Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MAZUNGUMZO BAINA YA MITUME NA KAUMU ZAO                Inaendelea ...

         Na mahala pengine tunaiona aina nyingine ya mdahalo/majadiliano yaliyo jiri baina ya Mtume Shuaib-Amani imshukie-na kaumu yake. Na majadiliano haya yamekuja kwa sura yenye ufafanuzi zaidi kuliko yale yaliyo tangulia, hebu yasikilize kupitia kauli yake Allah Ataadhamiaye: “NA KWA WATU WA MADYANA TULIWATUMIA NDUGU YAO SHUA’IB AKASEMA: ENYI WATU WANGU! MUABUDUNI ALLAH. NYINYI HAMNA MUNGU ILA YEYE, WALA MSIPUNGUZE VIPIMO NA MIZANI. MIMI NAKUONENI MMO KATIKA HALI NJEMA, NAMI NAKUKHOFIENI ADHABU YA SIKU KUBWA HIYO ITAKAYO KUZUNGUKENI. NA ENYI WATU WANGU! TIMIZENI VIPIMO NA MIZANI KWA UADILIFU WALA MSIWAKHINI WATU VITU VYAO; WALA MSIENEZE UOVU KATIKA NCHI MKAFANYA UHARIBIFU. ALIVYO KUBAKISHIENI ALLAH NDIYO BORA KWA AJILI YENU, IKIWA NYINYI NI WAUMINI. WALA MIMI SIYE MLINZI WENU”. [11:84-86]

Ndugu msomaji-Allah akurehemu-bila ya shaka unaona ya kwamba Mtume Shuaib-Amani imshukie-baada ya kuwaamrisha watu wake kumuabudu Allah Ataadhamiaye peke yake. Na baada ya kuwakataza kupunja katika vipimo na mizani, akawabainishia sababu ambazo zilizo mpelekea kuwaamrisha/kuwakataza, akasema: Hakika mimi ninakuoneni nyinyi mnamiliki mali nyingi, na aliye hivyo basi lililo la wajibu kwake ni kumpa kila mwenye haki, haki yake. Nami ninakucheleeni iwapo mtaendelea na ushirikina wenu na upunjaji wenu katika vipimo na mizani, kufikwa na adhabu ya siku yenye vishindo vikuu. Na adhabu ya siku hiyo ni yenye kumzunguka kila dhaalimu, mjaa madhambi.

Kisha Mtume Shuaib-Amani imshukie-akaendelea kuwanasihi watu wake, akawasisitizia yale aliyo kwisha kuwaamrisha katika twaa (utii kwa Allah) na yale aliyo kwisha wakataza miongoni mwa mabaya na ya hovyo. Na akawaongoza ya kwamba kile wanacho bakishiwa na Allah katika mali ya halali, hicho ndicho bora kwao kuliko mali ya haramu ijapo kuwa nyingi kiasi gani. Basi ni juu yao wao kumuitika katika hayo, iwapo wao ni katika wale waaminio haki na uadilifu. Naye aliwaambia nasaha zote alizo waambia, ili kujitoa katika dhima na kwa kuitekeleza amri ya Mola Mlezi wake ambayo ni kufikisha tu. Na hesabu ya kila aliye chupa mipaka na akafanya dhulma na akayafadhilisha mno maisha ya Dunia, iko kwa Allah Ataadhamiaye.

Na atakaye zisoma kwa makini aya hizo, ataona ya kwamba Mtume Shuaib-Amani imshukie-amewaongoza watu wake kwenye yale yanayo wafaa katika imani yao na miamala yao ya kimaisha. Na katika mahusiano/mafungamano yao wao kwa wao, na katika mienendo yao binafsi. Amewaongozea kwenye yote hayo, kwa muundo hekima, ulio kusanya kila kiletacho mafanikio na kuongozea kwenye haki. Basi je, unafikiri jawabu la watu wake lilikuwa ni nini?

