Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

KHABARI ZA AL-ASWAD

 Faida

SOMO LA TATU.

     I.        Khabari za Al-Aswad:

         Waislamu walipo ifungua nchi ya Yemen na kuwa chini ya himaya ya mamlaka ya Kiislamu, katika zama za Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Mtume akamtawadha Baadhaan Al-Faarisiy kuwa gavana wa Yemen, huyu ni Mfursi wa Iran ambaye alipelekwa Yemen na Kisraa (mfalme) Abrawiyz kuwa gavana huko kwa niaba yake. Akaendelea kumuwakilisha Kisraa huko mpaka Mtume wa Allah alipo twaa madaraka ya huko, nae ndiye aliye funga ukurasa wa magavana wa Kifursi walio itawala Yemen. Baada ya utawala wa Yemen kuangukia mikononi mwa waislamu, Baadhaan akasilimu na ndipo Mtume akambakisha katika wadhifa wake wa ugavana. Na makao yake makuu yalikuwa katika mji wa Sanaa. Aliendelea na wadhifa wake huo mpaka alipo fariki dunia. Alipo kufa Mtume wa Allah akayagawanya madaraka yake. Akampa ugavana wa mji wa Yemen mwanawe; Shahri Ibn Baadhaan. Abu Mousa Al-Ash’ariy akatawazwa kuwa gavana wa mji wa Ma’arab. Ugavana wa mji wa Hamdaan akapewa Aamir Ibn Shahri Al-Hamdaaniy, mji huu ulikuwa mashariki mwa Yemen. Twaahir Ibn Haalah akatawalishwa kwa makabila ya Aki na Ash-ariyin, ukoo wa Aki ulikuwa ukiishi baina ya miji ya Zabeed na Rumui. Na huyu mzee Aki ni mtoto wa Adnaan. Na Waash’ari walikuwa wakiishi kaskazini mwa mji wa Zabeed na wananasibishwa na Ash’ari Ibn Adad Ibn Zaid Ibn Yashjab Ibn Ariyb Ibn Zaid Ibn Kahlaan. Khalid Ibn Said Ibn Al-Aaswi yeye akapewa ugavana wa eneo lililo baina ya miji ya Najiraan, Rumui na Zabeed. Amrou Ibn Hazm akawa gavana wa Najiraan, mji wa Hadharamout akatawalishwa Ziyaad Ibn Labeed Al-Bayaadhiy. Ukaashah Ibn Thaur akasimikwa ugavana wa makabila ya Sakaasik na Sukuun, haya ni makabila ya Kandah yaliyo kuwa yakiishi kaskazini mwa mji wa Hadharamout. Al-Muhaajir Ibn Umayah ndugu wa mama wa waumini; Ummu Salamah, akateuliwa kuwa gavana wa ukoo wa Muawiyah. Lakini hakwenda kukalia kiti chake hicho mpaka Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo fariki, kwa sababu ya maradhi aliyo kuwa nayo. Ziyaad Ibn Labeed akakaimu ugavana kwa niaba yake. Ya’alaa Ibn Umayah yeye akapewa ugavana wa Al-Jundi. Muaadh Ibn Jabal akapewa wadhifa wa ualimu, akawa akiuzungukia mji baada ya mwingine.

Muda mchache kabla ya kifo cha Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-mtu mmoja wa kabila la Unsi aitwaye Ab-halah. Mwenye lakabu ya “Dhul-Khimaar”, akijulikana zaidi kwa jina la Al-Aswad, akaleta machafuko Yemen kwa kudai utume. Madai yake hayo yakaitikiwa kwa mikono miwili na watu wa kabila la Mudh-haj. Alipo pata uungwa mkono huu, akaenda kuuvamia mji wa Najiraan akamng’oa madarakani gavana wake; Amrou Ibn Hazmi. Pia akamuondosha madarakani Khalid Ibn Said Ibn Al-Aaswi, magavana wawili hawa wakatoroka wakaenda Madinah. Al-Aswad hakuushia hapo, akatoka na watu mia saba wa kabila lake, wakaelekea Sanaa. Huko akamuua gavana  Shahri Ibn Baadhaan na kukalia kiti chake na akamuoa kwa nguvu mjane wa marehemu. Akatawalia eneo lote lililo baina ya Sanaa na Hadharamout kwa upande wa Kaskazini mpaka Bahrein kwa upande wa Mashariki. Nguvu yake ikawa kubwa, Muaadh Ibn Jabal kuona hivyo akatoka hali ya kukimbia, akampitia Abu Mousa katika mji wa Ma’arab. Akatoka pamoja nae, wakaenda Hadharamout, Muaadh akashukia katika kabila la Sakaasik na Abu Mousa akawa mgeni wa kabila la Sukuun. Gavana Twahir Ibn Abu Haalah, yeye akabakia katika mji wa kabila la Aki.

