|
II.
Khabarari za Kandah:
Watu wa Kandah walikuwa wameritadi katika zama za
Nabii wa uwongo; Al-Aswad. Waliliritadi kwa sababu ya yaliyotokea baina yao
na gavana Ziyaad Ibn Labeed katika kadhia ya faradhi ya Zakah. Kadhia hii
ilitokana na makadirio ya zakah yaliyo kosewa na ikachochewa na watu wa
kabila la Amrou Ibn Muawiyah hapo Kandah. Kwa sababu ya uritadi wao huu,
ndipo gavana Ziyaad akakata shauri la kuwapiga vita, akawapiga na
kuwashinda.
Baniy Muawiya wote wa Kandah wakawafikiana na kukongamana
kuacha kutoa fungu la Zakah, ila Shurahbeelah Ibn As-samtw na mwanawe. Kwani
wawili hawa waliwaambia Baniy Muawiya: “Hakika ni jambo baya kwa watu
waungwana kubadili walicho kikubali. Hakika watu watukufu hujilazimisha na
jambo la shubuha basi hupata utukufu kwa kuhamia jambo lililo wazi zaidi
kuliko hilo (la shubuha). (Hufanya hivyo) kwa kuchelea aibu. Basi je, ni
vipi (inakuwa) kuliacha jambo zuri na jema na kuiendea batili iliyo mbaya!
Ewe Mola wa haki! Hakika sisi hatuiungi mkono kaumu katika hili”. Baada ya
kwisha kuwaambia jamaa zao maneno hayo yenye busara na nasaha njema,
wakaondoka kwenda kwa Ziyaad. Wakamwambia gavana: “Washambulie usiku watu
hawa, ukitofanya hivyo tunachelea watu wasije wakachangukana nasi”.
Gavana Ziyaad kwa kuyazungatia maslahi ya uma, akaukubali
ushauri wa Shurahbeelah na mwanawe. Akaandaa jeshi lake na kwenda kupambana
nao katika ngome zao, akawakamata wafalme (viongozi) wao na akawaua. Na
wakakimbia wale walio weza kukimbia, Waislamu wakarejea salama wakiwa
wamepata ngawira na mateka. Wakati wa kurejea kwao huku, wakapita kwenye
ngome za Al-Haarith Ibn Muawiyah (hawa ni miongoni mwa wale walio ipinga
faradhi ya Zakah). Miongoni mwao alikuwemo Ash-ath Ibn Qays, huyu akaja
akawanyang’anya Waislamu mateka wao. Gavana Ziyaad akachukua hatua za haraka
kwa kumuandikia waraka wa kumuita haraka Al-Muhajir Ibn Abi Umayyah; gavana
wa Baniy Muawiyah wa Kandah. Al-Muhajir akampa ukaimu wa jeshi lake Ikrimah
na yeye akatoka wangu wangu na watu wake mpaka akafika kwa Ziyaad. Wote kwa
pamoja wakayaunganisha majeshi yao na kupambana vikali na waritadi wale.
Baniy Al-Harith wakashindwa vibaya, wakakimbia na kwenda kujificha Najeer;
hii ni ngome yao. [Rejea AT-TWABAQAATUL-KUBRAA 6/22]
Waislamu wakawazingira, mzingiro ulipo shitadi na hali kuwa
ngumu, waliamua kutoka ngomeni na kupambana mpambano ambao haukuwafaa kwa
lolote. Wakalazimika kurudi tena kujificha ngomeni, kisha ndipo As-ath
akamtuma mjumbe kwa Waislamu kutaka kufanya nao suluhu. Katika suluhu hiyo,
wao wataisalimisha ngome hiyo na vyote vilivyomo humo kwa Waislamu, kwa
sharti la kupewa amani kwa viongozi tisa. As-ath akaandika tamko la suluhu
hii na akayaorodhesha majina ya viongozi anao taka wapewe amani na Waislamu,
lakini akasahau kuliorodhesha jina lake mwenyewe. Waislamu wakaikubali
suluhu hiyo, wakaingia katika ngome hiyo, wakawaua askari wapiganaji,
wakachukua mateka na ngawira. Kisha wakaangalia orodha ya watu walio ombewa
amani katika waraka wa suluhu, tahamaki jina la Ash-ath halimo. Al-Muhajir
akataka kumuua, lakini wafuasi wake wakamshauri asimuue na badala yake
ampeleke kwa khalifa Abu Bakri, yeye kama Amiri wa waumini ndiye aamue
hatima yake. Akaukubali ushauri huo wa wafuasi wake na akampeleka kwa
Sayyidna Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-nae akamsamehe na kumuacha huru.
Ash-ath huyu baadae alikuwa ni miongoni mwa Waislamu walio onyesha ushujaa
mkubwa katika ufunguzi wa Iraq.
Mpaka hapa, ewe ndugu mwema-Allah akurehemu-khabari za
waritadi zinakoma. Kutokana na khabari hizi, Waislamu wanao taka kufuata
nyayo za wahenga wao wema, wanapata somo kwamba muumini hatakiwi kuwa
dhalili vyovyote watakavyo kuwa wengi maadui zake. Kwa sababu Waislamu
hawashindwi kwa sababu ya uchache wao na wala hafedheheki ila ni kwa kufuata
kwao matamanio maovu ya nafsi zao. Na kwa sababu ya kukengeuka kwao,
wakaacha kuifuata njia ya sawa.