Hakika jibu rejezi lao lilikuwa limesheheni kumcheza shere na kumbeza, kwa ushahidi wa kauli yake Allah Ataadhamiaye: “WAKASEMA: EWE SHUA’IB! NI SWALA ZAKO NDIZO ZINAZO KUAMRISHA TUYAACHE WALIYO KUWA WAKIYAABUDU BABA ZETU, AU TUACHE KUFANYA TUPENDAVYO KATIKA MALI ZETU? AMA HAKIKA WEWE NI MSTAHAMILIVU KWELI NA MWONGOFU!” [11:87]

Yaani: Kaumu ya Shuaib walimwambia Mtume wao kwa njia/namna ya majivuno na kucheza shere: Ewe Shuaib! Hivi ni hizo swala zako unazo dai kuwa Mola wako amekuamrisha na ambazo wewe unazikithirisha, ndizo zinazo kuamrisha tuache kuyaabudu masanamu yaliyo kuwa yakiabudiwa na baba zetu! Na ndizo hizo zinazo kuamrisha utuambie: Acheni kupunguza katika vipimo na mizani, na ilhali hiyo ndio ada tuliyo izoea na wala hatuwezi kuihepa! Iwapo swala zako hizo ndizo zinazo kuamrisha utuambie hayo, basi hizo ni swala batili na si chochote wala lolote kwetu. Lakini sisi tunaziona ni aina mojawapo ya wazimu na usema hovyo wako.

Na sentensi “AMA HAKIKA WEWE NI MSTAHAMILIVU KWELI NA MWONGOFU”, ni ziada ya ucheza shere na ujivuni wao kwa Mtume wao, kama kwamba wao wanamwambia: Unathubutuje kutuamrisha kuacha kuyaabudu masanamu na tuache kupunguza katika vipimo na mizani, pamoja na kujua kwako kwa yakini ya kwamba mambo mawili hayo ndio tumeyajenga maisha yetu juu yake. Pamoja na kudai kwako kwetu ya kwamba wewe ni mstahamilivu kweli anaye ziangalia kwa utuvu hukumu zake. Tena ni mwongofu ambaye anaye waongoza wengine kwenye yale yanayo wanufaisha?! Hakika sifa mbili hizi si lahiki na stahiki yako, maadam unatuamrisha hayo. Na hakika si vinginevyo, lililo lahiki yako ni vinyume vyake, yaani ujinga na ufasiki na uharaka katika hukumu.

Hivyo ndivyo madhaalimu wajivuni wale walivyo mrudi Mtume na Muongozi wao; Shuaib-Amani imshukie-naye ndiye khatibu wa Mitume, akiupuuzilia mbali usafihi wote huo. Kwa kuwa yeye anahisi ya kwamba watu wake ni majaahili, kama anavyo ihisi nguvu ya haki aliyo waletea kutoka kwa Mola wake Mlezi, ndipo anapo warudi kwa kauli yake: “ENYI WATU WANGU! MWAONAJE IKIWA NINAYO DALILI WAZI INAYO TOKANA NA MOLA WANGU MLEZI, NA IKAWA YEYE AMENIRUZUKU RIZIKI NJEMA KUTOKA KWAKE? WALA MIMI SIPENDI KUKUKHALIFUNI NIKAFANYA YALE NINAYO KUKATAZENI. SITAKI ILA KUTENGENEZA KIASI NINAVYO WEZA. NA SIPATI KUWEZESHWA HAYA ILA NA ALLAH. KWAKE YEYE NINATEGEMEA, NA KWAKE YEYE NAELEKEA. NA ENYI WATU WANGU! KUKHALIFIANA NAMI KUSIKUPELEKEENI HATA MKASIBIWA KAMA WALIVYO SIBIWA WATU WA NUHU, AU WATU WA HUD, AU WATU WA SALEH. NA WATU WA LUT’ SI MBALI NANYI. NA OMBENI MSAMAHA KWA MOLA WENU MLEZI, TENA TUBUNI KWAKE. HAKIKA MOLA WANGU MLEZI NI MWENYE KUREHEMU NA MWENYE UPENDO”. [11:88-90]

