Fadhila za swaumu – I
Wapendwa wetu katika imani-Allah aithibitishe imani yenu. Baada ya utafiti
mfupi tulioufanya kwa msaada na taufiq ya Allah, tumegundua kwamba kuna
baadhi ya waislamu hawafungi swaumu ya Ramadhani. Hawafungi kwa sababu
wana udhuru wa kisheria unao wahalalishia kula, la hasha. Bali hawafungi
kwa sababu:
F
Hawakulelewa katika misingi/malezi
ya kidini tangu walipokuwa wadogo, hili likapelekea wao kutokuijua dini
yao na hivyo basi kutokuyathamini maamrisho/makatazo yake.
F
Hawajui ubora/fadhila za ibada
wanazo amrishwa kuzitekeleza.
Kwa
kuzizingatia sababu mbili hizi kuu, tumeonelea ni vema tukaitumia fursa
hii kwa msaada wa Allah, kubainisha baadhi tu ya fadhila za ibada tukufu
ya swaumu. Tukitaraji kuwa, waja wa Allah wakizijua fadhila hizo, ujuzi
wao huo utawasukuma kupania na kujipinda kuzivuna kheri zitokanazo na
ibada hii tukufu ya swaumu ya Ramadhani. Kwa jina lake Taala tunasema:
Katika jumla ya fadhila/ubora wa ibada ya swaumu ni kwamba:
1)
ALLAH TAALA AMEITEGEMEZEA NAFSI
YAKE:
Ibada ya swaumu ndio ibada pekee miongoni mwa
ibada zote iliyopata utukufu wa kuambiwa na Allah Taala: “Swaumu ni yangu
mimi”. Hivyo ndivyo ilivyothibiti katika hadithi – Qudsiy: “Kila amali
ya mwanadamu ni yake yeye ila swaumu, hakika hiyo ni yangu mimi na mimi
ndiye nitakayeilipa”. Muslim-Allah amrehemu.
Kauli hii tukufu ya Allah Taala, kama itakuwa inafahamisha
na kuashiria jambo, basi jambo hilo halitakuwa jingine zaidi ya kuonyesha
utukufu/ubora/daraja na cheo cha ibada hii adhimu ya swaumu. Ni kwa ajili
hii, ndipo pale Abu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-aliposema: Ewe Mtume wa
Allah, niamrishe kufanya amali, Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-akamwambia: “Jilazimishe kufunga, kwani hiyo (swaumu) haina
hesabu (katika malipo yake)”. Muslim-Allah amrehemu.
Na hivyo – Allah ndiye Mjuzi mno – ni kwa sababu ya uficho
wa amali uliomo ndani ya swaumu, kiasi cha kuwa ni siri baina ya Allah na
mja wake tu. Swaumu ni amali ya batini isiyojulikana hakika yake ila na
Allah Taala na ni amali pekee isiyokubali kuingiliwa na riyaa kama ilivyo
kwa baki ya amali nyingine. Kwa mantiki hii, swaumu ndio amali ambayo
ikhlasi hujidhihirisha humo sana kuliko katika amali nyingine. Kipande
hiki cha hadithi ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ni kielelezo
kizuri cha ikhlasi ndani ya swaumu: “...huacha matamanio yake na
chakula chake kwa ajili yangu...”. Kwa hivyo basi, mfungaji huwa
hakusudii wala kulenga lo lote katika swaumu yake zaidi ya kupata radhi ya
Mola wake Mtukufu. Yuko peke yake chumbani, njaa inamkwangua na kiu
kinamuunguza, chakula anacho na maji anayo na hakuna jicho limuonalo. Kwa
nini basi asile wala kunywa?! Ni kwa sababu ya ikhlasi iliyomjaa akilini,
moyoni na mwilini tu basi. Ni ikhlasi hiyo ndio inayompa hisia na imani
kuwa yeye kafunga kwa ajili ya Allah Mola Muumba na sio kwa ajili ya watu.
Sasa ni kweli humo chumbani watu hawamuoni, hata akila au kunywa
hawatajua, lakini Allah Taala aliyemuamrisha kufunga anamuona na ni Yeye
ndiye atakayemlipa juu ya ibada yake hiyo na wala si watu.