Huyu hapa Sayyidna Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-khalifa wa
kwanza wa Waislamu. Waarabu wote walikuwa dhidi yake, maadui zake, basi
akawa yeye na wote walio kuwa pamoja nae ni kama mwenge angavu ndani ya
pango lenye kiza totoro. Basi hilo la kuwa na mahasimu kila pembe,
halikumzuia yeye pamoja na Waislamu walio simama nae imara kuitukuza dini ya
Allah na kupigana na wale walio mkufuru Allah. Bali aliamini kwa yakini
kabisa ahadi ya Allah pale alipo sema: “ENYI MLIO AMINI! MKIMNUSURU ALLAH
NAE ATAKUNUSURUNI NA ATAITHIBITISHA MIGUU YENU”. [47:07] – Yaani mkiinusuru
dini ya Allah, na Yeye atakunusuruni muwashinde maadui zenu na ayatilie
nguvu mambo yenu.
Kwa imani yake hiyo, Allah Ataadhamiaye akamlipa kwa kumpa
nusura adhimu dhidi ya maadui zake na ushindi mkubwa akaupata, Uma wote wa
Kiarabu ukawa chini ya utii wake. Hivyo ndivyo unavyo kuwa Uislamu na Imani,
tanabahi na uzingatie!
III.
Suala (kadhia) la Iraq:
Sayyidna Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-alipo maliza
kuwashughulikia waritadi na kufanikiwa kuwakusanya Waarabu wote chini ya
Uislamu na Allah akalifanya neno lao kuwa moja. Akaielekeza hima yake katika
kuuneza uadilifu na usawa wa Uislamu miongoni mwa mataifa mengine. Ambayo
wafalme wake walikuwa wakiitakidi kwamba wao wako katika daraja ya juu
kuliko raia zao. Kwa itikadi yao hii, wakawasawirisha fikirani/akilini mwao
kuwa ni watumwa wao wasio na mamlaka yoyote na nafsi zao. Natija ya taswira
ovu hii ikawa ni kuamiliana nao kwa dhuluma na jeuri kubwa.
Tawala/falme kubwa zilizo jiranikiana na Dola ya Kiislamu
enzi hizo, ulikuwa ni ufalme wa Fursi kwa upande wa Mashariki na ufalme wa
Urumi kwa upande wa Kaskazini. Akaamua kuanza na Fursi na tukio la mwanzo
lililo tokea baina ya Waislamu na dola hii kubwa, ni ule waraka wa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alio muandikia Kisraa (mfalme) Abrawiyzi
akimlingania Uislamu. Kisraa akauchana chana waraka huo wa Mtume kwa
ujivuni, jeuri na kiburi. Kitendo chake hiki kinakuonyesha kiwango cha jeuri
na kiburi topea ambavyo ndivyo vilikuwa nembo ya wafalme enzi hizo, dini ya
haki ikaja kuyaondosha mambo mabaya haya. Jeuri ya Abrawiyzi kwa waraka huu
wa Mtume, ilimfikisha kumpa amri gavana wake wa Yemen; Baadhaan atume watu
wawili mashujaa, weledi wa vita wakamkamate na kumleta mbele yake Mtume.
Gavana akaipokea amri hiyo, akawatuma watu wawili nao wakaenda kama walivyo
amrishwa. Watu wawili hao walipo fika Madinah, walipokelewa na Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawaambia: “Leo ameuawa Abrawiyzi,
ameuawa na mwanawe”. Na hali ikawa kama alivyo ieleza Mtume wa Allah,
kwani Shairawaihi alimpindua kwa msaada wa wakuu wa Fursi, akamuua na
kukalia kiti cha ufalme wa Fursi. [Rejea AL-BIDAAYATU WAN-NIHAAYAH 4/269].
Watu wawili hao walipo tambua kuwa ni kweli maneno waliyo
ambiwa na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakasilimu. Na
Shairawaihi (Kisraa mpya) akamtumia ujumbe gavana Baadhaan ya kwamba
asimbughudhi Mtume wa Allah.
Na katika zama zake Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-nchi ya Yemen ilifunguliwa na Baadhaan akasilimu, hapo Mtume
akamtawaza kuendelea kuwa gavana wake. Yemen ikawa ndio nchi ya kwanza iliyo
kuwa chini ya himaya ya Fursi, kujiunga na Uislamu. Kisha zikafuatia baada
yake Bahrein na Oman ambazo nazo pia zilikuwa chini ya Fursi. Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo fariki na khalifa Abu Bakri kumaliza
kupambana na waritadi. Akamteua Sayyidna Khalid Ibn Al-Waleed; panga la
Allah kuwa mtu wa kwanza atakaye asisi misingi ya dini nyoofu katika nchi za
Fursi. Uteuzi huu ulifanyika mwanzoni mwa mwezi wa Muharram (Mfunguo nne) wa
mwaka wa 12 Hijiria. [Rejea AL-BIDAAYATU WAN-NIHAAYAH 4/739 na
TAARIKHUT-TWABARIY 2/332].
Na akamuamuru kuanza na Ubullah (mojawapo ya ngome za Fursi
iliyo kuwa katika Ghuba ya Kiarabu kwenye maporomoko ya mto Dajlah) na
akamuongezea nguvu kwa kumpa msaidizi, Al-Qa’aqaa Ibn Amrou. Na akamteua
Iyaadhw Ibn Ghanam kuishambulia Fursi kwa kutokea Kaskazini mwa Iraq na
akamuamuru kuanza na Muswayakh (kijiji kilicho kuwa pembezoni mwa mto
Furaat, Kaskazini mwa Iraq). Na akamuongezea nguvu kwa kumpa usaidizi wa
Abdi Yaghuuth Al-Humeiriy, akawaamuru kuwatolea wito wa kutoka pamoja
nao, wale walio pigana na waritadi. Na kwamba wasishirikiane pamoja na
waritadi, kwani maoni yake Khalifa Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-yalikuwa ni
kutotaka msaada wa kijeshi kwa mritadi.
|