Yaani: Mtume Shuaib-Amani imshukie-aliwaambia watu wake: Enyi watu wangu! Hebu niambieni, lau mimi nitakuwa na hoja/dalili ya wazi, uoni/ujuzi uangazao nilio tunukiwa na Mola wangu Mlezi, aliye Mmiliki wa yangu yote. Na akaniruzuku riziki njema kutokana na fadhila zake, baada ya fadhila zote hizo, hivi mnaona mimi ninafaa kufuata matamanio/matashi yenu?! Hapana, na katu sitayafuata matashi yenu hayo, bali nitaendelea na njia yangu hii mpaka niufikishe ujumbe wa Mola wangu Mlezi. Kisha anawafichulia mwenendo wake pamoja nao, anawaambia: Na si sehemu ya hulka yangu mimi kukukatazeni nyinyi kutenda jambo fulani, kisha mimi nikalitenda hilo hilo. Na hakika si vinginevyo, mimi ninalo litaka katika haya ninayo kuamrisheni na yale ninayo kukatazeni, ila ni kwa msaada na auni yake Allah. Kwani ni Yeye peke yake ndiye ninaye mtegemea katika mambo yangu yote.

Halafu Mtume Shuaib-Amani imshukie-anaendelea kuinasihi kaumu yake, anawagurishia kwenye kuwakumbusha maanguko ya walio tangulia. Akiwatahadharisha usije ukawa mwisho wao kama ule mwisho wa madhaalimu wa kabla yao, anawaambia: Enyi watu wangu! Uadui wenu kwangu usikupelekeeni kunizulia uwongo na kuendelea kuniasi na kunipiga vita. Kwani hilo litakupelekeeni kusibiwa na adhabu kama ile iliyo ipata kaumu ya Nuhu, au kaumu ya Hud au kaumu ya Saleh. Na ikiwa nyinyi hamuwaidhiki na hayo yaliyo zisibu kaumu zilizo tangulia, basi hebu waidhikini na kaumu Lut ambao walishukiwa na adhabu, wao na mji wao. Ardhi yao ikapinduliwa juu chini, chini juu, na wala wao hawako mbali nanyi, si kizama wala kikanda.

Kisha baada ya nasaha na majadiliano yote hayo, ndipo akawafungulia mlango wa matumaini ya kupata rehema za Allah Ataadhamiaye, iwapo tu wao watatubu na kurejea kwa Mola wao, akasema: Na mtakeni maghufira Mola wenu Mlezi kutokana na madhambi yote mliyo yatenda na kisha tubieni kwake toba ya kweli. Allah-utakati wa mawi ni wake-atakutakabalieni toba yenu, kwani Yeye ni Mrehemevu mno kwa waja wake na ni Mwingi mno wa mapenzi kwa yule anaye mtii.

Kama hivi tunamuona Mtume Shuaib-Amani imshukie-akiipa kaumu yake aina kwa aina za nasaha na mawaidha bali mbali na akiwazungusha katika uringo wa uraghibishi na ukhofishi. Na akijadiliana na kuhojiana nao kwa miundo mbali mbali. Lakini wapi, kaumu yake ilikuwa imesha fikia kileleni mwa ufisadi, wakamrudi kwa kauli yao, kama walivyo nukuliwa na Qur-ani Tukufu: “WAKASEMA: EWE SHUA’IBU! MENGI KATIKA HAYO UNAYO YASEMA HATUYAFAHAMU. NA SISI TUNAKUONA HUNA NGUVU KWETU. LAU KUWA SI JAMAA ZAKO TUNGE KUPIGA MAWE, WALA WEWE SI MTUKUFU KWETU”. [11:91]