2)
MFUNGAJI HULIPWA UJIRA WAKE PASIPO
NA HESABU:
Allah Taala ametaja ujira wa amali nyingine
zisizo swaumu, kwamba mja akitenda amali kadha moja atalipwa kumi mfano
wake mpaka mia saba maradufu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zismhukie-amesema: “Kila mwanadamu hurudufishiwa jema kwa kumi mfano
wake (jema hilo) mpaka mia saba maradufu”. Allah Taala nae akasema:
“...ila swaumu, hakika hiyo (swaumu) ni yangu nami ndiye niilipaye...”
Muslim-Allah amrehemu.
Allah Taala atakapoitawalia jazaa/ujira wa ibada hii ya
swaumu, basi yeye ni Karimu mno ambaye vipawa na upaji wake hauna
ukomo/mpaka. Na hayo ndio malipo/ujira wa wenye kusubiri, kwani hakika
swaumu ni katika subira, Allah Taala amesema: “...NA BILA SHAKA WAFANYAO
SUBIRA (wakajizuilia na maasi na wakaendelea kufanya ya twaa) WATAPEWA
UJIRA WAO PASIPO HESABU”. [39:10] Imamu Auzaaiy-Allah amrehemu amesema:
“Hawatapimiwa (ujira wao) kwa mizani wala kilo, hakika si vinginevyo
watachotewa (tu) mchoto”.
3)
SWAUMU NI KINGA DHIDI YA MATAMANIO
MAOVU:
Ni maumbile ya nafsi ya mwanadamu kupenda mno
kutenda maovu kama alivyosema Allah Taala: “...KWA HAKIKA (kila) NAFSI NI
YENYE KUAMRISHA SANA MAOVU, ISIPOKUWA ILE AMBAYO MOLA WANGU AMEIREHEMU...”
[12:53] Hayo ndio maumbile na matashi ya kila nafsi, kwa kulitambua hilo
ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akatuelekeza kuyavunja na
kuyazima matamanio kwa kutumia silaha ya swaumu, akasema: “Enyi
kusanyiko la vijana! Ye yote miongoni mwenu atakayeweza kuangalia nyumba,
basi na aoe, kwani huko (kuoa) kunalihifadhi mno jicho na kunaipa ngome
tupu. Na asiyeweza (gharama za nyumba), basi na ajilazimishe na swaumu,
kwani hiyo (swaumu) ni kinga kwake (dhidi ya maasi)”. Bukhaariy &
Muslim-Allah awarehemu. Na ni kweli kabisa aliyoyasema Bwana Mtume, kwani
imethibiti kupitia majaribio kwamba swaumu inapunguza matamanio kwa
kiwango kikubwa sana, kama sio kuyakata kabisa.
4)
SWAUMU NI KINGA DHIDI YA KAULI ZA
POROJO NA MATENDO YA KIPUUZI:
Muislamu mkamilifu wa imani ni yule
anayeithamini kila pumzi ya uhai wake, kwa kutambua kuwa hiyo ndio
rasilimali yake. Haipotezi rasilimali yake hii katika baraza za porojo
wala katika kutenda matendo ya kipuuzi yasiyomnufaisha kwa cho chote
katika dunia wala akhera yake. Lakini Allah Taala kwa kutambua kuwa hayo
ndio yapendwayo na mwanadamu, akamuwekea ibada ya swaumu ili impe kinga
dhidi ya mambo hayo yasiyo mnufaisha wala kumfaidisha. Mtume wa
Allah-Rehama na Amani zimshukie-amesema: “...na swaumu ni kinga,
atakapofunga mmoja wenu asiseme maneno machafu siku hiyo na wala
asipayuke. Iwapo mtu atamtukana au kumpiga, basi na aseme hakika mimi
nimefunga”. Muslim-Allah amrehemu.
Mfungaji kukatazwa kusema maneno machafu na kupayukapayuka
hovyo, kuna msaada mkubwa kwake katika kuidhibiti nafsi yake; ulimi,
viungo na moyo wake dhidi ya kutenda maasi.
