoa. Kwa
mantiki hii tunaona kuwa lengo mama (kuu) la ndoa ni kupata watoto ili
kukiendeleza kizazi cha wanadamu. Tusome pamoja: “NA ALLAH AMEKUUMBIENI WAKE
KATIKA JINSI YENU (wanadamu wenziwenu sio malaika wala majini) NA
AKAKUJAALIENI KUTOKA KWA WAKE ZENU WATOTO NA WAJUKUU NA AKAKURUZUKUNI VITU
VIZURI VIZURI ………..” (16:72).
Ili
lengo la ndoa liweze kutimia, Mwenyezi Mungu Mtukufu akamuumbia mwanadamu
huyu nguvu, msukumo na mvuto wa kimaumbile kama kichocheo. Mwanamume na
mwanamke kila mmoja awe ni samaki na ulimbo wa kumnasa na kuvuta mwenziwe
katika ndoa na sio katika uchafu wa zinaa. Wawili hawa wapendane katika ndoa
na waendeleze ukhalifa kupitia watoto
watakaowazaa. Ni kweli usiopingika kwamba Allah Mtukufu ndiye aliyeumba jozi
mbili, dume na jike katika kila kitu tuvijuavyo na tusivyovijua, AMETUKUKA
ALLAH ALIYEUMBA DUME NA JIKE KATIKA (vitu) VYOTE, KATIKA VILE IOTESHAVYO
ARDHI, NA KATIKA NAFSI ZAO (wanadamu) NA KATIKA VILE WASIVYOVIJUA” (36:36)
Akaliumba
tone la manii katikati ya mifupa ya mgongo wa baba na kifua (mbavu) za mama.
Akaliumbia tone hili mishipa na kuliandalia mapito. Akaliumbia tumbo la uzazi
kuwa ndio mahala pake pa utulivu na hifadhi yake: “NA KWA YAKINI TULIMUUMBA
MWANADAMU KWA UDONGO ULIO SAFI. KISHA TUKAMUUMBA KWA TONE LA MANII (mbegu ya
uzazi) LILILOWEKWA KATIKA MAKAO YALIYOHIFADHIKA KISHA TUKALIFANYA TONE HILO KUWA PANDE LA DAMU, NA TUKALIFANYA
PANDE LA DAMU HILO KUWA PANDE LA NYAMA,
KISHA TUKALIFANYA PANDE LA NYAMA HILO KUWA MIFUPA, NA MIFUPA TUKAIVIKA NYAMA,
KISHA TUKAMFANYA KIUMBE KINGINE ……………(23: 13-14)
Huyu
ndio mwanadamu aandikaye leo makala haya na wewe uyasomayo na hizo ndizo
hatua za kuumbwa kwake hata leo akafikia hapo alipo. Yote haya yanashuhudia
mradi na makusudio ya Muumbaji Muweza aliyetuumba sisi viumbe wake. Mumbaji
huyu asiyeshindwa na chochote bali yeye ndiye Mshindi Mtukuka analifumbuliza
lengo la ndoa kupitia ulimi wa Mtume wake Rehema na Amani zimshukie: Oaneni
mzaane mtaongezeka (mtakuwa wengi) kwani hakika mimi nitajifakharisha kwa nyumati
kwa sababu yenu siku ya Qiyamah” Al-baihaqy. Ni kutokana na
sababu zote hizi ndio sheria ya kiislamu ikalifanya ni hatia kubwa kosa
la kuwaua watoto: “ WALA MSIWAUE WATOTO WENU KWA KUOGOPA
UMASIKINI SISI NDIO TUNAOWARUZUKU WAO NA NYINYI (pia) KWA YAKINI KUWAUA NI
KHATIA KUBWA” (17: 31)
Kosa
hili la uuaji wa watoto limekuwa ni khatia kubwa kwa sababu linapelekea
kutokuendelea kizazi cha wanadamu. Kauli jumla, ndoa ndio utaratibu Allah
aliowawekea wanadamu wazaane na kuuendeleza ukhalifa aliowapa katika
ulimwengu huu. Kwa kauli hii hatuna
hatia kusema kuwa lengo mama la ndoa ni kupata watoto, japokuwa yako malengo
tawi mengine.
