|
9.
Kushikamana na
kitendo cha Sayyidna Umar, ndio kushikamana na Sunna ya Mtume-Rehema na
Amani zimshukie:
Tunaharakia kusema na tunawaambia maimamu wa
Ijitihadi katika zama hizi: Hakika aliyo yafanya Umar au aliyo yaamrisha
Umar, si uzuzi (bidaa) katika dini. Bali hilo ni kushikamana na muongozo
wa Mtume na ni kuifuata Sunna ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-kwa sababu zifuatazo:
(a)
Kwamba Sayyidna Umar Bin
Al-Khatwaab, alipewa na Mtume jina la “Al-Faarouq”, kwa sababu Allah
aliifarikisha (aliitenganisha) haki na batili kupitia kwake. Na
alitenganisha kwaye uwongofu na upotofu, basi yeye ni Al-Faarouq
Umar-Allah amuwiye radhi.
(b)
Yeye ni mletewa ilhamu (ufahamu)
ambaye hasemi ila ambalo ndani yake imo haki na ilivyo ndivyo, na kheri
(wema) na uongozi, kwa sababu ya nuru ya uoni (utambuzi) wake. Na Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema juu yake: “Hakika Allah
Atukukiaye, ameiweka haki kwenye ulimi na moyo wa Umar”. Tirmidhiy &
JAAMIUL-USWUUL 08/608. Na amesema: “Hakika walikuwemo miongoni mwa wa
kabla yenu wapewa ilhaamu, basi kama yuko yeyote katika umati wangu,
basi bila ya shaka huyo ni Umar”. Bukhaariy [07/40]-Allah amrehemu.
(c)
Qur-ani imeshuka mahala pengi
ikiwafikiana na rai/maoni ya Umar. Imamu Bukhaariy-Allah
amrehemu-amepokea kutoka kwa Umar Bin Al-Khatwaab-Allah amuwiye
radhi-kwamba yeye amesema: “Nimewafikiana na Mola wangu katika sehemu
tatu: katika Maqaamu Ibraahim, katika suala la Hijaabu na katika kadhia
ya mateka wa Badri. Mimi nilisema: Ewe Mtume wa Allah! Unaonaje lau
tungepafanya Maqaamu Ibraahim kuwa ni mahala pa kuswalia? Ikashuka aya
“...NA ALIPO KUWA AKISIMAMA IBRAHIM PAFANYENI PAWE PA KUSWALIA...”
[02:125] Na nilisema: Ewe Mtume wa Allah! Hakika wanaingia kwa wake
zako, wema na waovu, basi unaonaje lau utawaamrisha wavae Hijaabu? Hapo
ikashuka aya ya Hijaabu “... NA MNAPO WAULIZA WAKEZE HAJA WAULIZENI
NYUMA YA MAPAZIA...” [33:53] Na wake za Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-walikusanyika juu yake katika wivu, nikasema: “Asaa Mola wake
Mlezi, akikupeni talaka, akampa wengine badala yenu nyinyi, walio bora
kuliko nyinyi”. Ikashuka aya kama hivyo”. Bukhaariy-Allah amrehemu.
Basi ikiwa Qur-ani inashuka ikimuwafiki/ikikubaliana na
rai ya Umar, ni vipi basi maswahaba wasiitwae kauli yake na
wakakongamana juu yake?!
Na Imamu Tirmdhiy-Allah amrehemu-amepokea kutoka kwa
Abdullah Bin Umar-Allah awawiye radhi-kwamba yeye amesema:
“Halikupata katu kuwashukia watu jambo, wakalizungumza na akalizungumza
Ibn Al-Khatwaab, ila ilishuka Qur-ani katika jambo hilo kwa namna alivyo
sema Umar”. Tirmdhiy & JAAMIUL-USWUUL 08/608.
(d)
Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-aliwaamrisha Waislamu kushikamana na muongozo wa makhalifa
waongofu na Sunna ya Abubakar na Umar. Akasema: “Na hakika atakaye
kuwa na maisha marefu miongoni mwenu, basi ataona ikhtilafu nyingi. Basi
(wakati huo), nyinyi shikamaneni na Sunna (mwendo) wangu na Sunna ya
makhalifa waongofu, viongozi wenye kuongoza. Ziumeni kwa magego”.
Abu Daawoud & Tirmidhiy-Allah awarehemu.
Na amesema Mtume-Rehema na Amani zimshukie:
“Wafuateni wale baada yangu, Abubakar na Umar”.
Na amesema Abdullah Bin Masoud-Allah amuwiye radhi:
“Yeyote mwenye kuwa mshika Sunna, basi na ashikamane (afuate) na Sunna
ya walio kwisha kufa, kwa sababu aliye hai haiaminiwi juu yake fitina.
Hao (walio kufa) ni maswahaba wa Muhammad-Rehema na Amani
zimshukie-walikuwa ni wabora wa umma huu. Wema wao kwa nyoyo, wenda kina
wao kwa elimu na wachache wao kwa taklifu. Allah aliwachagua kusuhubiana
na Mtume wake na kuisimamisha dini yake. Basi ukirini ubora wao na
zifuateni nyoyo zao na shikamaneni na mnacho kiweza katika tabia na
mwendo wao. Kwani wao walikuwa juu ya uwongofu nyoofu”. Ibn
Abdul-Barri [JAAMIU BAYAANIL-ILMI WAFADHWLIHI 02/97].
Mimi
ninasema: Basi je, ni nani anaye stahiki zaidi kufuatwa uwongofu
(muongozo) wake kuliko Abubakar na Umar?! Na ni vipi kuwe kumfuata Umar
katika lile alilo washariia Waislamu ni “Bidaa potofu”, kama wanavyo
sema baadhi ya watu majahili miongoni mwa wanao dai kuwa na elimu?!