5)
SWAUMU NI KINGA NA SITARA DHIDI YA
ADHABU KALI YA MOTO:
Sote tunaamini kwamba Allah Taala ameiandaa pepo
na moto (jahanamu) huko akhera. Pepo yake tukufu amewaandalia waja wake
wema watakaoishi hapa duniani kwa kuufuata muongozo wake. Na moto
amaeuweka tayari kwa wale wote watakaoukhalifu muongozo wake huo, tusome:
“TUKASEMA: SHUKENI HUMO NYOTE; NA KAMA UKIKUFIKIENI UWONGOZI UTOKAO
KWANGU, BASI WATAKAOUFUATA UWONGOZI WANGU HUO HAITAKUWA KHOFU JUU YAO WALA
HAWATAHUZUNIKA. LAKINI WENYE KUKUFURU NA KUYAKADHIBISHA MANENO YETU, HAO
NDIO WATAKAOKUWA WATU WA MOTONI, HUMO WATAKAA MILELE”. [2:38-39]
Naam, ni kweli kabisa kuwa adhabu kali ya moto ipo na ipo
kwa ajili tu ya watakao zikhalifu amri za Mola wao. Sasa basi mojawapo ya
mambo yatakayokusaidia kuiepa adhabu kali hii ya moto kwa fadhila zake
Allah ni ibada hii ya swaumu. Kama alivyosema Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie: “Swaumu ni kinga na ni ngome madhubuti dhidi ya
(adhabu ya) moto”. Ahmad-Allah amrehemu. Na katika hadithi nyingine
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Atakayefunga siku
moja katika njia ya Allah, Allah atauepusha uso wake na moto kwa matapo
sabini”. Muslim-Allah amrehemu. Kila swaumu inahesabika kuwa iko
katika njia ya Allah, pale itakapokuwa ni kwa ajili ya Allah tu kama
walivyosema hivyo baadhi ya wanachuoni.
Hali kadhalika, Allah huwaneemesha baadhi ya wafungaji kwa
kuwaacha huru na adhabu ya moto kama alivyosema Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie: “Hakika Allah Taala anao waachwa huru na moto wakati
wa kila kufuturu na hilo (hupatikana) katika kila usiku”. Ahmad-Allah
amrehemu.
6)
SWAUMU NI NJIA YA KUENDEA PEPONI:
Imepokewa kutoka kwa Abu Hurayrah-Allah amuwiye
radhi-kwamba yeye alisema: Ewe Mtume wa Allah, niamrishe jambo
litakalonifaa. (Mtume) akasema: “Shikamana na swaumu, kwani hiyo
(Swaumu) haina mfano wake”. Muslim-Allah amrehemu. Mtume-Rehema na
Amani zimshukie-amebainisha kupitia kauli yake hii, kwamba hapana kitu
kinachomkurubisha zaidi mja kwa Mola Muumba wake na kumuepusha na moto
kama swaumu. Na katika kuonyesha ukarimu wake kwa wafungaji, Allah Taala
akawawekea wafungaji mlango maalumu peponi, ambao humo hataingia ila
mfungaji tu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Hakika
peponi kuna mlango unaoitwa RAYYAAN, wataingia humo wafungaji siku ya
Kiyama. Hataingia humo ye yote asiye wao, patasemwa: Wako wapi wafungaji?
Watainuka, hataingia humo ye yote asiye wao, watakapoingia (mlango)
utafungwa na hataingia humo ye yote”.
Walipostahamili machungu na joto la kiu kwa ajili ya Allah
Taala, nae akawaingiza peponi kupitia mlango huo RAYYAAN, kwani jazaa
hutegemeana na hulingana na amali iliyo tendwa. Na joto linapomzidia
mfungaji ndivyo ujira navyo unavyozidi, Allah atamlipa na kumnywesha
katika siku hiyo ya kiu kali. Imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas-Allah awawiye
radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimtuma Abu Mousa
na sariya (kikosi cha askari) baharini. Basi wakati wako hivyo wakiwa
wameinua tanga katika usiku wa giza, tahamaki wakasikia sauti ikisema:
Enyi watu wa jahazi, simameni nikuambieni hukumu ya Allah aliyoihukumia
nafsi yake. Abu Mousa akasema: “Haya tukhabarishe ikiwa wewe ni
mkhabarishaji. Ikasema (sauti): Hakika Allah Taala ameihukumia nafsi yake,
kwamba ye yote atakayeitia kiu nafsi yake katika siku ya joto kali, Allah
atamnywesha siku ya kiu”. [SAHIHUT-TARGHIYBU WAT-TARHIYBU].
