Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MAKALA MAALUM-WAADHI WA EID

 

KALIMA YA EIDIL-FITRI (WAADHI WA EID).

Ndugu waislamu,

Assalaamu Alaykum!

Himda njema zote zinamstahikia Allah na rehema na amani zimuendee Nabii Muhammad, maswahaba na aali zake wote na kila awafuataye kwa wema mpaka siku ya Kiyama.

Ama baad,

Ndugu zanguni waislamu! Sote tunakubaliana kwamba siku ya Eid ni siku ya furaha, na ni siku ambayo mmehalalishiwa kula na kunywa mchana. Ni siku inayoashiria kumalizika kwa ibada tukufu na kongwe ya swaumu ya Ramadhani. Ni siku ya watu kuvaa vizuri, kutembeleana, kusaidiana na kuwalisha watu chakula. Hebu itegee sikio pamoja nami kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Inapokuwa siku ya Eidil-Fitri, malaika hukaa mwanzoni mwa njia wakalingana: Damkeni enyi waislamu, enendeni kwa Mola Mkarimu aneemeshaye kisha kulipa thawabu juu ya neema hizo. Mmeamrishwa kusimama usiku kuswali (taraweh) mkasimama na mliamrishwa kufunga mchana mkafunga. Na mkamtii Mola wenu, pokeeni zawadi zenu. Eeh hakika Mola wenu amekwisha kusameheni, basi rejeeni majumbani mwenu hali ya kuwa mmeongoka. Nayo ni siku ya zawadi na siku hii huitwa mbinguni (siku ya zawadi)”.

Twabaraaniy

Siku ya Eid ni siku ya mahafali. Waislamu wamehitimu mafunzo yao ya mwezi mmoja katika Chuo Kikuu Cha Ucha-Mungu (swaumu). Leo ndio siku ya kutunukiwa na kukabidhiwa wahitimu vyeti vyao. Na leo ndio kila mtu atajua matokeo ya mafunzo yake kama amefaulu au amefeli. Hili litajulikana kutokana na namna atakavyoisherehekea siku yake hii ya leo.

Ndugu zanguni wapenzi! Katika kumalizika mwezi mtukufu wa Ramadhani tunapata fundisho moja kubwa sana. Nalo ni kwamba kama vile tulivyoushuhudia mwanzo wa mwezi wa Ramadhani na leo hii tunashuhudia kumalizika kwake. Tujiulize na tutafakari hili linaashiria nini katika maisha yetu ya kila siku? Ikiwa hili linatoa ishara ya kitu/jambo, basi jambo hilo litakuwa si jingine. Bali ni kwamba tujue kwa yakini kuwa kila chenye mwanzo hakina budi kuwa na mwisho. Isipokuwa Allah pekee yeye ndiye asiye na mwanzo wala mwisho. Tuukiri na kuukubali ukweli huu usiopingika, tujue na tufahamu kuwa kama ambavyo kila mmoja wetu alikuwa na siku ya kuja kwake katika ulimwengu huu. Kadhalika anayo siku inayomngojea ya kuondoka kutoka katika ulimwengu huu umalizikao kuyaendea ima maisha ya milele peponi au motoni. Tusome na tuzingatie: “KILA KILICHO JUU YAKE (ardhi na mbingu) KITATOWEKA (kitaondoka). INABAKI DHATI YA MOLA WAKO (tu mwenyewe) MWENYE UTUKUFU NA HISHIMA”.