Amesema
Ibn Al-Athiyr-Allah awarehemu-katika kuizungumzia hadithi iliyo pokewa
kutoka kwa Bukhaariy-Allah amrehemu-kutoka kwa Umar katika kauli yake:
“Bora ya bidaa, ni hii”. Amesema maneno ambayo nassi (nukuu) yake
ni: “Neno bidaa linatokana na neno Ibtidaa – (kuanzisha
upya/kuzua/kuleta kisicho kuwepo kabla). Na hiyo Ibtidaa (kuzua) ikiwa
kinyume na aliyo amrisha Allah na Mtume wake, basi huko kuko katika wigo
wa kulaumiwa na kukanushwa. Na kukiwa kunatuka (kunaingia) chini ya
uenevu wa aliyo yapendezesha Allah na akayahimiza au Mtume wake, basi
hicho kiko kwenye wigo wa kusifiwa. Kama aina ya wema na ukarimu na
kutenda mema. Basi hii (Ibtidaa) ni katika amali (matendo) zenye
kusifiwa na inatiwa nguvu na hadithi “Atakaye anzisha Sunna (mwendo)
njema, atapata ujira wake (hiyo Sunna) na ujira wa atakaye itendea
kazi”. Na hilo linaungwa mkono na kauli ya Sayyidna Umar Bin
Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi-katika swala ya Tarawehe: “Bora ya
bidaa, ni hii”. Kwa kuwa lilikuwa katika matendo ya kheri na
linaingia katika wigo wa kusifiwa, akaliita bidaa na akalisifia. Na hiyo
(swala) ajapo kuwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliiswali,
ila yeye aliiacha, hakuidumisha na wala hakuwakusanya watu juu yake.
Basi kule kuidumisha kwake Umar (swala hiyo) na kuwakusanya watu juu
yake na kuwapendezeshea, ni bidaa. Lakini hiyo ni bidaa njema, yenye
kusifiwa”. [JAAMIUL-USWUUL 01/281]
Na
hakika si vinginevyo, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliikata
swala ya Tarawehe, kwa ajili ya kuuonea huruma umati wake. Na Sayyidna
Umar-Allah amuwiye radhi-akawa miongoni mwa walio wazindua watu juu yake
(Sunna hii) na akaisunisha kwa udaima (miaka yote). Basi kwa ajili hii,
yuna yeye ujira wake na ujira wa wenye kuitendea amali mpaka siku ya
Kiyama. [JAAMIUL-USWUUL 06/123]
Na
amesema Ibn Hajar Al-Asqalaaniy katika FAT-HUL-BAARIY: Na asili ya
bidaa, ni lile lililo zushwa bila ya kuwa na mfano tangulizi, na
hutumika (neno hili) katika sheria kwenye mkabala wa Sunna, na hapo huwa
ni lenye kutaiwa (kulaumiwa na kusemwa vibaya). Na uthibitifu ni kwamba
hiyo (bidaa) ikiwa ni miongoni mwa yanayo bimbirikia chini ya lenye
kuonwa zuri katika Sharia, basi nalo hilo huwa zuri, kama alivyo sema
Umar: “Bora ya bidaa, ni hii”. Na ikiwa ni miongoni mwa yanayo
bimbirikia chini ya yenye kuonwa vibaya katika Sharia, basi hilo nalo
huwa baya. Na kama si hivyo, basi hilo ni katika fungu la Mubaaha”.
[FAT-HUL-BAARIY, SHEREHE YA BUKHAARIY, 04/253]
Kisha
akaendelea kusema-Allah amrehemu: Na kisimamo cha Ramadhani ni Sunna,
kwa sababu Umar hakika si vinginevyo, alikichukua kutoka kwenye kitendo
cha Mtume-Rehema na Amani zimshukie. Na hakika si vinginevyo, Mtume
alikiacha kwa kuchelea kisije kufaradhishwa na Mtume alipo kufa, hofu
hiyo ikawa imeondoka. Kukawa na nguvu mbele za Umar kuwakusanya watu
nyuma ya Imamu mmoja, kwa sababu ya utengano wa neno unao patikana ndani
ya kukhitilafiana. Na kwa sababu ya kukusanyika nyuma ya Imamu mmoja
kunawatia uchangamfu waswaliji wengi... Na wala haikutuka katika riwaya
hii (ya Bukhaariy) idadi ya rakaa ambazo alikuwa Ubayyi Bin Ka’ab
akiwaswalisha. Na pamekindanwa katika hilo, pakasemwa: Hakika hizo ni
rakaa kumi na moja, na walikuwa wakisoma aya mia mbili na wakitegemea
vifimbo kutokana na urefu wa kisomo. Na pamesemwa: Ni rakaa kumi na
tatu. Na Imamu Maalik-Allah amrehemu-amepokea kwa njia ya Yazid Bin
Khuswaifah: Kwamba hizo ni rakaa ishirini, na (idadi) hii inachukuliwa
bila ya (kuchanganya na) Witri.
Na
imepokewa kutoka kwa Yazid Bin Roumaan: “Watu walikuwa wakisimama katika
zama za Umar kwa rakaa ishirini na tatu”.
Na
amesema Atwaau: “Niliwadiriki katika Ramadhani wakiswali rakaa ishirini
(Tarawehe) na rakaa tatu za Witri”.
Na
mjumuisho baina ya riwaya hizi unamkinika kwa khitilafu za hali. Na
inawezekana kwamba khitilafu hiyo ni kwa sababu ya urefushaji wa kisomo
na ufupishaji wake. Kwa hivyo basi, pale kinapo refushwa kisomo, idadi
ya rakaa (nayo) hupungua na kinyume chake pia”. [FAT-HUL-BAARIY: 04/252,
253]
|