7)
HARUFU YA KINYWA CHA MFUNGAJI NI
NZURI ZAIDI MBELE YA ALLAH KULIKO HARUFU YA MISKI:
Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-amesema: “Naapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad i mkononi
mwake, kwa yakini harufu ya kinywa cha mfungaji yapendeza mno mbele ya
Allah siku ya Kiyama kuliko harufu ya miski”. Hapo zitakapo dhihiri
thawabu za amali kwani huo ndio wakati wa kudhihiri athari ya ibada.
Hadithi hii ya Bwana Mtume, inafahamisha kwamba athari itokanayo na ibada
ni miongoni mwa vitu anavyovipenda Allah Taala. Na hili linatuwekea wazi
mapenzi makubwa ya Allah Taala katika kuipenda amali njema na hali ilivyo
mtumwa hupupia na kupania kutenda kila amali impendazayo Bwana wake ili
apate mkuruba wake.
8)
SWAUMU HURITHISHA MAFANIKIO
DUNIANI NA AKHERA:
Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-anasema: “Mfungaji ana furaha mbili; furaha wakati wa
kufuturu kwake na furaha wakati wa kukutana na Mola wake”. Bukhaariy &
muslim-Allah awarehemu.
Furaha ya muumini mfungaji wakati wa kufuturu kwake
hupatikana kwa ajili ya kufurahikia kuwafikishwa na Allah kuikamilisha
swaumu ya siku hiyo. Na hufurahi pia kwa sababu Allah Taala
amemuhalalishia kula na kunywa na hivyo ni miongoni mwa vitu vinavyopendwa
mno na nafsi. Na huu ni mfano wa ladha na mafanikio ya kweli anayo yapata
muumini kwa sababu ya kumtii kwake Mola wake.
9)
SWAUMU NI MUOMBEZI WA MFUNGAJI
SIKU YA KIYAMA:
Imepokewa kutoka kwa Abdullah Ibn Amrou-Allah
amuwiye radhi-kwamba Mtume-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Swaumu
na Qur-ani vitamuombea mja siku ya Kiyama. Swaumu itasema: Ewe Mola wangu!
Mimi nilimnyima chakula na matamanio yake wakati wa mchana, basi nikubalie
uombezi wangu kwake. Na Qur-ani itasema: Ewe Mola wangu! Nilimnyima kulala
usiku, basi nikubalie uombezi wangu kwake. (Mtume) akasema: Basi
zitakubaliwa uombezi wao”. Ahmad-Allah amrehemu.
10)
SWAUMU NI KAFARA NA KIFUTIO CHA
DHAMBI:
Ibada tukufu ya swaumu inakuwa kafara na
kifutio cha dhambi, kwa sababu inajumuisha na kukusanya ndani yake mema
mengi, na Allah Taala amesema: “...HAKIKA MEMA HUONDOA MAOVU. HUU NI
UKUMBUSHO KWA WANAOKUMBUKA”. [11:114] Na zimepokewa hadithi nyingi
zinazobainisha kuwa swaumu ni kifutio cha dhambi, miongoni mwa hizo ni
kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Fitna ya mtu kwa
mkewe, mali yake na jirani yake, hufutwa na swala, swaumu na sadaka”.
Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Yaani kila makosa anayoyafanya mtu kwa upande wa haki ya
mkewe, wanawe na jirani yake kutokana na maneno yake mabaya au haki za
kimali. Dhambi zitokanazo na makosa hayo hufutwa na thawabu za ibada ya
swala, swaumu na sadaka. Na swaumu ya Ramadhani ndio inayokhusika zaidi
na ufutaji wa dhambi, kama lilivyothibiti hili katika kauli ya
Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Atakayefunga (swaumu ya) Ramadhani
kwa imani na kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah, atasamehewa dhambi zake
zilizotangulia”. Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Na katika hadithi nyingine, Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-amesema: “Swala tano (swala ya) Ijumaa mpaka Ijumaa na
(swaumu ya) Ramadhani mpaka Ramadhani, ni kafara ya madhmabi yaliyo baina
yao pale yatakapoepukwa madhambi makubwa”. Muslim-Allah amrehemu.