[55:26-27]

Ndugu zanguni, tujiandae vema na mapema na siku hii ngumu na nzito ambayo haikwepeki, hatuna budi tutakutana nayo tu. Siku hii ndio mwanzo wa safari ya kuhudhurishwa mbele ya mahakama yenye kila aina ya uadilifu, haki na usawa. Kwa ajili ya kuhesabiwa na kulipwa kwa mujibu wa amali zetu tulizozitenda hapa duniani bila ya kudhulumiwa mtu. Kitakachofuatia baada ya hapo ni: “...KUNDI MOJA LITAKUWA PEPONI NA KUNDI JINGINE MOTONI”. [42:7]

Kuwa katika kundi la peponi/motoni, huo ni uchaguzi wako mwenyewe na hili litategemea jinsi utakavyo zichanga karata za maisha yako katika ulimwengu huu wa mpito. Utavuna pepo/moto kwa akili, nguvu na mali yako mwenyewe. Tuiogopeni ndugu zanguni siku hii: “NA IOGOPENI SIKU AMBAYO MTARUDISHWA KWA ALLAH, KISHA VIUMBE WOTE WATALIPWA KWA UKAMILIFU YOTE WALIYOYACHUMA; NAO HAWATADHULUMIWA”. [2:281]

Naam, mwezi wa Ramadhani umemalizika na bila ya shaka utatushuhudia mbele ya Allah kwa yote mema/mabaya tuliyoyatenda ndani yake. Katika mwezi huu mtukufu sote tumeshuhudia jinsi misikiti ilivyokuwa ikijaa waumini katika swala zote za fardhi, hata ile swala nzito na ngumu ya alfajiri. Misikiti ilikuwa ikiamirishwa kwa kusomwa sana Qur-ani Tukufu na kudhukuriwa sana Allah. Takriban wakati wote usiku na mchana utawakuta waumini misikitini wakifanya namna kwa namna za ibada. Na utaviona vikundi vya ilimu, waumini wanasomeshana, kukumbushana na kupeana nasaha kuhusiana na dini yao. Yote haya tumeyaona na kuyashuhudia ndani ya mwezi wa Ramadhani, lakini kwa masikitiko makubwa leo mwezi umemalizika na mambo yake yote mema na mazuri yanamalizika pamoja nao. Hutayaona tena hadi Ramadhani ya mwakani panapo uhai na majaliwa. Ni kweli kuwa Ramadhani imekwisha, lakini yule tuliyekuwa tunafunga na kuswali kwa ajili yake yu hai milele, hamaliziki na wala haishi kama ilivyokwisha Ramadhani. Kwa hivyo ni wajibu wetu kuendelea kuuelekeza utii wetu kwake hata nje ya Ramadhani kama tulivyokuwa tukifanya ndani ya Ramadhani. Eh! Hasara, msiba na majuto yaliyoje kwa waja hawa, kama kwamba walikuwa wanauabudu mwezi wa Ramadhani na sio Mola wa mwezi wa Ramadhani! Mwezi ukiisha, hakuna tena kuswali, kufunga, kusoma Qur-ani, wala..., wala....Hii ni dalili na ishara ya wazi ya kutokukubaliwa kwa swaumu na amali zao nyingine walizozitenda ndani ya mwezi wa Ramadhani. Kwani amali ya mja ikikubaliwa na kupokelewa, Mola humzidishia mja huyo taufiki na kutengenea. Hapo ndipo utamuona kila siku anazidi na kuendelea kumtii Mola wake.

Ndugu zanguni waislamu, ni muhali kabisa kwa mtu aliyefunga kwa Ikhlaaswi, halafu akawa leo baada ya swala ya Eid ndio anaagana na msikiti. Haswali tena hadi Ramadhani ya mwakani ambayo hana dhamana nayo. Ikiwa itakuwa hivi ni wazi kuwa swaumu ya mja huyu haikumfikisha kwenye lengo lake ambalo ni kumuandaa na kumfinyanga mja kuwa mcha-Mungu. Tusome na tuzingatie: “ENYI MLIOAMINI! MMELAZIMISHWA KUFUNGA (swaumu) KAMA WALIVYO LAZIMISHWA WALIOKUWA KABLA YENU ILI MPATE KUMCHA ALLAH”. [2:183]