Yaani: Watu wa Shuaib walisema katika kumrudi Mtume wao: Ewe Shuaib! Hakika sisi hatuyajui mengi katika hayo unayo yasema, kwani hayo ni maneno ambayo hatujayazoea na kamwe hayatakubaliwa na nafsi zetu. Na umesha fanya nasi midahalo mingi mpaka tunakuchukia na wala hatutaki kukuona, nasi tunakuona wewe ni mtu dhaifu tu kwetu, usiye na ubavu wa kupambana nasi iwapo tutataka kukufukuza katika mji wetu. Na lau kuwa si jamaa/ndugu zako ambao wao wako pamoja nasi katika dini yetu, tungeli kupopoa kwa mawe ukafilia mbali. Na wewe kwetu si mtu mtukufu na hupendwi, bali kwetu sisi wewe ni mtu dhaifu, mkataliwa achukiwaye.

Hapo sasa ndipo tunamkuta Mtume Shuaib-Amani imshukie-akigura kutoka katika muundo wa mazungumzo laini na watu wake, na kuingia kwenye muundo wa ukali na ukanyi wa upole. Ili kuulinda/kuutetea utukufu wa Mola wake Mlezi, anawaambia: “ENYI WATU WANGU! KWANI JAMAA ZANGU NI WATUKUFU ZAIDI KWENU KULIKO ALLAH? NA YEYE MMEMUEKA NYUMA YA MIGONGO YENU! HAKIKA MOLA WANGU MLEZI NI MWENYE KUYAZUNGUKA YOTE MNAYO YATENDA. NA ENYI WATU WANGU! FANYENI MWEZAYO, NA MIMI PIA NINAFANYA. KARIBUNI MTAJUA NI NANI ITAKAYE MFIKA ADHABU YA KUMHIZI, NA NANI ALIYE MWONGO. NA NGOJENI, NAMI PIA NINANGOJA PAMOJA NANYI”. [11:92-93]

Yaani: Mtume Shuaib-Amani imshukie-aliwaambia watu wake kwa ghadhabu kwa ajili ya kuilinda dini na itikadi yake dhidi ya kudharauliwa: Hivi ni kwa sababu tu ya ndugu na jamaa zangu ndio hamkunipopoa mawe, hao ndio bora na watukufu kwenu kuliko Allah ambaye Yeye ndiye Muumba wenu, Mpa riziki wenu, Mfishaji na Mpa uhai wenu. Na ambaye mmeyafanya maarimsho na makatazo yake niliyo kuleteeni kutoka kwake, kuwa ni kitu kitupwacho kisicho na punje ya thamani! Hakika Mola wangu Mlezi ameyazunguka kwa kuyajua fika maneno yenu hayo na kauli zenu hizo na atakulipeni adhabu fedheheshi iliyo stahiki yenu. Na enyi watu wangu nyie! Tendeni lolote mnalo weza kunitendea na nitisheni na nikamieni mtakavyo, yote hayo hayatanidhuru hata ukucha. Yatawezaje kunidhuru na ilhali mimi ninamtegemea Allah Mtegemewa wa msaada na uangalizi/ulinzi wake?! Nami sitayakabili matendo yenu hayo maovu kwa uovu, bali nitayarudi kwa matendo mema nako ni kule kukuiteni kwenye upweke wa Allah Ataadhamiaye na kwenye tabia njema. Na punde tu mtajua ni nani baina yetu nanyi atakaye fikwa na adhabu itakayo mfedhehesha na kumdunisha. Na ni nani miongoni mwetu aliye muongo katika kauli na matendo yake. Na ngojeeni mwisho mbaya kwa kunikadhibisha, nami ninangojea pamoja nanyi. Mtume Shuaib-Amani imshukie-hakungojea muda mrefu, kwani iliwafikia kaumu yake walio madhaalimu, adhabu iliyo wadamirisha (walihikisha) kabisa.

  

 | Tuandikie |