Kwa kauli hii ya Bwana Mtume, inatuwazikia kumbe swaumu
hufuta madhambi madogo madogo na wala sio yale makubwa. Madhambi makubwa
hayafutwi ila na toba, Allah Taala anasema: “KAMA MKIJIEPUSHA NA MAOVU
MAKUBWA MNAYOKATAZWA. TUTAKUFUTIENI MAKOSA YENU MADOGO NA TUTAKUINGIZENI
MAHALI PATUKUFU (kabisa, napo ni peponi)”. [4:31]
Hadithi mbili tulizozinukuu na aya hii tukufu
zimefahamisha kwamba ili kuyapata maghfira (msamaha) ya Allah, ni lazima
zipatikane sharti tatu hizi zifuatazo:
i.
Kufunga swaumu ya Ramdhani kwa
kumuamini Allah na Mtume wake na kusadikisha ufaradhi wa ibada ya swaumu
na ujira aliowaandalia Allah waja wake wafungaji.
ii.
Afunge Ramadhnai kwa kutarajia
ujira kutoka kwa Allah Taala ilhali akiwa mwenye ikhlasi kwake.
iii.
Kujiepusha na madhambi makubwa, na
haya ni kila dhambi ambayo inapotendwa huandamiwa na adhabu “haddi” hapa
duniani au makamio akhera au na ghadhabu au laana ya Allah na mfano wake.
Madhambi ya namna hiyo ni kama vile shirki, kula riba, kula mali ya
yatima, zinaa, uchawi, kuua, kuwaasi wazazi, kukata udugu, kutoa ushahidi
wa uongo, ghushi (utapeli), kusengenya, kuficha haki na kadhalika.
Naam, ndugu mpendwa katika Allah, tayari umekwishaona
fadhila/ubora wa swaumu ya mwezi mtukufu wa Ramadhani. Hebu sasa na
tujiulize:
Je, ni
swaumu ipi ndio inaweza kumpatia muislamu fadhila hizi adhimu?
Fadhila zote ambazo tumezitaja kuwa zinapatikana ndani ya ibada ya swaumu
ya mwezi mtukufu wa Ramadhani, hatazipata ila yule atakayefunga kwa sharti
zifuatazo:
i.
Awe na ikhlasi katika swaumu yake;
yaani afunge tu kwa ajili ya Allah Taala, hasikusudie ila kupata radhi za
Allah. Asifunge kwa ajili ya kuonekana/kusifiwa na watu, kwa ujumla
asifunge kwa ajili ya kupata malengo yake ya kudunia.
ii.
Swaumu yake yote ifuate muongozo
wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-; yaani afunge kama
alivyofundisha Bwana Mtume.
iii.
Viungo vyake navyo vyote vifunge;
yaani avizuie na yale yote yaliyoharamishwa. Ulimi wake ufunge, usiseme
uongo, kusengenya, kutoa maneno machafu na.... na.... Jicho lake nalo
lifunge, lisiangalie vilivyo haramishwa. Sikio nalo pia lifunge,
lisisikilize muziki na kila lililo haramishwa. Mkono nao pia ufunge, usile
haramu, usipige pasina haki na mguu nao ufunge, uuzuie kwenda katika mambo
ya haramu. Na haya ndio malengo makuu ya ibada ya swaumu, kwa ajili hii
basi swaumu imekuwa ndio chuo cha kulea nafsi katika mambo matukufu/mema
na kumuepusha na mambo maovu/mabaya.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema:
“Ambaye hakuacha maneno ya uongo na kuyafanyia kazi na (hakuacha) upuuzi,
basi Allah hana haja katika kuacha kwake chakula na kinywaji chake”.
Muslim-Allah amrehemu.
Na
katika hadithi nyingine, amesema: “Huenda mfungaji, fungu lake katika
swaumu yake (likawa ni) njaa (tu) na kiu. Na huenda msimamaji (usiku
kufanya ibada), fungu lake kutokana na kisimamo chake hicho (likawa) ni
kukesha (tu)”. Ahmad-Allah amrehemu.
|