Khabari za tukio hilo zilipo mfikia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawapelekea ujumbe vijana wa Kiislamu wa Yemen, na magavana Abu Mousa, Muaadh na Twahir. Ya kwamba wachukue jukumu la kumuua Nabii wa uwongo; Al-Aswad. Vijana Feiruz na Daadhawiyhi wakalibeba jukumu hilo, wakapanga mipango ya kumuua wakisaidiwa na mke wake ambaye alimuoa kwa nguvu baada ya kumuua mumewe; gavana Shahri Ibn Baadhaan. Hata mipango ilipo iva, wakafanikiwa kumuua usiku, Feiruz ndiye aliye muua usiku. Kulipo pambazuka asubuhi wakapiga mbiu mgambo ya Kiislamu, nayo ni adhana, waislamu wakaja kama mawimbi ya bahari. Kuona hivyo, wafuasi wa Al-Aswad wakawakwapua baadhi ya watoto wa waislamu kama ngao, wakatoka mjini wakiwaacha nyuma wengi miongoni mwa watoto wao. Kisha pande mbili hizi; kundi la Mtume wa haki na lile la Mtume wa uwongo, zikatumiana ujumbe ya kwamba kila upande urejeshe watoto wa upande mwingine. Baada ya kutekelezwa matakwa haya kwa kila upande, wafuasi wa Al-Aswad wakawa wakitangatanga baina ya Sanaa na Aden.

Baada ya hali kurejea shwari, magavana wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakarejea kwenye nyadhifa zao. Na wakawafikiana ya kwamba mwalimu Muaadh ashike makamu ya kuwaswalisha watu Sanaa kufuatia kuuawa kwa gavana wake; Shahri mpaka yaje maelekezo mengine kutoka kwa Mtume wa Allah. Wakapeleka taarifa za kadhia yote Madinah; makao makuu ya Dola ya Kiislamu. Mjumbe akawasili Madinah ilhali tayari Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akiwa ameshaaga Dunia na khalifa Abu Bakri kushika makamu yake. Ikawa hii ndio khabari njema ya kwanza ya ushindi wa Uislamu kumfikia Amirul-Muuminina; Abu Bakri.

Khabari za kifo cha Mtume zilipo tangaa, Qays Ibn Abdi Yaghuuth akaritadi na akawaandikia waraka washindwa katika jeshi la mtume wa uwongo; Al-Aswad. Wakajikusanya kwake, akala njama ya kuwaua wakubwa wa vijana, nao Feiruz, Daadhawiyhi na Khashanshi. Akawaandalia karamu, akawaalika wote ili apate kuwaua kwa hila, akafanikiwa kumuua Daadhawiyhi na wenzake wawili wakaponyoka. Akatoka kuwafuatia, nao wakakimbia na kwenda kuomba hifadhi kwa kabila la Khaulaan. Hapo ndipo zilipo komelea mbio za Qays, akarejea Sanaa akajiimarisha hapo. Akaziendea familia za vijana wale, akawaghuri na kuwatoa Yemen barani na baharini na kuwatishia amani. Feiruz alipo pata khabari hizo akakusudia kumpiga vita, akaomba msaada kwa makabila ya Aqeel Ibn Rabeeah na Aki. Wakamuendea na kufanikiwa kuzikomboa familia alizo kuwa ameziteka Qays na kuwaua watu wake alio kuwa nao.

Baada ya kumalizika kwa zoezi hilo, wakaelekea kwa Feiruz, akawaongoza kupambana na Qays na watu wake mpaka wakawashinda. Na ni katika kipindi hicho aliwajia Muhaajir Ibn Umayah ambaye Sayyidna Abu Bakri alimsimikia bendera na kumpeleka kupambana na majeshi ya Al-Aswad na kuwasaidia wale vijana. Na akafuatiwa na Ikrimah Ibn Abu Jahli baada ya kumaliza kazi aliyo tumwa kuifanya Oman na Mahrah. Wote wawili hawa wakawasaidia vijana kupambana na majeshi ya Qays Ibn Abdi Yaghuuth. Wakapigana nao mpaka wakawashinda na kuwatwaa mateka Qays na Amrou Ibn Ma’ad Yakrib Az-zabeediy ambaye alikuwa ameritadi na kumfuata Al-Aswad. Wakawapeleka Madinah kwa khalifa Abu Bakri-Allah amuwiye radhi.

Walipo fikishwa kwa khalifa Abu Bakri, akasema: Ewe Qays! Umewaua waja wa Allah na ukawafanya waritadi kuwa ndio watu wako wa karibu na wasiri wako kinyume na waumini. Qays akakanusha kushiriki kwa lolote katika kadhia ya Daadhawiyhi na haukuwepo ushahidi wa wazi juu ya kumuua kwake, kwa sababu mauaji yake yalikuwa ni ya kificho. Kwa unakushi wake huo na kwa kukosekana kwa ushahidi wa moja kwa moja utakao mtia hatiani, akawa amejikosha na damu ya Daadhawiyhi iliyo mwagika. Na akamwambia Amrou Ibn Ma’adi Yakrib; Hivyo wewe huoni haya kwamba wewe kila leo ama unashindwa au unatekwa! Lau ungeli inusuru dini hii, bila ya shaka Allah angeli kunyanyua daraja ya juu. Akasema: hapana ubaya, ninakubali makosa na sitarudia tena. Baada ya kukiri huku, Amirul-Muuminina; Abu Bakri akawaacha huru, wakarejea kwa jamaa zao hali ya kuwa ni waumini.

Baada ya hapo Al-Muhaajir Ibn Abu Umayah akayafuatilia mabaki ya jeshi la Al-Aswad kila mahala na kuyafyekelea mbali kwa kila njia. Ili yasiweze kusimama tena na kuleta usumbufu kwa waislamu. Na kipindi cha nabii huyu wa uwongo; Al-Aswad tangu alipo dai utume mpaka anauawa, ilikuwa ni miezi minne takriban. [Rejea AL-KAAMIL FIT-TAAREEKH 2/231 na AL-BIDAAYAH WAN-NIHAAYAH 4/702].

 

 



 | Tuandikie |