Ni ukweli usiopingika kwamba mtu hawezi kuwa mcha-Mungu bila ya kushikamana na swala tano. Ndugu zanguni, Allah aliwaamrisha malaika pamoja na Ibilisi ambaye alikuwemo kundini kumsujudia Nabii Adam-Amani ya Allah imshukie. Wamsujudie hali ya kumuamkia na wala sio kwa njia ya kumuabudu. Iblisi kwa ushupavu na upasito aliokuwa nao alikataa kuitekeleza amri hii ya Mola wake. Ni kwa sababu hii ya kuikhalifu na kukataa kuitii amri hii, Allah akamfukuza na kumtoa Iblisi huko alikokuwa kwenye neema za daima. Na akamtenga mbali na rehema zake (akamlaani) na isitoshe kesho akhera ataingia motoni ikiwa ni jazaa ya inadi na kibri chake. Basi wewe ndugu yangu mpenzi usiotaka kuswali, hivi hujioni kuwa wewe ni mbaya zaidi kuliko Iblisi? Pengine utajiuliza kwa nini au utaona kuwa unatukanwa kwa kufananishwa na kiumbe mbaya huyu aliyelaaniwa! Lakini huo ndio ukweli na utaendelea kuwa ndio ukweli maadam wewe ni tariku-swala (mwenye kuacha swala). Hakuna cha kuubadilisha ukweli huu ila ni wewe kuwa miongoni mwa wenye kuswali kama alivyoamrisha Allah Mola Muumba wako. Naam, hii ni kwa sababu Iblisi alikataa kumsujudia baba yetu Nabii Adam sijida ya maamkizi kwa amri ya Allah. Wewe usioswali leo, unakataa kumsujudia sijida ya ibada yule aliyemuumba Nabii Adam. Iblisi alikataa kusujudu mara moja tu katika umri wake wote, wewe usioswali unakataa kusujudu mara thelathini na nne (34) kila siku. Naam ,mara 34 kwa siku, kwani jumla ya rakaa za swala tano za fardhi ulizofaradhishiwa na Allah kuziswali kila siku ni rakaa kumi na saba. Mbili alfajiri, adhuhuri nne, laasiri nne, maghribi tatu na Ishaa nne, jumla ni rakaa kumi na saba. Na kila rakaa moja ina jumla ya sijida mbili, ukizidisha kumi na saba kwa mbili utapata jumla ya sijida thelathini na nne (34), hizo ndizo sijida unazopaswa kumsujudia Mola wako kila siku. Hebu iangalie tena adhabu aliyopewa Iblisi kwa kuacha sijida moja tu, hii inamaanisha kuwa mwenye kuacha sijida 34 kila siku anastahiki kupata adhabu kali zaidi kuliko aliyopewa Iblisi. Sikwambii tena asoswali wiki, mwezi, mwaka, muongo (decade) au umri mzima anastahiki adhabu gani. Eeh! Ndugu yangu, kiumbe dhaifu wee! Ionee huruma nafsi yako, acha ukaidi utakaokuletea majuto, huiwezi tena huiwezi hata chembe adhabu ya Mola wako. Badili mwenendo wako sasa kabla hujachelewa, tusome na tuzingatie: “...NA BILA SHAKA ADHABU YA AKHERA NI KALI ZAIDI NA IENDELEAYO SANA”. [20:127]

Pia kuna khatari kubwa ya kuwa kafiri mtu asoswali, hebu itegee sikio kauli hii ya Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “YE YOTE atakayeacha swala kwa makusudi, bila shaka atakuwa AMEKUFURU”.