MTOTO
NI NEEMA
Tumesema
na tunasema tena kwamba kuishi milele na kubakia daima katika dunia hii ni
tabia na mapenzi yaliyomo ndani ya mwanadamu. Sasa ikiwa hakuna njia wala
hila ya kumuwezesha kubakia milele ulimwenguni hapa kwa dhati yake mwenyewe
bali hata kuishi kwa miongo kadhaa na muhali wa hili anauona na kuishuhudia
kupitia wahenga wake, Ni jinsi gani watu waliomzunguka wanavyouacha ulimwengu
hali ya kuwa bado wanaupenda mmoja baada ya miwingine ili neno la Allah
litimie: “KILA NAFSI ITAONJA MAUTI……….” (3: 185)
KILA
KILICHO JUU YAKE (ardhi na mbingu) KITATOWEKA (kitaondoka) INABAKI DHATI YA
MOLA WAKO (tu mwenyewe) MWENYE UTUKUFU NA HESHIMA” (55; 26-27)
Kutokana
na neno hili la Allah lililokwishahukumiwa litimie na ambalo kiumbe mwanadamu
hana uwezo, nguvu wala hila za kuliepuka au kulizuia lisitimie kwake.
Mwanadamu huyu akaona njia pekee itakayomuwezesha kuendelea kuishi na kutajwa
hata baada ya kifo chake ni kupitia kizazi atakachokiacha nyuma yake. Kizazi
hiki kitaendelea kunasibishwa na yeye na jina lake kuendelea kuishi kwa
miongo kadhaa. Ni kwa ajili hi tunawaona/tunasoma kwamba manabii na mitume wa
Allah - Rehema na Amani ziwashukie wote. Walitamani kupata watoto wema.
Watoto wema ambao watakuwa ni alama ya kuendelea kuwepo kwao na kutajwa vema. Huyu hapa Nabii
Ibrahim - Rehema na Amani zimshukie
akiinua mikono yake juu kwa unyenyekevu mkubwa anamuomba Mola wake mtoto
mwema, anasema: EWE MOLA WANGU WEE! NIPE (mtoto awe) MIONGONI MWA WATENDA
MEMA” NDIPO TUKAMPA HABARI NJEMA YA (kuwa atapata) MTOTO MPOLE. (basi
akampata , naye ndiye Nabii Ismail)” (37: 100-101).
Na
huyu hapa ni Nabii Zakaria - Amani imshukie akimuomba Mola wake amruhusu
kizazi chema kitakachobeba jukumu la kufikisha ujumbe wa Allah baada yake,
anasema (PALE PALE ZAKARIA AKAMUOMBA MOLA WAKE AKASEMA: MOLA WANGU! NIPE
KUTOKA KWAKO MTOTO MWEMA. WEWE NDIYE USIKIAYE MAOMBI ( ya wanakuomba)” (3: 38)
“………………BASI
NIPE MRITHI (anijie) KUTOKA KWAKO, ATAKAYENIRITHI (ilimu yangu na uwongozi
yangu) NA KUWARITHI (wazee wake wengine) KIZAZI CHA YAAKUBU. NA UMFANYE, MOLA
WANGU, MWENYE KUKURIDHISHA” (19: 5-6)
Allah akaisikia dua na maombi ya mja wake huyu
mwema na kumjulisha hilo kupitia bishara ya malaika, MARA MALAIKA
WAKAMLINGANIA, HALI AMESIMAMA AKISWALI CHUMBANI, KWAMBA ALLAH ANAKUPA KHABARI
NJEMA ZA (kuwa utazaa mtoto, umuite) YAHYA, ATAKAYEKUWA MWENYE KUMSADIKISHA
(Mtume atakayezaliwa) KWA NENO LITOKALO KWA ALLAH (naye ni Nabii Issa) NA
ATAKAYEKUWA BWANA KABISA NA MTAWA NA NABII ANAYETOKANA NA WATU WEMA” (3: 39)
Hawa
hapa waja wa Allah awapandao nao wanampenda wakimnyenyekea Mola wao na
kumuomba awape burudani ya macho kutoka kwa wake na watoto wao: ‘NA WALE
WANAOSEMA MOLA WETU TUPE KATIKA WAKE ZETU NA WATOTO WETU YABURUDISHAYO MACHO
(yetu/nyoyo zetu) NA UTUJAALIE KUWA WAONGOZI KWA WAMCHAO ALLAH: (25: 74).
Allah
Mtukufu anatuonyesha dhahiri nafasi aliyonayo mtoto anapomtumia katika kiapo
chake kitukufu na kumuunganisha pamoja na mji mtukufu na Mtume wa mwisho,
ansema: “NAAPA KWA MJI HUU (wa Makkah) NAWE UTASHUKA (utateremka) KATIKA MJI
HUU (ambao wamekutoa na utahalalishiwa). (na ninaapa) KWA KILA KILICHOZAA NA
KILAKILICHOZALIWA ( 90:13)
|