Ndugu zanguni waislamu, inasikitisha sana jinsi waislamu tunavyoisherehekea sikukuu yetu hii. Siku ya Eid ndiyo siku ambayo waislamu wenyewe wanautukanisha uislamu wao na kuudhihirishia ulimwengu kwamba akthari ya wafanyao maasi ni waislamu. Mtu alikuwa hawezi kukesha msikitini kufanya ibada, siku ya leo atakesha katika ulevi, atakunywa hadi atajimwagia. Huyu eti anasherehekea kumalizika kwa mfungo mtukufu wa Ramadhani. Sub-haanalla! Na huyu si mwingine bali ni yule yule muislamu tuliyekuwa naye msikitini katika kipindi chote cha Ramadhani akiswali na kufunga pamoja na sisi. Huyu haisherehekei Eid bali ukweli na uhalisia wa mambo ni kwamba anausherehekea moto wa Jahanamu unaomngojea iwapo hataidiriki toba kabla ya kufikwa na mauti. Na huyu ndiye mtu aliyefeli vibaya kabisa katika mafunzo ya Chuo Kikuu Cha Ucha-Mungu (swaumu). Siku ya Eid ndio siku ambayo utawaona dada zetu wamevaa mavazi ya ajabu ajabu na kuwa kama mbuzi wasio na mchunga, wanauuza utu wao na kununua maradhi sambamba na moto wa milele. Ili muradi siku ya Eid, watu watashindana katika kumuasi Mola wao na kumfurahisha shetani. Wote hawa tunawaasa na kauli hii tukufu ya Allah: “AMA YULE ALIYEASI. NA AKAPENDA ZAIDI (akayafadhilisha maisha) YA DUNIA. BASI KWA HAKIKA JAHANAMU NDIYO ITAKAYOKUWA MAKAZI YAKE. NA AMA YULE ALIYEOGOPA KUSIMAMISHWA MBELE YA MOLA WAKE, AKAIKATAZA NAFSI YAKE NA MATAMANIO (maovu). BASI (huyo) PEPO NDIO ITAKAYOKUWA MAKAZI YAKE”. [79:37-41]

Ndugu zanguni waislamu, funga ya Ramadhani imemalizika, LAKINI hii haimaanishi kuwa muislamu hana tena fursa ya kufunga hadi Ramadhani ya mwakani. La hasha, bali anayo fursa adhimu ya kujikurubisha na kujipendekeza zaidi kwa Mola wake kwa kufunga swaumu mbali mbali za suna. Miongoni mwa swaumu hizo za suna ni kufunga siku sita za mfunguo mosi (Shawwal). Imepokelewa hadithi na Abuu Ayuub-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume-Rehema na Amani zimshuie-amesema: “Atakayeufunga mwezi wa Ramadhani, halafu akaufuatishia na siku sita za mfunguo mosi. Itakuwa ni kama kufunga mwaka mzima”.

Muslim

Ndugu zanguni hayo ndio malipo na ujira adhimu na mnono wa funga ya Ramadhani iambatanishwayo na funga ya siku sita za mfunguo mosi. Tumeweza kufunga mwezi mzima, hivi ni kweli tutashindwa kufunga siku sita! Ikiwa tuna nia ya kujipendekeza na kujikurubisha kwa Mola wetu kwa maslahi na manufaa yetu wenyewe hatutashindwa. Haya na tujihimize ndugu zanguni, kwani: “ANAYEFANYA WEMA ANAJIFANYIA (mwenyewe) NAFSI YAKE, NA MWENYE KUTENDA UBAYA NI JUU (nafsi) YAKE (vile vile); NA MOLA WAKO SI DHALIMU (hata kidogo) KWA WAJA (wake)”. [41:46]

“...NA KHERI YO YOTE MNAYOITANGULIZA KWA AJILI YA NAFSI ZENU MTAIKUTA KWA ALLAH IMEKUWA BORA ZAIDI NA INA THAWABU KUBWA SANA...” [73:20]

Mwisho, Website yenu WEBSITE UISLAMU inakutakieni waislamu wote po pote mlipo ulimwenguni kote kheri, baraka, amani, furaha na radhi ya Allah katika sikukuu hii ya Eidil-Fitri. Tunawapongezeni nyote kwa kusema: TAQABBALAL-LAAHU MINNAA WA MINKUM WA AHYAAKUM. KULLU AAMUN WA ANTUM BIKHAYRI!

Wasalaamu Alaykum Warahmatullaah Wabarakaatuh!

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |